Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mazungumzo Pamoja na Jirani

Je, Mungu Anawaadhibu Watu Katika Moto wa Mateso?

Je, Mungu Anawaadhibu Watu Katika Moto wa Mateso?

MASHAHIDI WA YEHOVA wanafurahia kuzungumza kuhusu Biblia pamoja na jirani zao. Je, kuna jambo lolote kuhusu Biblia ambalo limekuwa likikutatiza? Je, kuna jambo lolote ambalo Mashahidi wa Yehova wanaamini au kufanya ambalo ungependa kulifahamu zaidi? Ikiwa ndivyo, basi unapokutana tena na Shahidi wa Yehova usisite kumwuliza. Atafurahi kuzungumzia jambo hilo pamoja nawe.

Mazungumzo yafuatayo yanaonyesha jinsi Shahidi wa Yehova anavyoweza kuzungumza na jirani yake. Hebu tuwazie Shahidi anayeitwa John amemtembelea mwanamume anayeitwa David nyumbani kwake.

Je, Mungu Anawaadhibu Watu Waovu?

John: Nimefurahi kukuona tena, David.

David: Hata mimi nimefurahi kukuona tena.

John: Nimekuwa nikifikiria kuhusu jambo fulani ulilotaja wakati uliopita.

David: Jambo gani hilo?

John: Ulisema kwamba ulishangaa wakati uliposikia kuwa Mashahidi wa Yehova hawaamini kwamba kuna moto wa mateso.

David: Ndiyo, jambo hilo lilinishangaza. Na kusema kweli, ni vigumu kwangu kukubaliana na wewe kwamba hakuna moto wa mateso.

John: Asante kwa kuniambia hivyo. Mimi hupenda kusikiliza maoni ya wengine. Kwa kuwa watu wana maoni yanayotofautiana kuhusu moto wa mateso, ningependa kujua maoni yako kuhusu jambo hilo?

David: Siku zote nimeamini kwamba watu wabaya wanapokufa huenda motoni na kwamba wanateswa milele.

John: Watu wengi wana maoni kama hayo. Acha nikuulize swali David, umewahi kupatwa na mambo mabaya katika maisha yako?

David: Ndiyo. Dada yangu aliuawa miaka mitano iliyopita.

John: Ninasikitika sana kusikia hivyo. Ni lazima unamkosa sana dada yako.

David: Ndiyo, ninamfikiria kila siku.

John: Nimegundua kwamba watu fulani wanashikilia sana fundisho la moto wa mateso kwa sababu wamewahi kuathiriwa na vitendo vibaya vya watu waovu. Isitoshe, watu wasio na hatia wanataka kuwaona watu wabaya wakiadhibiwa kwa sababu ya vitendo vyao.

David: Kweli kabisa! Ninataka mwanamume aliyemuua dada yangu aadhibiwe kwa sababu ya kitendo alichokifanyia familia yetu.

John: Ni kawaida kuhisi hivyo. Biblia inafundisha kwamba hata Mungu hukasirika watu wasiokuwa na hatia wanapotendewa vibaya na anatuahidi kwamba atawaadhibu watu waovu. Ona andiko la Isaya 3:11 linavyosema: “Ole wake mtu mwovu!—Msiba; kwa maana matendo yaliyotendwa kwa mikono yake mwenyewe atalipwa yeye!” Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atawaadhibu watu waovu.

David: Lakini hilo linawezekanaje ikiwa hakuna moto wa mateso, kama unavyosema?

John: Hilo ni swali zuri. Kwa ufupi, jibu ni kwamba Mungu huwaadhibu watu waovu kwa kuwaangamiza kabisa. Fikiria yale ambayo Biblia inasema kwenye andiko la 2 Wathesalonike 1:9. Tafadhali, soma andiko hilo.

David: Acha nisome. Linasema hivi: “Watu hao watahukumiwa adhabu ya uharibifu wa milele kutoka mbele ya Bwana.”

John: Unaona David, hakuna tumaini kwa watu waovu, kwa sababu Mungu huwahukumu kifo milele. Hawana tumaini la uhai wa wakati ujao.

David: Nimeona jinsi mistari hiyo inavyosema, lakini jambo hilo halionekani kuwa haki. Kila mtu hufa. Je, watu waovu hawastahili kuadhibiwa vikali?

Haki ya Mungu Inataka Nini?

John: Nimetambua kwamba wewe unajali haki.

David: Ndiyo, ninajali sana.

John: Unastahili pongezi. Ukweli ni kwamba, wanadamu wana uwezo wa kujua mambo mema na mabaya kwa sababu Mungu ametuumba tukiwa na uwezo huo. Yeye pia anapendezwa sana na haki. Lakini viongozi wa dini wanapofundisha kwamba Mungu anawaadhibu watu katika moto wa mateso, kwa kweli wanaonyesha kwamba Mungu hana haki hata kidogo.

David: Unamaanisha nini?

John: Acha nikupe mfano. Je, unajua simulizi la Biblia kuhusu Adamu na Hawa?

David: Ndiyo. Mungu aliwaambia wasile tunda la mti fulani, lakini hawakutii.

John: Kweli kabisa. Acha tusome pamoja simulizi hilo. Linapatikana katika andiko la Mwanzo 2:16, 17. Mistari hiyo inasema: “Yehova Mungu akamwekea mtu amri hii: ‘Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.’” Kwa hiyo, Mungu alisema nini kingetokea ikiwa Adamu angekula tunda alilokatazwa?

David: Alisema kwamba Adamu angekufa.

John: Ni kweli. Hebu fikiria: Kwa sababu ya dhambi ya Adamu, wanadamu wote wanazaliwa wakiwa watenda dhambi. * Na bado hata katika kisa hiki, je, Mungu anasema jambo lolote kuhusu kuwaadhibu Adamu na Hawa katika moto wa mateso?

David: Hapana.

John: Lakini kama Adamu na Hawa wangekuwa katika hatari ya kuteswa milele, je, si ni kweli kwamba Mungu alipaswa kuwaonya? Je, hilo halingekuwa jambo lenye haki na upendo?

David: Nafikiria hivyo.

John: Fikiria pia, kile ambacho Mungu aliwaambia Adamu na Hawa baada ya kutenda dhambi. Tafadhali soma andiko la Mwanzo 3:19.

David: Linasema hivi: “Kwa jasho la uso wako utakula mkate mpaka utakaporudi katika udongo kwa kuwa ulitolewa katika huo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.”

John: Asante. Kulingana na neno la Mungu, Adamu angeenda wapi baada ya kufa?

David: Mungu alisema kwamba Adamu angerudi mavumbini.

John: Kweli kabisa. Je, unakubaliana nami kwamba ili mtu arudi mahali fulani ni lazima aliwahi kuwa hapo wakati uliopita?

David: Bila shaka.

John: Na Adamu alikuwa wapi kabla ya kuumbwa na Mungu?

David: Hakuwepo.

John: Ni kweli. Utaona kwamba katika hukumu ya Mungu hakuna mahali popote ambapo moto wa mateso umetajwa. Je, lingekuwa jambo la haki Mungu amwambie Adamu kwamba angerudi mavumbini ikiwa Adamu alikuwa anaenda kuteketezwa motoni?

David: Hapana, isingekuwa haki.

Je, Ibilisi Hutumiwa Kufanya Mapenzi ya Mungu?

John: Kuna jambo lingine kuhusu fundisho la moto wa mateso ambalo ningependa tulifikirie.

David: Ni jambo gani hilo?

John: Mara nyingi watu husema ni nani “atakayewachoma” watu katika moto wa mateso? Wanadhani ni nani hasa anayewaadhibu watu walio motoni?

David: Ni Ibilisi.

John: Hata hivyo, Ibilisi ni adui mkubwa wa Mungu. Ikiwa Mungu huwapeleka watu motoni wateswe na Ibilisi, je, jambo hilo halingeonyesha kwamba kuna ushirikiano fulani kati ya Mungu na Ibilisi?

David: Aha! Sijawahi kufikiria jambo hili katika njia hiyo.

John: Ili kuelewa jambo hilo fikira mfano huu. Wewe ni baba, sivyo?

David: Ndiyo, nina mvulana. Hivi karibuni alifikisha miaka 15.

John: Wazia kwamba mvulana wako amekuwa mwasi sana. Anafanya mambo mengi mabaya ambayo yanayokuhuzunisha. Ungefanya nini?

David: Ningejaribu kumrekebisha.

John: Nina hakika kwamba ungejaribu tena na tena kumsaidia ili abadilike.

David: Bila shaka.

John: Tuseme licha ya jitihada zako zote, mwana wako anakataa kile unachomwambia. Mwishowe, huenda ukahisi huna njia nyingine ya kumsaidia isipokuwa kumwadhibu kwa njia fulani.

David: Ndiyo.

John: Lakini namna gani ikiwa ungetambua kwamba mwanamume fulani mwovu amekuwa akimchochea mwana wako, kwa kumfundisha kufanya mambo hayo yote mabaya?

David: Ningemkasirikia sana mwanamume huyo.

John: Sasa, ningependa kupata maoni yako. Ukijua kwamba mwanamume fulani mwovu mwenye maadili mabaya amekuwa akimchochea mwana wako afanye mambo mabaya, je, ungeenda kwa mwanamume huyo na kumwomba amwadhibu mwana wako kwa niaba yako?

David: Siwezi kamwe. Jambo hilo lisingepatana na akili.

John: Kwa kweli, unafikiri ni jambo linalopatana na akili kwa Mungu kumwomba Shetani Ibilisi​—anayechochea wanadamu wawe waovu—awaadhibu watu hao waovu?

David: Hapana, ninadhani haiwezekani.

John: Ikiwa Mungu angetaka watu waovu waadhibiwe, kwa nini Ibilisi—adui mkubwa wa Mungu—atumiwe kutimiza mapenzi ya Mungu na kuwatesa wanadamu?

David: Sijawahi kufikiria katika njia hiyo!

Yehova Atakomesha Uovu Wote

John: Hata hivyo, uwe na hakika kwamba Mungu atachukua hatua dhidi ya waovu wasiotaka kubadilika. Labda tunaweza kusoma pamoja andiko hili la mwisho ambalo linafafanua waziwazi wazo hilo. Andiko la Zaburi 37:9. Tafadhali, unaweza kusoma andiko hilo?

David: Ndiyo. Linasema hivi: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia.”

John: Asante. Umeona Yehova Mungu atawafanyia nini waovu?

David: Andiko hilo linasema Mungu atawakatilia mbali waovu.

John: Jambo hilo ni kweli. Kwa maneno mengine atawaharibu milele. Lakini watu wazuri—“wale wanaomtumaini Yehova”—watafurahia maisha hapa duniani milele. Bila shaka, jambo hilo linaweza kutokeza maswali mengi akilini mwako. Kwa mfano, kwa nini Mungu hajawazuia wanadamu wasitende mambo maovu? Na ikiwa amekusudia kuwaadhibu watu waovu, kwa nini bado hajafanya hivyo?

David: Hayo ni maswali mazuri.

John: Labda nitakuonyesha majibu ya Biblia wakati ujao. *

David: Ningependa kujua majibu ya maswali hayo.

^ fu. 79 Kwa habari zaidi, ona sura 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.