Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Matatizo Yanayowakabili Wanawake

Matatizo Yanayowakabili Wanawake

“Ninapoona jinsi wanawake wanavyotendewa, kwa kweli singependa kuwa mmoja wao.”​—ZAHRA, MWENYE UMRI WA MIAKA 15, aliyenukuliwa katika gazeti la GEO, toleo la Kifaransa.

MANENO ya msichana huyo mdogo, yaliyo upande wa kulia, yanafunua ukweli wenye kuhuzunisha ulio ulimwenguni pote, jeuri na ubaguzi kuelekea wasichana na wanawake katika maisha yao yote. Fikiria mambo yafuatayo.

  • Ubaguzi wa kijinsia. Barani Asia, wazazi wengi wanapendelea wavulana kuliko wasichana. Ripoti ya mwaka wa 2011 ya Umoja wa Mataifa inakadiria kwamba katika bara hilo, karibu wanawake milioni 134 wamekufa kwa sababu ya utoaji mimba, mauaji ya watoto, na kupuuzwa.

  • Elimu. Ulimwenguni pote, asilimia 67 ya watu ambao hawajaenda shuleni hata kidogo au wameenda shuleni kwa miaka isiyozidi minne ni wanawake.

  • Kusumbuliwa kingono. Zaidi ya wanawake bilioni 2.6 wanaishi katika nchi ambazo bado hazioni ubakaji katika ndoa kuwa hatia.

  • Afya. Katika nchi zinazoendelea, karibu kila dakika mbili, mwanamke hufa kutokana na matatizo ya mimba au kujifungua yanayosababishwa na kukosa huduma za msingi za kitiba.

  • Haki za kumiliki mali. Ingawa wanawake hukuza zaidi ya nusu ya vyakula ulimwenguni, katika nchi nyingi hawana haki za kisheria za kumiliki mali au kurithi mashamba.

Kwa nini wanawake wamenyimwa haki kama hizo za kimsingi? Jamii fulani hufuata itikadi za kidini na mazoea ambayo huendeleza au hata kutetea jeuri dhidi ya wanawake. Gazeti fulani la Kifaransa lilimnukuu mwanasheria wa India Chandra Rami Chopra ambaye alisema: “Sheria zote za kidini zinapatana katika jambo hili: Zinaunga mkono ubaguzi dhidi ya wanawake.”

Je, una maoni kama hayo? Je, unafikiri Biblia inafundisha kwamba wanawake ni duni, kama vitabu vingine vingi vya kidini vinavyofundisha? Watu fulani wanafikiri kwamba baadhi ya maandiko katika Biblia yanaunga mkono jambo hilo. Lakini kwa kweli Mungu aliyetunga Biblia anawaonaje wanawake? Ingawa hili linaweza kuwa jambo lenye kuchochea sana hisia, kuchunguza kwa makini na kwa unyoofu mambo ambayo Biblia inasema kutatusaidia kupata jibu.