Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Thomas Emlyn​—Je, Alikuwa Mkufuru au Mtetezi wa Ukweli?

Thomas Emlyn​—Je, Alikuwa Mkufuru au Mtetezi wa Ukweli?

THOMAS EMLYN alikuwa nani na nini kilichomchochea kuutetea ukweli? Tunaweza kujifunza nini kutoka kwake ambacho kinaweza kutusaidia leo?

Ili kujibu maswali hayo, tutachunguza kilichotokea mwishoni mwa karne ya 17 na mwanzoni mwa karne ya 18 huko Uingereza na Ireland. Kanisa la Anglikana lilikuwa na mamlaka kubwa sana wakati huo. Vikundi vya Waprotestanti na watu fulani walipingana na kanisa hilo.

ALIKUWA NANI?

Thomas Emlyn alizaliwa kipindi hicho mnamo Mei 27, 1663, huko Stamford, Lincolnshire, Uingereza. Alihubiri kanisani kwa mara ya kwanza alipokuwa na umri wa miaka 19. Baadaye akawa mhudumu wa mwanamke fulani mwenye cheo huko London; kisha akahamia Belfast, Ireland.

Huko Belfast akawa msimamizi wa kanisa. Muda ulivyozidi kupita, Emlyn alitumika kama mhudumu katika maeneo mbalimbali, kutia ndani Dublin.

KWA NINI ALISHTAKIWA KUWA MKUFURU?

Wakati huo, Emlyn alikuwa akisoma Biblia kwa makini. Utafiti wake ulimfanya aanze kutilia shaka fundisho la Utatu hata ingawa mwanzoni aliliamini. Alipochunguza vitabu vya Injili, alisadikishwa kwamba viliunga mkono mambo mapya aliyojifunza.

Emlyn hakusema mara moja mambo aliyokuwa amejifunza. Hata hivyo, waumini wenzake katika kanisa la Dublin walitambua kwamba hakutaja Utatu katika mahubiri yake. Akitambua kwamba uchunguzi wake haungekubaliwa, alisema: “Ikiwa nitasema maoni yangu, sitaendelea kushikilia cheo changu cha sasa.” Mnamo Juni 1702, waumini wenzake wawili walimuuliza sababu iliyofanya asitaje Utatu katika mahubiri yake. Emlyn alikiri kwamba hakuamini tena fundisho hilo na akaamua kujiuzulu.

Kitabu cha Emlyn kilichokuwa na uthibitisho wa Maandiko kwamba Yesu si Mungu Mweza-Yote

Baada ya siku chache, aliondoka Dublin, huko Ireland, na kuelekea Uingereza. Hata hivyo, baada ya majuma kumi alirudi Dublin ili kushughulikia mambo fulani, ingawa alikusudia kuhamia London kabisa. Akiwa Dublin, alitaka kufafanua maoni yake, hivyo akaandika kitabu kilichoitwa An Humble Inquiry Into the Scripture-Account of Jesus Christ. Katika kitabu hicho, alithibitisha waziwazi kwa Maandiko kwamba Yesu hawezi kuwa Mungu Mweza-Yote. Hilo liliwakasirisha wafuasi wa kanisa la zamani la Emlyn huko Dublin. Hivyo, wakamfungulia mashtaka.

Emlyn alikamatwa na kupelekwa kwenye Mahakama ya Malkia huko Dublin mnamo Juni 14, 1703. Katika kitabu chake kinachoitwa True Narrative of the Proceedings, Emlyn anasema kwamba alishtakiwa “kwa sababu ya kuandika na kuchapisha kitabu, na kwamba alikuwa amekufuru na kadhalika. Kwamba Yesu Kristo hakuwa  sawa na Mungu Baba.” Kesi yake haikufanywa kwa haki. Maaskofu saba wa Kanisa la Ireland waliketi mbele pamoja na baraza la kuhukumu. Emlyn hakuruhusiwa kujitetea. Richard Levins, mwanasheria maarufu, alimwambia Emlyn kwamba angewindwa “kama mbwa-mwitu.” Mwishoni mwa kesi hiyo, Richard Pyne, Hakimu Mkuu wa Ireland aliliambia baraza la kuhukumu kwamba kama hawangetoa hukumu iliyotazamiwa wangekiona cha mtema kuni, labda akimaanisha kwamba wangeadhibiwa.

Niko tayari kuteseka kwa sababu ya yale ninayoamini kuwa ukweli na utukufu wake [Mungu].”​—Thomas Emlyn

Baada ya Emlyn kupatikana na hatia, kiongozi wa mashtaka alipendekeza kwamba akanushe mambo aliyosema. Emlyn alikataa. Alitozwa faini na akahukumiwa kufungwa mwaka mmoja. Kwa vile alishindwa kulipa faini, alikaa jela miaka miwili hadi rafiki yake mmoja alipowashawishi wenye mamlaka wapunguze faini hiyo. Emlyn aliachiliwa mnamo Julai 21, 1705. Mateso aliyopitia yalimsukuma kusema maneno yaliyonukuliwa mwanzoni: “Niko tayari kuteseka kwa sababu ya yale ninayoamini kuwa ukweli na utukufu wake [Mungu].”

Emlyn alihamia London, ambako mwishowe alishirikiana na William Whiston, msomi mwingine wa Biblia aliyekuwa ametengwa na jamii kwa sababu ya kuchapisha mambo aliyoamini ni ukweli wa Biblia. Whiston alimheshimu Emlyn, na kumwita “‘mtetezi wa kwanza’ wa ‘ukristo wa zamani.’”

KWA NINI ALIPINGA UTATU?

Kama William Whiston na msomi mwingine maarufu, Isaac Newton, Emlyn aligundua kwamba Biblia haiungi mkono fundisho la Utatu kama lilivyoandikwa kwenye Imani ya Athanasia. Alisema hivi: “Baada ya kutafakari sana na kuyachunguza Maandiko matakatifu, . . . Nilipata sababu kubwa . . . ya kubadili maoni yangu kuhusu jinsi nilivyoliona fundisho la Utatu.” Alifikia mkataa huu: “Mungu, Baba ya Yesu Kristo ndiye Mweza-Yote.”

Ni nini kilichofanya Emlyn afikie mkataa huo? Alisoma maandiko mengi yaliyoonyesha tofauti kati ya Yesu na Baba Yake. Yafuatayo ni baadhi ya maandiko hayo (maelezo ya Emlyn yameandikwa kwa mlazo):

  •  Yohana 17:3: “Kristo hatajwi kuwa Mungu mmoja au Mungu, na hivyo kuwa Mungu wa pekee.” Baba tu ndiye anayeitwa “Mungu wa pekee wa kweli.”

  •  Yohana 5:30: “Mwana hafanyi mapenzi yake mwenyewe, bali anafanya mapenzi ya Baba.”

  •  Yohana 5:26: “Baba ndiye anayempa Uzima.”

  •  Waefeso 1:3: “Yesu Kristo anatajwa mara nyingi kuwa Mwana wa Mungu, lakini hakuna andiko linalosema Baba ni Baba ya Mungu, ingawa mara nyingi anaitwa Baba ya Bwana wetu Yesu.”

Baada ya Emlyn kuchunguza uthibitisho wote alisema hivi kwa usadikisho: “Hakuna andiko hata moja katika Biblia linalosema kwamba Baba, Mwana, na Roho Takatifu ni mtu mmoja.”

TUNAJIFUNZA NINI?

Leo, watu wengi wanaogopa kutetea mafundisho ya Biblia. Lakini Emlyn alikuwa tayari kutetea ukweli wa Biblia. Aliuliza hivi: “Ikiwa mtu hawezi kukubaliana na ukweli muhimu zaidi, unaopatikana waziwazi katika Maandiko matakatifu, basi kwa nini asome na kuchunguza Maandiko?” Emlyn hakulegeza msimamo wake.

Mfano uliowekwa na Emlyn na watu wengine unapaswa kutuchochea tuchunguze kama tuko tayari kutetea ukweli hata tunapodhihakiwa. Sisi pia tunaweza kujiuliza: ‘Ni nini kilicho muhimu​—je, ni kuheshimiwa na kukubaliwa na watu au ni kuunga mkono ukweli wa Neno la Mungu?’