Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wateteaji wa Kweli

Wateteaji wa Kweli

Kuhitimu kwa Darasa la 132 la Gileadi

Wateteaji wa Kweli

MACHI 10, 2012, ilikuwa siku ya pekee katika kituo cha elimu cha Mashahidi wa Yehova huko Patterson, New York. Maelfu ya watu waliovalia vizuri, kutia ndani wageni kutoka nchi za kigeni, walikusanyika pamoja ili kuhudhuria programu ya kuhitimu kwa darasa la 132 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Watu wengi walikusanyika katika ukumbi ulio Patterson; wengine walikusanyika ili kutazama programu hiyo katika sehemu nyingine zilizounganishwa kwa mfumo wa video. Kwa ujumla, watu waliohudhuria walikuwa 9,042.

Wengi walitamani kujua jinsi ambavyo mambo yangekuwa. Tofauti na madarasa yaliyotangulia, wanafunzi wote waliokuwa wakihitimu tayari walikuwa katika aina fulani ya utumishi wa pekee wa wakati wote—walikuwa wakitumika kama Wanabetheli, mapainia wa pekee, waangalizi wanaosafiri, au wamishonari—ingawa hawakuwa wamehudhuria Shule ya Gileadi. Wanafunzi hao wenye uzoefu wangeambiwa nini?

Wasikilizaji hawakuhitaji kusubiri kwa muda mrefu ili kupata jibu. Gerrit Lösch, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alikuwa mwenyekiti wa programu hiyo na alitoa hotuba ya kwanza. Aliuliza swali lenye kuchochea fikira, “Je, Wewe Ni Mteteaji wa Kweli?” Alieleza kwamba Wakristo ni wateteaji wa kweli, wanaotetea mafundisho yote ya Kikristo. Kutetea kweli hakutii ndani tu kuwafundisha watu ukweli bali pia kuwasaidia watu wapende kweli.

“Tunajuaje kwamba tuna ukweli?” aliuliza Ndugu Lösch. Alisema uthibitisho haupatikani tu kupitia idadi ya watu wanaoikubali kweli. Ingawa leo kuna mamilioni ambao wameikubali ibada safi, kulikuwa na watu wachache tu katika Pentekoste 33 W.K. Kisha, akataja njia tano zinazotuthibitishia kwamba tuna ukweli: (1) Tunafuata mafundisho ya Yesu, (2) tunapendana, (3) tunafuata viwango vya juu vya maadili ambavyo Mungu ametuwekea, (4) hatuungi mkono upande wowote katika mizozo ya ulimwengu huu, na (5) tunaitwa kwa jina la Mungu.

“Tii na Ufuate Mwongozo”

Wahudhuriaji walishangaa walipomwona Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, akitembea kuelekea kwenye kinara huku akiwa amebeba sanduku la kubebea nguo! Kichwa cha hotuba yake kilikuwa “Tii na Ufuate Mwongozo,” kilichotegemea Isaya 50:5. Andiko hilo linatabiri hivi kumhusu Yesu Kristo: “Nami kwa upande wangu sikuwa mwasi. Sikugeuka upande ulio kinyume.”

Ndugu Jackson aliwatia moyo wanafunzi watii bila kukawia mwongozo unaotolewa na Yehova kupitia roho yake takatifu, Biblia, na tengenezo lake. Katika mfano wa talanta, ulio katika Mathayo 25:14-30, kila mtumwa alipewa kulingana na uwezo wake. Walipaswa kujitahidi kufanya yote wawezayo. Watumwa wawili walipongezwa na wakaitwa watumwa ‘wema na waaminifu.’ Si lazima uaminifu uonekane kupitia matokeo bali kwa kutii na kufuata mwongozo.

Mtumwa wa tatu aliitwa “mwovu na goigoi” na “asiyefaa kitu.” Alikuwa na tatizo gani? Aliizika talanta yake. Talanta haikuwa sarafu, bali kipimo cha uzito kinacholingana na dinari 6,000, chenye uzito wa kilo 20. Huo ni uzito unaokaribia uzani ambao mtu anaruhusiwa kubeba katika sanduku anaposafiri kwa ndege. Mtu angehitaji kufanya kazi ili kuzika kifaa kinachotoshana na sanduku. Basi yule mtumwa alifanya jambo fulani—aliizika ile talanta—​lakini hakuagizwa afanye hivyo. Vivyo hivyo mmishonari anaweza kuwa na shughuli nyingi, lakini anashughulikia nini? Je, ni kuandika barua ndefu, kutembelea vituo vya Intaneti, kukutana na marafiki, au kufanya biashara? Mtu kama huyo anaweza kuwa mchovu sana baada ya siku kwisha kwa sababu ya kufanya mambo kama hayo, lakini hakufanya mambo aliyoagizwa. Ndugu Jackson alimalizia kwa kusema: “Fuateni mwongozo sikuzote!”

“Epuka Kuwa na Shaka”

Hicho ndicho kichwa cha hotuba iliyotolewa na Anthony Morris wa Baraza Linaloongoza. “Biblia haihusianishi kamwe imani na shaka,” akasema. “Imani huondoa shaka.” Shetani alifaulu kutia shaka katika akili ya mwanamke mkamilifu, Hawa, basi anaweza kutia shaka katika akili yetu. “Lisha imani yako, na hutakuwa na shaka kamwe,” akasema Ndugu Morris. Alikazia simulizi kuhusu Petro ambaye ‘alitembea juu ya maji’ lakini ‘alipoitazama ile dhoruba ya upepo,’ akaogopa na akaanza kuzama. Baada ya Yesu kumshika akamuuliza hivi: “Kwa nini umekuwa na shaka?” (Mathayo 14:29-31) “Ingawa ninyi wamishonari mtakuwa na shughuli nyingi katika utumishi wa wakati wote, wengine watashangazwa na mambo mtakayofanya, ni kana kwamba mnatembea juu ya maji, lakini dhoruba itakapopiga, msiruhusu muwe na shaka.”

Ndugu Morris aliendelea kusema kwamba, ingawa inaweza kuwa vigumu kukabiliana na hali zenye dhoruba, mwishowe upepo huacha kuvuma. Kuhusiana na nyakati ngumu, aliwahimiza wanafunzi wafikirie jambo ambalo Paulo na Sila walifanya walipokuwa gerezani huko Filipi. Andiko la Matendo 16:25 linasema hivi: “Karibu na katikati ya usiku Paulo na Sila walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo; ndiyo, wafungwa walikuwa wakiwasikia.” Ona jambo hili: Hawakusali tu bali pia waliimba. Waliimba kwa sauti ya juu hivi kwamba wafungwa wengine waliwasikia. Ndugu Morris alisema kwamba wengine wetu si waimbaji stadi, lakini hatupaswi kuogopa kuimba, hasa tunapokabiliana na hali ngumu. Ndugu Morris alimalizia kwa kusoma maneno ya Wimbo namba 135 wenye kichwa “Kuvumilia Mpaka Mwisho,” katika kitabu cha nyimbo Mwimbieni Yehova.

Hotuba Nyingine Zenye Kutia Moyo

“Je, Utapenda Siku za Kutosha?” Hicho kilikuwa kichwa cha hotuba iliyotolewa na Robert Luccioni, wa Idara ya Ununuzi. Kichwa hicho kilitegemea maneno ya Mfalme Daudi yaliyo katika Zaburi 34:12. Hotuba ya Ndugu Luccioni ilionyesha jinsi ya kukabiliana na hali ngumu na wakati uleule kudumisha uhusiano mzuri na Yehova. Tunaweza kujifunza mambo mengi kutokana na simulizi lililo katika andiko la 1 Samweli sura ya 30. Wakati Daudi, wanaume wake, na familia zao walipokuwa wakimkimbia Mfalme Sauli, waliishi uhamishoni Siklagi. Familia zao zilipovamiwa na kutekwa na Waamaleki, wanaume hao walimlaumu Daudi na walitaka kumpiga mawe. Daudi alitendaje? Hakuvunjika moyo bali “akajitia nguvu kwa Yehova Mungu wake.” (1 Samweli 30:6) Alimwomba Yehova ampe mwongozo na akafuta mwongozo wa Mungu, kisha akawakomboa watu waliokuwa wametekwa. Msemaji aliwahakikishia wanafunzi kwamba ikiwa watamtegemea Yehova kwa njia hiyo, na kutii mwongozo wake, watapenda siku za kutosha kuona mema. Watakuwa na maisha yenye furaha katika pendeleo lenye thamani ambalo wamepewa.

“Kazieni Macho Mchana Ulio Mbele Yenu.” Hicho kilikuwa kichwa cha hotuba iliyotolewa na Ndugu Michael Burnett, mmoja wa walimu wa Shule ya Gileadi. Waisraeli waligawa usiku katika vipindi vitatu vya kulinda, kutoka machweo mpaka mapambazuko. Kila kipindi kilikuwa na urefu wa saa nne. Kipindi cha mwisho kilianza saa 8 usiku mpaka saa 12 asubuhi, kilikuwa chenye giza zaidi, chenye baridi kali, na ilikuwa vigumu kukaa macho. Mtunga-zaburi alijaza akili zake na maneno ya Yehova ili wakati wa kipindi cha mwisho cha kulinda asilemewe na usingizi. (Zaburi 119:148) Ndugu Burnett aliwaambia hivi wanafunzi: “Mtahitaji kuwa macho. Mtakabiliana na siku za giza zenye kuvunja moyo na mtaona athari za ulimwengu wenye baridi na usio na upendo. Mnahitaji kuamua mapema hatua mtakazochukua ili kukabiliana na hali hizo zenye kuvunja moyo.” Kisha akawakumbusha kwamba wanapaswa kuendelea kujifunza mambo mazito yaliyo katika Biblia ili waendelee kukaa macho kiroho. Ndugu Burnett alitoa mfano huu ili kukazia jambo hilo: “Kila siku unasali kwa Yehova kwa sababu unataka awe rafiki yako. Kwa hiyo, acha Yehova akiwa rafiki yako azungumze nawe kila siku kupitia kurasa za Biblia. Usiku umesonga sana, hivyo panga jinsi utakavyotumia siku zako, na kwa kufanya hivyo utaendelea kukazia macho mchana ulio mbele.”

“Mmezoezwa kwa Ajili ya Kazi Iliyo Mbele Yenu.” Hotuba hiyo iliyotegemea andiko la 1 Petro 5:10, ilitolewa na mwalimu mwingine wa Gileadi anayeitwa Mark Noumair. Aliwauliza wanafunzi swali hili: “Kwa kuwa ninyi ni wahudumu wenye uzoefu, kwa nini mlialikwa kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower?” Jibu: “Kwa sababu mna ustadi katika kazi yenu. Watu wengi wenye ustadi hutumia muda fulani ili kuhudhuria masomo ya kuboresha ujuzi wao. Katika kipindi cha miezi mitano iliyopita Yehova amekuwa ‘akiwaimarisha’ na kuwatia ‘nguvu’ kupitia kujifunza Neno lake na kujifunza kuhusu tengenezo lake ili mweze kutimiza madaraka mazito ambayo mtapewa. Mbao ambazo ni imara hazijikunji, hazijipindi, wala kupasuka zinaposhikilia sehemu nzito za nyumba. Matokeo ya mazoezi yenu yataonekana mnapofanya kazi pamoja na ndugu na dada zenu. Je, mkazo mtakaopata utafanya mwache kufuata kanuni za Mungu au mtazifuata kwa uthabiti kulingana na mambo mliyojifunza kupitia Neno la Mungu? Kitu kilicho imara kinaweza kubeba mizigo mizito. Uimara wa mbao hutegemea nyuzinyuzi zilizojisokota kwa nguvu. Nguvu zenu zinategemea nyuzinyuzi zilizo ndani yenu zinazoonyesha nyinyi ni watu wa aina gani. Yehova amewaleta hapa ili mtiwe nguvu, muwe wenye kutegemeka, na wenye kuaminika kwa ajili ya kazi iliyo mbele yenu. Mungu ametimiza sehemu yake, hivyo sala zetu ni kwamba mtimize sehemu yenu na mmruhusu ‘Mfundishaji wenu Mkuu’ akamilishe mazoezi yenu.”

Mambo Yaliyoonwa na Mahojiano

Kila wakati wa kuhitimu kwa darasa la Gileadi, inaburudisha kusikia kutoka kwa wanafunzi wenyewe, na ilikuwa hivyo pia wakati huu. Katika sehemu fulani ya programu, wanafunzi waliigiza baadhi ya mambo waliyojionea walipokuwa wakihubiri. Kwa mfano, wenzi fulani wa ndoa kutoka Ufaransa, walipokuwa njiani kwenda kwenye Shule ya Gileadi, walilazimika kungoja kwa saa sita katika uwanja wa ndege. Katika mkahawa wa uwanja wa ndege, walianzisha mazungumzo pamoja na wanaume wawili ambao pia walikuwa wakisubiri ndege. Mmoja wao aliposema kwamba alikuwa ametoka Malawi, walizungumza naye katika Kichichewa. Kwa mshangao aliwauliza walijuaje lugha yake. Walimweleza kwamba walikuwa wamishonari huko Malawi. Yule mwanamume mwingine aliposema alikuwa ametoka Kamerun, alishangaa walipoanza kuzungumza naye Kifaransa. Wanaume wote wawili waliwaheshimu sana Mashahidi wa Yehova, na wamishonari hao waliwahubiria.

Wenzi wa ndoa wanne walihojiwa na Nicholas Ahladis, wa Idara ya Utumishi wa Kutafsiri. Wenzi wawili wa ndoa walikuwa wamehama kutoka Australia na kwenda kwa mgawo wa umishonari katika nchi yenye vita ya Timor Mashariki. Wale wenzi wengine walihama kutoka Korea na kwenda kutumika nchini Hong Kong. Wenzi wote wanne walikuwa na hamu ya kurudi katika migawo yao ya nchi za kigeni ili watumie mambo waliyojifunza shuleni.

Baada ya wahitimu kupewa diploma zao, mmoja wa wanafunzi alisoma barua ya shukrani kwa sababu ya masomo waliyopokea. Kisha Ndugu Lösch, alimalizia programu hiyo kwa kutaja semi fulani za mfano zenye kupendeza, akisema kweli ni kama upinde maridadi wa mvua, kama chemchemi katika jangwa, na kama nanga katika bahari yenye dhoruba. Alisema, “Ni baraka iliyoje kujua ukweli. Uwe mteteaji wa kweli, na uwasaidie wengine wawe wateteaji pia.”

[Chati/​Ramani katika ukurasa wa 31]

TAKWIMU ZA DARASA

Nchi zilizowakilishwa 12

Wastani wa umri 36

Wastani wa miaka 20 tangu kubatizwa

Wastani wa miaka katika 15 huduma ya wakati wote

[Ramani]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Wahitimu walitumwa katika nchi zilizoonyeshwa hapa chini:

NCHI AMBAZO WANAFUNZI WALITUMWA

BELIZE

BENIN

KAMBODIA

KAMERUN

CAPE VERDE

CÔTE D’IVOIRE

JAMHURI YA DOMINIKA

TIMOR MASHARIKI

EKUADO

GABON

GEORGIA

GUINEA

HONG KONG

LIBERIA

MADAGASKA

MALAWI

PERU

SAMOA

SÃO TOMÉ NA PRÍNCIPE

MAREKANI

ZIMBABWE

[Picha katika ukurasa wa 31]

Darasa la 132 Lililohitimu la Shule ya Gileadi

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanza mbele kwenda nyuma, na majina yemeorodheshwa kuanzia kushoto kwenda kulia katika kila safu.

(1) Iap, R.; Iap, J.; Ng, T.; Ng, P.; Laurino, F.; Laurino, B.; Won, S.; Won, S.

(2) Morales, N.; Morales, M.; Zanutto, J.; Zanutto, M.; Rumph, I.; Rumph, J.; Germain, D.; Germain, N.

(3) Atchadé, Y.; Atchadé, Y.; Thomas, C.; Thomas, E.; Estigène, C.; Estigène, P.

(4) Ehrman, D.; Ehrman, A.; Bray, J.; Bray, A.; Amorim, M.; Amorim, D.; Seo, Y.; Seo, Y.

(5) Simon, J.; Simon, C.; Seale, C.; Seale, D.; Erickson, J.; Erickson, R.

(6) McCluskey, D.; McCluskey, T.; Brown, A.; Brown, V.; Mariano, D.; Mariano, C.; Loyola, Y.; Loyola, C.

(7) Rutgers, P.; Rutgers, N.; Foucault, P.; Foucault, C.; Wunjah, J.; Wunjah, E.