Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ufisadi Unazidi Kuongezeka?

Kwa Nini Ufisadi Unazidi Kuongezeka?

“Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”—MHUBIRI 8:9.

MANENO ya andiko hilo yanaonyesha kikamili historia ya utawala wa wanadamu. Utawala huo umesababisha kuteseka na huzuni nyingi. Kwa muda mrefu, jitihada za watu wenye nia nzuri ambao wamejaribu kutokeza jamii iliyo na haki, sikuzote zimezuiwa na tamaa na ufisadi. Kwa nini hali iko hivyo? Kwa nini ufisadi unazidi kuongezeka? Kwa ujumla, ni kwa sababu ya mambo matatu yafuatayo ambayo husababisha uvutano usiofaa.

1. Uvutano wa dhambi.

Biblia inataja waziwazi kwamba ‘sote tuko chini ya dhambi.’ (Waroma 3:9) Kama tu ugonjwa wa kurithiwa usioweza kutibiwa, dhambi ‘inakaa’ ndani yetu. Kwa maelfu ya miaka, dhambi ‘imewatawala’ wanadamu kama mfalme. “Sheria” yake imeendelea kufanya kazi ndani yetu. Mwelekeo wa kutenda dhambi umewafanya watu wengi watangulize mapendezi yao au kutafuta mali na mamlaka huku wakiwaumiza watu wengine.—Waroma 5:21; 7:17, 20, 23, 25.

2. Uvutano wa ulimwengu mwovu tunamoishi.

Ulimwengu wetu umejaa pupa na ubinafsi. Watu wengi wanaona kuwa ni vigumu kujiendesha kwa njia tofauti na watu wanaowazunguka. Wakisukumwa na ubinafsi wanakuwa wenye njaa ya kutaka mamlaka. Pia, wanakuza tamaa ya kupata pesa na mali kwa wingi hata kuliko wanavyohitaji. Jambo la kusikitisha ni kwamba wako tayari kujihusisha na ukosefu wa haki ili watimize malengo yao. Badala ya kukataa uvutano usiofaa, watu kama hao “[wanafuata] umati kwa ajili ya makusudio maovu.”​—Kutoka 23:2.

3. Uvutano wa Shetani Ibilisi.

Shetani, kiumbe mwasi wa kiroho, ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufunuo 12:9) Anafurahia kuwapotosha wanadamu. Kwa ujanja anaweza kumshawishi mtu atumie vibaya tamaa ya asili ya kutaka kuwa na vitu vya kimwili na pesa na hata kumfanya atende kwa udanganyifu.

Je, hilo linamaanisha sisi ni kama vikaragosi ambavyo vinaongozwa na Shetani, yaani, tunapaswa kutii kila jambo analotuamuru? Tutapata jibu katika makala inayofuata.