Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sasa Ninamjua Mungu Mungu Ninayemwabudu

Sasa Ninamjua Mungu Mungu Ninayemwabudu

Kasisi wa Kanisa la Pentekoste ambaye ilisemekana kwamba alikuwa na nguvu za kuponya alikuja kututembelea. Aliponigusa, nilianguka chini na kupoteza fahamu, “nikaingiwa na roho.” Nilipopata fahamu, nilihisi kwamba nilikuwa na kitu nilichotaka, nguvu za kuponya. Ni nini kilichonifanya nijipate katika hali hiyo, na tukio hilo liliathirije maisha yangu? Kabla sijawasimulia jambo hilo, acheni niwaeleze kuhusu maisha yangu.

NILIZALIWA huko Ilocos Norte, Ufilipino, Desemba 10, 1968, nikiwa mtoto wa saba katika familia ya watoto kumi. Kama ilivyo kawaida kwa Wafilipino wengi, familia yetu ilikuwa ya Wakatoliki. Nilihitimu masomo ya shule ya sekondari mwaka wa 1986, na nilitaka kuwa muuguzi. Hata hivyo, kwa sababu nilishikwa na ugonjwa mbaya, sikufaulu kuwa muuguzi. Hata nilifikiri kwamba ningekufa. Nikiwa nimekata tamaa, nilimwomba Mungu anisaidie na nikamwahidi kwamba ikiwa ningepona, ningemtumikia kwa muda wote wa maisha yangu.

Baada ya kuugua kwa muda mrefu mwishowe nilipona na nikakumbuka jambo nililomwahidi Mungu. Hivyo, Juni 1991, nikajiunga na shule ya Biblia ya Kanisa la Pentekoste. Ilisemekana kwamba ratiba ya shule ingetia ndani kupokea “zawadi ya bure ya roho takatifu.” Nilitamani kupata nguvu za kuponya. Shule hiyo ilitufundisha kwamba uwezo huo ungepatikana kupitia kufunga na kusali. Ili nionyeshe kwamba nilikuwa na “zawadi,” pindi moja nilisikiliza kisirisiri mwanafunzi mwenzangu alipokuwa akisali kwa sauti kwenye sehemu fulani ya chumba wakati wa sala. Alipokaribia kumaliza sala yake, nilirudi haraka mahali nilipokuwa nimepiga magoti. Baadaye, nikamwambia kila kitu alichokuwa akiomba katika sala, na akaamini kwamba nilikuwa na “zawadi ya bure”!

Nilipokuwa nikiendelea na masomo yangu katika shule hiyo, nilikuwa na maswali mengi. Kwa mfano andiko la Mathayo 6:9 linamtaja “Baba” na “jina” lake. Niliuliza maswali kama vile “Baba anayetajwa na Yesu ni nani?” na “Ni jina la nani ambalo linapaswa kutakaswa?” Mara nyingi majibu ya walimu wangu hayakueleweka na hayakuniridhisha. Walizungumza kuhusu fundisho la Utatu na wakasema kwamba lilikuwa fumbo. Fundisho hilo lilinitatanisha sana. Licha ya hayo yote, niliendelea na mazoezi yangu ya kuwa kasisi.

Jinsi Nilivyowajua Mashahidi wa Yehova

Katika shule ya Biblia, tulifundishwa kwamba Mashahidi wa Yehova walieneza uwongo mbaya zaidi wa kidini. Pia, waliitwa wapinga-Kristo. Nikasitawisha chuki kuelekea dini hiyo.

Katika mwaka wangu wa pili shuleni, nilienda nyumbani kuwatembelea wazazi wangu wakati wa likizo. Mmoja wa dada zangu wakubwa, anayeitwa Carmen, alisikia kwamba nilikuwa nyumbani naye pia akaja kutembea. Tayari alikuwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova aliyebatizwa. Alipojaribu kunifundisha kumhusu Mungu, nilimjibu hivi kwa ukali: “Tayari ninamjua Mungu ninayemtumikia!” Baada ya kumtukana kwa sauti, nilimsukuma na sikumpa nafasi nyingine ya kuzungumza nami.

Baada ya kurudi kwenye shule ya Biblia, Carmen alinitumia nakala ya broshua Je! Uamini Utatu? * Mara moja nikaikunja-kunja na kuichoma kwa moto. Bado nilikuwa nimemkasirikia.

Kufanya Maendeleo Nikiwa Kasisi

Nilipokuwa nikiendelea na masomo yangu katika shule ya Biblia, nilifaulu kuwageuza watu fulani wakawa waamini. Nilifurahi hasa mama na ndugu yangu walipojiunga nami katika Kanisa la Pentekoste.

Mnamo Machi 1994, nilihitimu kutoka kwenye shule hiyo ya Biblia ya Kanisa la Pentekoste. Kama nilivyotaja mwanzoni, pindi hiyo kasisi fulani alikuwa ametutembelea. Sote tuliokuwa tukihitimu tulitaka kuwa pamoja naye kwa sababu tuliamini kwamba alikuwa na zawadi ya uponyaji. Tulijiunga naye jukwaani, huku tukiruka-ruka na kupiga makofi pamoja naye na kucheza muziki uliokuwa ukipigwa na bendi. Kisha, yule kasisi alipomgusa mtu yeyote, alianguka chini na, “kuingiwa na roho.” * Aliponigusa, mimi pia nikaanguka na kupoteza fahamu. Niliporudiwa na fahamu, niliogopa, lakini nilihisi kwamba sasa nilikuwa na nguvu za kuponya, na nikafurahi.

Muda mfupi baadaye, nilitumia nguvu hizo kumponya mtoto fulani ambaye alikuwa na homa kali sana. Niliposali, mara moja yule mtoto alianza kutokwa na jasho na ile homa ikakwisha. Mwishowe, nilihisi kwamba ningetimiza ahadi niliyompa Mungu. Jambo la kushangaza ni kwamba nilihisi nimekosa kitu fulani. Moyoni mwangu niliamini kuna Mungu mmoja tu wa kweli, lakini sikujua alikuwa nani hasa. Na nilikuwa na shaka kuhusu mafundisho mengi ya kanisa letu.

Nilitumia nguvu hizo kumponya mtoto fulani ambaye alikuwa na homa kali sana

Mambo Yaliyobadili Maoni Yangu

Baada ya matukio hayo, nikaanza kuwachukia Mashahidi wa Yehova hata zaidi. Kila nilipopata machapisho ya Mashahidi wa Yehova, niliyateketeza. Kisha jambo lisilotazamiwa likatokea. Nilishtuka kutambua kwamba mama yangu hakutaka tena kushirikiana na dini yetu. Carmen alikuwa akijifunza Biblia pamoja naye! Nilimkasirikia sana dada yangu.

Kisha nikapata gazeti la Amkeni! katika nyumba ya mama yangu. Kama kawaida ningeliteketeza. Lakini nilitaka kujua mambo aliyokuwa akisoma, hivyo nikapitia kurasa za gazeti hilo. Kisha nikaona makala iliyozungumzia mtu ambaye aliamini kabisa mambo ambayo kanisa lake lilifundisha. Hata hivyo, alipoanza kusoma machapisho ya Mashahidi pamoja na Biblia, akasadikishwa kwamba mafundisho ya Utatu, moto wa mateso, na kutokufa kwa nafsi hayapatani na Maandiko. Niliguswa moyo sana. Haya ndiyo mambo niliyotaka kuelewa. Tangu wakati huo, nilitamani kuelewa kweli za Biblia.

Baada ya kusoma simulizi lingine la maisha katika gazeti la Amkeni! kuhusu mtu aliyekuwa akinywa pombe kupita kiasi na kutumia dawa za kulevya ambaye alifanya mabadiliko makubwa na kuboresha maisha yake kwa sababu ya kujifunza Biblia, nikaanza kusoma machapisho mengi zaidi ya Mashahidi. Nilipata broshua inayoitwa Jina la Mungu Litakaloendelea Milele. * Baada ya kuisoma, nilijifunza kwamba jina la Mungu ni Yehova. Nilifurahia kujifunza ukweli kumhusu Mungu wa pekee wa kweli.​—Kumbukumbu la Torati 4:39; Yeremia 10:10.

Nilifurahi sana kujifunza ukweli kumhusu Mungu wa pekee wa kweli!

Niliendelea kusoma kisiri na nikajifunza kweli nyingine nyingi za Biblia. Kwa mfano, katika shule ya Kanisa la Pentekoste nilikuwa nimefundishwa kwamba Yesu ni Mungu, lakini nilijifunza kupitia Biblia kwamba yeye ni “Mwana wa Mungu aliye hai.”—Mathayo 16:15, 16.

Kubadili Maoni Yangu

Nilipokutana tena na Carmen, alishangaa nilipomwomba nakala ya kibinafsi ya broshua Jina la Mungu Litakaloendelea Milele na machapisho mengine. Nilikuwa nimetumia miaka mingi katika ile shule ya Biblia, lakini sikufundishwa ukweli, nilikuwa nimepofushwa. Sasa nilijawa na shangwe moyoni kwa sababu ya kweli nilizokuwa nikijifunza katika Biblia. Nilielewa kabisa maana ya maneno haya ya Yesu: “Mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yohana 8:32) Kweli hizo zilikuwa zimeanza kubadili maisha yangu.

Kweli hizo zilikuwa zimeanza kubadili maisha yangu

Kwa muda fulani, nilifikiri kwamba ningeweza kumwabudu Yehova kisiri na wakati huohuo niendelee kuwa kasisi. Baada ya muda nikatambua kwamba singeendelea tena kufundisha mafundisho mengi ya kanisa. Hata hivyo, niliogopa. Ningepataje riziki ikiwa ningeacha kuwa kasisi? Ni jambo la kuaibisha kama nini kwa kanisa ikiwa kasisi wao angegeuka na kuwa Shahidi wa Yehova! Hivyo, nikaendelea kufundisha nikiwa kasisi, lakini nikaepuka kuzungumzia mafundisho ya uwongo ya kanisa hilo.

Nilipokutana tena na dada yangu Carmen, alipendekeza kwamba nihudhurie mkutano wa Mashahidi wa Yehova. Kwa vile nilikuwa nikienda kwa ukawaida kwenye kanisa letu kuu katika Jiji la Laoag, nilitafuta kisiri mahali ambapo Mashahidi wa Yehova walifanyia mikutano, katika Jumba la Ufalme la jiji hilo. Nilikutana na Alma Preciosa Villarin, aliyeitwa kwa jina la utani “Precious,” mhudumu wa wakati wote katika kutaniko hilo. Ingawa bado nilikuwa na maoni yasiyofaa kuelekea Mashahidi, nilikubali alipoomba kunifundisha Biblia.

Dada yangu alinitendea kwa subira sana alipokuwa akinifundisha kweli za Biblia. Precious pia alionyesha roho hiyohiyo ya subira. Alinisaidia kwelikweli kuielewa Biblia, ingawa ningekasirika na kujaribu kubishana naye, na hata nyakati nyingine kuzungumza kwa sauti ya juu, huku nikisisitiza mambo fulani niliyokuwa nimefundishwa. Niliguswa moyo sana na jinsi Precious na Mashahidi wengine walivyopendezwa nami kibinafsi, jinsi walivyokuwa wanyenyekevu, na walivyonitendea kwa wororo. Hilo lilinichochea nitake kumwabudu Yehova.

Mwezi wa Julai 1995, nilitambua kwamba nilipaswa kuacha cheo changu cha kuwa kasisi. Kwa nini? Andiko la Ufunuo 18:4 linazungumzia dini ya uwongo kwa njia ya mfano linaposema hivi: “Tokeni kwake, watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake, na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya mapigo yake.” Ningepataje riziki? Andiko la Waebrania 13:5 lilinifundisha kwamba tukifanya mapenzi ya Mungu, anatuahidi hivi: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.”

Ingawa sasa baba yangu na ndugu yangu walikuwa wakinipinga vikali, majuma mawili kabla ya kubatizwa na kuwa Shahidi, niliamua kwenda nyumbani na nikateketeza vitu vyote ambavyo nilikuwa nikitumia nilipokuwa kasisi. Baada ya kufanya hivyo, nikatambua kwamba sikuwa tena na nguvu za kipekee nilizokuwa nazo. Kabla ya hapo, kila nilipolala, nilihisi kitu fulani kikinisukuma chini bila kuacha. Sasa sikuhisi hivyo tena. Sikuona tena vivuli ambavyo nilikuwa nikiviona kwenye dirisha la chumba changu. Kupitia kujifunza Biblia, nilikuwa nimejifunza kwamba leo zile zinazoitwa eti zawadi, kama vile nguvu za kuponya, hazitoki kwa Mungu bali kwa roho waovu. Ninafurahi sana kwamba niliacha kushirikiana nao, kama vile tu yule kijakazi ambaye Paulo alimweka huru kutoka kwa “roho mwovu wa uaguzi.”​—Matendo 16:16-18.

Katika mwezi wa Septemba 1996, ilikuwa shangwe iliyoje kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova siku ileile pamoja na mama yangu! Baada ya kubatizwa nilijaza maombi ya kuwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, na nilifurahia kutumika kwa miaka mingi katika huduma ya wakati wote.

Sasa ninaishi na mume wangu anayeitwa Silver. Tukiwa pamoja, tunajitahidi kumzoeza binti yetu ili aishi kulingana na kweli za Biblia. Baadhi ya dada zangu wamejiunga nasi pia katika kumtumikia Yehova. Ingawa ninasikitika kwamba kwa miaka mingi sikumjua Mungu, nina furaha nyingi kwa sababu sasa ninamjua Mungu ninayemwabudu.

^ fu. 10 Iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa haichapishwi tena.

^ fu. 13 “Kuingiwa na roho” kunamaanisha tukio lisilo la kawaida katika dini fulani ambapo inasemekana “roho” huja juu ya waamini kwa nguvu sana hivi kwamba wanaanguka chini.

^ fu. 18 Iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.