Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Neno “towashi” linamaanisha nini linapotumiwa katika Biblia?

Mchoro wa towashi uliochorwa na Wasiria

Nyakati nyingine neno towashi humaanisha mwanamume aliyehasiwa. Katika nyakati za Biblia, baadhi ya wanaume walihasiwa kama adhabu au kwa sababu walikuwa mateka wa vita au watumwa. Wanaume waliohasiwa walifanya kazi kwenye makao ya kifalme au walisimamia nyumba za wanawake. Kwa mfano, matowashi Hegai na Shaashgazi walifanya kazi ya kuwalinda wake na masuria wa Mfalme Ahasuero wa Milki ya Uajemi, anayejulikana kama Shasta wa I.—Esta 2:3, 14.

Hata hivyo, si watu wote wanaoitwa matowashi kwenye Biblia walikuwa wamehasiwa. Baadhi ya wasomi wa lugha za awali wanasema kwamba neno towashi lilikuwa na maana pana. Lingeweza kumaanisha pia ofisa wa cheo cha juu aliyefanya kazi kwenye makao ya mfalme. Kwa hiyo inaelekea kwamba Ebed-meleki rafiki yake Yeremia, na yule Mwethiopia aliyehubiriwa na Filipo hawakuwa matowashi waliohasiwa. Ebed-meleki alikuwa ofisa wa cheo cha juu kwa sababu aliweza kuonana ana kwa ana na Mfalme Sedekia. (Yeremia 38:7, 8) Pia, towashi Mwethiopia anatajwa kuwa alikuwa mweka-hazina, na “alikuwa ameenda Yerusalemu kuabudu.”—Matendo 8:27.

Kwa nini wachungaji katika nyakati za Biblia walitenganisha kondoo na mbuzi?

Alipokuwa akieleza kuhusu wakati ujao wa hukumu, Yesu alisema hivi: “Wakati Mwana wa binadamu atakapofika katika utukufu wake, . . . atawatenganisha watu, mmoja kutoka kwa mwenzake, kama vile mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi.” (Mathayo 25:31, 32) Kwa nini wachungaji katika nyakati za Biblia ­walitenganisha kondoo na mbuzi?

Kwa kawaida, wakati wa mchana kondoo na mbuzi walikusanywa na kulishwa pamoja. Wakati wa usiku walifungiwa mabandani ili kuwalinda dhidi ya baridi, wezi, na wanyama mwitu. (Mwanzo 30:32, 33; 31:38-40) Wanyama hao walitenganishwa ili kuwalinda kondoo ambao kiasili ni watulivu, na hasa kondoo wadogo na majike, ili wasiumizwe na mbuzi ambao kwa kawaida hufanya fujo. Pia mchungaji alitenganisha kondoo na mbuzi wakati wa “kuwakamua maziwa, kuwakata manyoya, na hata wakati wa kuzaa,” kinasema kitabu kinachoitwa All Things in the Bible. Mifano ambayo Yesu alitumia alipofundisha ilitokana na mambo ambayo wasikilizaji wake waliyafahamu vizuri katika maeneo ya wafugaji kama ilivyokuwa katika taifa la kale la Israeli.