Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Swali la 1: Je, Maisha Yangu Yana Kusudi?

Swali la 1: Je, Maisha Yangu Yana Kusudi?

ROSALIND, aliyelelewa huko Uingereza, alikuwa na tamaa kubwa ya kupata ujuzi. Pia, alitaka kuwasaidia watu. Baada ya kumaliza shule alipata kazi yenye mshahara mnono ambayo ilihusisha kuwasaidia watu wasio na makao na pia aliwasaidia watu wasiojiweza na wenye matatizo ya kujifunza. Ingawa alikuwa na kazi yenye kuridhisha na alikuwa na vitu vya kimwili, anasema: “Kwa miaka mingi nilijiuliza, ‘Kwa nini tuko hai?’ na ‘Kusudi la maisha ni nini?’”

Kwa nini tuulize swali hilo?

Wanadamu si kama wanyama wasioweza kufikiri. Tuna uwezo wa kujifunza kutokana na mambo yaliyopita, kupanga wakati ujao, na kutafuta kusudi la maisha yetu.

Watu fulani wanafikiri jibu ni nini?

Wengi wanafikiri kwamba kusudi kuu la maisha ni kupata utajiri au umaarufu na hivyo kuwa na furaha.

Jibu hilo linamaanisha nini?

Tunajiamulia mambo ya kutanguliza maishani. Mapenzi ya Mungu si ya maana kuliko tamaa zetu.

Biblia inafundisha nini?

Mfalme Sulemani alijikusanyia utajiri mwingi na kufuatia anasa lakini akatambua kwamba vitu hivyo havikumletea kusudi la kweli maishani. Alitaja jambo linaloleta kusudi la kweli maishani alipoandika: “Huu ndio mwisho wa mambo, kila jambo limekwisha sikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.” (Mhubiri 12:13) Kushika amri za Mungu kunatia ndani nini?

Mungu anakusudia kwamba tuwe na furaha maishani. Sulemani aliandika: “Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kwamba ale, naam, anywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu. Hilo pia mimi nimeliona, naam mimi, ya kwamba linatoka kwenye mkono wa Mungu wa kweli.”—Mhubiri 2:24.

Mungu pia anataka tupende na kutunza familia zetu. Ona mwongozo rahisi na ulio wazi ambao kila mshiriki wa familia anapewa.

  • “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.”—Waefeso 5: 28.

  • “Mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”—Waefeso 5:33.

  • “Enyi watoto, watiini wazazi wenu.”—Waefeso 6:1.

Tukifuata kanuni hizo za Biblia, tutaridhika na kuwa na na furaha ya kadiri. Hata hivyo, jambo muhimu zaidi ambalo tunaweza kufanya ni kujifunza mengi iwezekanavyo kumhusu Muumba na kumkaribia kama Rafiki yetu. Hata Biblia inatualika ‘tumkaribie Mungu.’ Kisha inatoa ahadi hii nzuri ajabu: “Naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Ukikubali mwaliko huo, maisha yako yatakuwa na kusudi halisi.

Rosalind aliyetajwa mapema, sasa anahisi kwamba ametambua kusudi la maisha. Kwenye ukurasa wa 10 wa gazeti hili, unaweza kusoma mambo yaliyomfanya abadili mtazamo wake.