Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Je, Inawezekana Kujua Wakati Ujao?

Je, Inawezekana Kujua Wakati Ujao?

Sisi sote hufikiri kuhusu wakati ujao. Tunajiuliza jinsi maisha yetu na ya wapendwa wetu yatakavyokuwa. Tunajiuliza maswali kama vile: ‘Je, watoto wangu wataishi katika ulimwengu bora? Je, ulimwengu utaangamizwa? Nifanye nini sasa ili niishi vizuri wakati ujao?’ Ni kawaida kwa wanadamu kujiuliza maswali hayo; tunatamani sana kuishi tukiwa na uhakika, utaratibu, na utulivu. Ikiwa ungejua yatakayotokea wakati ujao, ungejitayarisha vizuri kimwili na pia kihisia.

Hivyo basi, je, unajua itakavyokuwa wakati ujao? Je, kuna yeyote anayejua? Wataalamu wanaojaribu kutabiri wakati ujao wamefaulu kwa kiasi fulani lakini pia mara nyingi wao hukosea. Hata hivyo, inasemekana kwamba Mungu anaweza kutabiri kwa usahihi matukio ya wakati ujao. Neno lake linasema hivi: “Tangu mwanzo [ninatangaza] ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.” (Isaya 46:10) Je, sikuzote amekuwa akitabiri kwa usahihi?

UNABII WA MUNGU UMEFANIKIWA KWA KADIRI GANI?

Kwa nini ungependa kujua kama mambo ambayo Mungu ametabiri yametimia kwa usahihi? Kwa kweli, ungefurahi kama ungepata mtu anayeweza kutabiri hali ya hewa ya kila siku kwa usahihi kwa muda mrefu. Bila shaka, ungesikiliza anachosema kuhusu hali ya hewa ya siku inayofuata. Vivyo hivyo, ikiwa ungejua kwamba unabii uliotabiriwa na Mungu wakati uliopita ulitimia kikamili, bila shaka ungetaka kujua anachotabiri kuhusu wakati wako ujao.

Ukuta uliojengwa upya kwenye magofu ya jiji la kale la Ninawi

KUHARIBIWA KWA JIJI KUBWA:

Kwa mfano, lingekuwa jambo la pekee kutabiri kwa usahihi kwamba jiji kubwa, ambalo limedumu kwa miaka mingi, litaanguka. Mungu alimtumia mtumishi wake kutabiri  kuhusu kuharibiwa kwa jiji la Ninawi. (Sefania 2:13-15) Wanahistoria wamepata nini baada ya kufanya utafiti? Katika karne ya saba K.W.K., inaelekea miaka 15 hivi baada ya Mungu kutabiri, Wababiloni na Wamedi walivamia na kulipindua jiji la Ninawi. Kwa kuongezea, Mungu alisema kwamba jiji hilo lingeachwa ‘ukiwa, na jangwa.’ Je, utabiri huo ulitimia? Ndiyo. Ingawa jiji hilo na eneo lililolizunguka lilikuwa na ukubwa wa kilomita 518 za mraba, wavamizi hao hawakumiliki jiji hilo, kama ambavyo ingetazamiwa. Badala yake waliliharibu kabisa. Je, kuna mchanganuzi yeyote wa mambo ya kisiasa ambaye angetabiri matukio hayo kwa usahihi hivyo?

MIFUPA YA WATU INGETEKETEZWA:

Ni nani angethubutu kutangaza​—miaka 300 mapema—jina na ukoo wa mtu ambaye angeteketeza mifupa ya watu kwenye madhabahu, na kutaja mji ambao madhabahu hiyo ingekuwa? Kama utabiri huo ungetimia, bila shaka mtabiri huyo angekuwa maarufu. Nabii wa Mungu alitabiri hivi: “Mwana atazaliwa katika nyumba ya Daudi, ambaye jina lake ni Yosia . . . , naye atateketeza mifupa ya watu” katika madhabahu huko Betheli. (1 Wafalme 13:1, 2) Miaka 300 hivi baadaye, mfalme aliyeitwa Yosia​—jina ambalo halikutumiwa sana katika enzi za Biblia—​alizaliwa kutoka katika ukoo wa Daudi. Kama ilivyotabiriwa, Yosia alituma “watu kuichukua mifupa kutoka katika makaburi . . . , akaiteketeza kwa moto juu ya ile madhabahu” iliyokuwa Betheli. (2 Wafalme 23:14-16) Mwanadamu angewezaje kutabiri kwa usahihi hivyo isipokuwa awe ameongozwa na nguvu za Mungu?

Unabii wa Biblia kuhusu kuanguka kwa utawala wa Babiloni ulitimia kwa usahihi kabisa

KUANGUKA KWA SERIKALI:

Ni jambo la kushangaza kutabiri kwa usahihi jina la mtu—muda mrefu kabla hajazaliwa—ambaye angeongoza mashambulizi na kuangusha serikali kubwa ya ulimwengu, na hata kutaja mbinu isiyo ya kawaida ambayo angetumia. Mungu alitanganza kwamba mwanamume aitwaye Koreshi angeongoza mashambulizi hayo. Koreshi pia angewaweka huru mateka Wayahudi na kuunga mkono kujengwa upya kwa hekalu lao takatifu. Kwa kuongezea, Mungu alitabiri kwamba mbinu ya kivita ya Koreshi ingetia ndani kukausha maji ya mito na akatabiri kwamba malango ya  jiji yangeachwa wazi na hivyo kufanya jiji lishindwe kwa urahisi. (Isaya 44:27–45:2) Je, mambo hayo yote yaliyotabiriwa yalitimia kwa usahihi? Wanahistoria wanakubali kwamba ushindi huo wa Koreshi ulitukia. Jeshi la Koreshi lilitumia mbinu ya hali ya juu kwa kugeuza mkondo wa mto fulani huko Babiloni,​— na hivyo kukausha maji ya mito. Isitoshe, wanajeshi waliingia jijini kupitia malango yaliyokuwa yameachwa wazi. Kisha Koreshi akawaweka huru Wayahudi na kutangaza kwamba wangeweza kulijenga upya hekalu lao huko Yerusalemu. Hilo ni jambo la kushangaza kwa sababu Koreshi hakumwabudu Mungu wa Wayahudi. (Ezra 1:1-3) Ni nani ila Mungu tu ambaye angetabiri matukio hayo ya kihistoria kwa usahihi hivyo?

Tumetaja mifano mitatu inayoonyesha kwamba unabii wa Mungu ulitimia kwa usahihi kabisa. Kuna mifano mingine mingi inayoonyesha kwamba unabii wa Mungu ulitimia. Kiongozi wa Wayahudi aliyeitwa Yoshua alitaja jambo ambalo wasikilizaji wake walilijua aliposema hivi: “Nanyi mnajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.” (Yoshua 23:1, 2, 14) Watu hao hawangeweza kupinga uthibitisho wa kutimia kwa ahadi za Mungu. Hata hivyo, Mungu anatimizaje ahadi zake? Kuna tofauti kubwa kati ya njia za Mungu na njia za wanadamu. Ni muhimu tujue jambo hilo kwa sababu Mungu ametoa matangazo ya pekee ambayo yatatimia hivi karibuni na ambayo yanakuhusu.

TOFAUTI KATI YA UNABII WA MUNGU NA UTABIRI WA WANADAMU

Mara nyingi utabiri wa wanadamu hutegemea utafiti wa kisayansi, uchanganuzi wa habari fulani, au watu wanaodai kuwa na uwezo wa kujua wakati ujao. Baada ya kutabiri, wanadamu hukaa kitako na kungoja waone jinsi mambo yatakavyokuwa.—Methali 27:1.

Tofauti na wanadamu, Mungu anajua mambo yote. Anaelewa vizuri tabia na mwelekeo wa wanadamu; kwa hiyo, akitaka anaweza kujua mapema jinsi ambavyo watu na hata mataifa yatakavyotenda. Lakini Mungu anaweza kufanya mengi zaidi. Anaweza kuongoza mambo na kuhakikisha kwamba unabii wake unatimia. Mungu anasema hivi: “Neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, . . . hakika litafanikiwa.” (Isaya 55:11) Kwa hiyo, baadhi ya utabiri wa Mungu ni kama matangazo. Anahakikisha kwamba unabii wake unatimia kwa usahihi kabisa.

WAKATI WAKO UJAO

Je, kuna utabiri wowote unaotegemeka ambao unahusu wakati wako ujao na wa wapendwa wako? Kama ungejua kwamba kutakuwa na kimbunga, bila shaka ungechukua hatua ili uokoke. Vivyo hivyo, unapaswa kuzingatia unabii wa Biblia. Mungu ametangaza kwamba hivi karibuni kutakuwa na mabadiliko makubwa duniani. (Ona sanduku “ Matangazo ya Mungu Kuhusu Wakati Ujao.”) Wakati huo ujao ni tofauti sana na yale ambayo wataalamu hutabiri.

Hebu fikiria hili: Matukio ya ulimwenguni ni kama hadithi iliyoandikwa. Tayari mambo yote yameandikwa na unaweza kusoma kuhusu yatakayotukia. Mungu anasema hivi: “Ninatangaza tangu mwanzo ule mwisho, . . . Ninasema, ‘Shauri langu mwenyewe litasimama, na kila jambo ambalo ni mapenzi yangu nitafanya.’” (Isaya 46:10) Wewe na familia yako mnaweza kuwa na wakati ujao mzuri. Waulize Mashahidi wa Yehova mambo ambayo Biblia inasema kuhusiana na wakati ujao. Mashahidi wa Yehova si wabashiri, wala hawadai kwamba wanawasiliana na roho au kwamba wana uwezo wa pekee wa kutabiri. Badala yake, wao ni wanafunzi wa Biblia wanaoweza kukuonyesha mambo mazuri ambayo Mungu anataka uyapate wakati ujao.