Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Urithi Uliodumu kwa Vizazi Saba

Urithi Uliodumu kwa Vizazi Saba

Watu husema kwamba nimefanana sana na baba yangu. Wanasema kwamba nimerithi kila kitu kutoka kwake, mwonekano wangu, macho yangu, na ucheshi. Hata hivyo, ameniachia kitu kingine, urithi uliothaminiwa na vizazi saba katika familia yetu. Acheni nisimulie.

Nikijifunza kuhusu urithi wa familia yetu pamoja na baba yangu

Babu yangu, Thomas (1) * Williams, alizaliwa Januari 20, 1815 katika mji wa Horncastle, Uingereza. Mama yake alikufa miaka miwili baadaye, hivyo yeye na ndugu zake watatu walilelewa na baba yao, John Williams. John alimzoeza Thomas ufundi wa useremala, hata hivyo Thomas alipenda kufanya kazi tofauti.

Nchini Uingereza, watu walianza tena kupendezwa na dini. Mhubiri John Wesley alijitenga na Kanisa la Anglikana ili kuanzisha Kikundi cha Wamethodisti kilichokazia kujifunza kibinafsi Biblia na kufanya kazi ya kutangaza injili. Mafundisho ya Wesley yalisambaa kila mahali, hata familia ya Williams ilikubali mafundisho hayo. Thomas akaanza kuwa mhubiri wa dini ya Wesley, na mara moja akajitolea kufanya kazi ya umishonari Pasifiki Kusini. Mnamo Julai 1840, Thomas na mke wake, Mary, (2) walifika katika Kisiwa cha Lakeba, * Fiji, kisiwa kilichotokezwa na mlipuko wa volkano, na kilichokuwa na wenyeji waliokuwa na zoea la kula watu.

KUISHI MIONGONI MWA WANAOKULA WATU

Thomas na Mary walikabili hali nyingi ngumu walipoanza kuishi Fiji. Walifanya kazi kwa saa nyingi chini ya mazingira magumu na joto kali. Pia, walikabili mambo mengi yenye kuogopesha kama vile vita vya kikabila, kunyongwa kwa wajane, mauaji ya watoto wachanga, ulaji wa nyama za watu, na kwa ujumla wenyeji walipinga ujumbe wao. Mary na mwana wake wa kwanza, John, waliugua sana na karibu wafe. Katika mwaka wa 1843, Thomas aliandika hivi: “Nilikuwa na mahangaiko mengi sana moyoni. . . . Nilikuwa nimekata tamaa kabisa.” Pamoja na hali hizo, Thomas na Mary walivumilia na kuendelea kupata nguvu kwa sababu ya kuwa na imani kwa Yehova Mungu.

Baada ya muda, Thomas alitumia vizuri ustadi wake wa useremala kwa kujenga nyumba ya kwanza Fiji iliyofuata mtindo wa nyumba zilizojengwa Ulaya. Nyumba hiyo ilikuwa na orofa na mambo mengine mapya yaliyofanya wenyeji wengi wa Fiji wavutiwe nayo. Kabla tu nyumba hiyo haijakamilika kujengwa, Mary alijifungua mwana wake wa pili, Thomas Whitton3 Williams, babu yangu.

Mnamo 1843, Thomas Williams alisaidia kutafsiri Injili ya Yohana katika Kifiji, jambo ambalo halikuwa rahisi kwake. * Hata hivyo, alikuwa mwana anthropolojia mwenye kipawa cha kuchunguza mambo. Aliandika uchunguzi wake wote kwa uangalifu katika kitabu chake kilichoitwa, Fiji and the Fijians (1858), ambacho kilizungumzia maisha ya watu wa Fiji katika karne ya 19.

Kwa sababu ya hali ngumu aliyokabili kwa miaka 13 akiwa Fiji, afya ya Thomas ilianza kuwa mbaya, hivyo yeye na familia yake walihamia Australia. Baada ya kufanya kazi bora na kwa muda mrefu akiwa kasisi, Thomas alikufa mwaka wa 1891, huko Ballarat, Victoria.

“DHAHABU” UPANDE WA MAGHARIBI

Katika mwaka wa 1883, Thomas Whitton Williams na mke wake, Phoebe (4) walihamia Perth, mji ulio Magharibi mwa Australia. Mtoto wao wa pili, Arthur Bakewell (5) Williams, babu yangu, alikuwa na umri wa miaka tisa.

Arthur alipokuwa na umri wa miaka 22, alihamia katika mji wa Kalgoorlie, kilomita 600 hivi mashariki mwa Perth, mji uliokuwa unasitawi kwa sababu ya kuwa na migodi ya dhahabu. Akiwa huko, alisoma machapisho yaliyochapishwa na Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyokuwa wakijulikana wakati huo. Aliomba pia kutumiwa gazeti la Zion’s Watch Tower. Kwa sababu ya kuvutiwa na kile alichosoma, Arthur alianza kuhubiria wengine ujuzi mpya alioupata na kufanya mikutano ya kujifunza Biblia. Huo ndio uliokuwa mwanzo wa Mashahidi wa Yehova Magharibi mwa Australia.

Arthur aliwaambia pia washiriki wa familia yao mambo aliyokuwa akijifunza. Baba yake, Thomas Whitton, aliunga mkono jitihada za Arthur za kushirikiana na Wanafunzi wa Biblia ingawa alikufa baada ya muda mfupi. Mama yake, Phoebe, na dada zake, Violet na Mary walianza pia kuwa Wanafunzi wa Biblia. Violet akawa mweneza injili wa wakati wote, au painia. Arthur alisema kwamba “Violet alikuwa painia mwenye bidii na mwenye kuchukua mambo kwa uzito Australia Magharibi.” Huenda maneno hayo ya Arthur yakawa ya upendeleo, hata hivyo, bidii ya Violet ilichochea sana kizazi kilichofuata cha akina Williams.

Baada ya muda, Arthur alifunga ndoa na kuhamia Donnybrook, mji uliojulikana kwa kulima matunda, kusini magharibi mwa Australia Magharibi. Alipewa jina la utani, “Mzee Aliyechanganyikiwa na mwaka wa 1914!” kwa sababu ya bidii yake ya kutangaza unabii wa Biblia unaozungumzia mwaka huo. * Watu waliacha kumtania Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipotokea. Arthur aliwahubiria kwa ukawaida wateja wake waliokuja kununua vitu katika duka lake ambapo aliweka machapisho ya Biblia kwa ukawaida katika dirisha. Pia, aliweka tangazo dirishani lililosema kwamba mtu yeyote ambaye angeweza kuthibitisha fundisho la Utatu—fundisho lisilopatana na maandiko ambalo Arthur alilipinga kwa uthabiti, angepewa pauni 100. Hakuna mtu aliyepata pesa hizo.

Nyumba ya familia ya Williams ilianza kuwa kituo cha kikundi cha funzo la Biblia na mikutano ya kutaniko katika mji wa Donnybrook. Baadaye, Arthur alijenga Jumba la Ufalme, au jengo la mikutano katika mji huo— lililokuwa mojawapo ya jengo la kwanza, Australia Magharibi. Hata alipokuwa na umri wa miaka 70, bado angevaa suti na tai na kisha kupanda farasi wake mzee aliyeitwa Doll, na kwenda kuhubiri maeneo ya mbali kuzunguka wilaya ya Doonybrook.

Watoto wa Arthur walichochewa sana na baba yao aliyekuwa mkimya na mwenye heshima, lakini mwenye bidii. Binti yake, Florence (6) alitumika akiwa mmishonari nchini India. Watoto wake, Arthur Lindsay (7) na Thomas, walitumika kwa muda mrefu wakiwa wazee wa kutaniko, kama tu baba yao.

MATOFAA MATAMU YA MAMA WILLIAMS

Babu yangu, Arthur Lindsay Williams, alijulikana sana na kupendwa na wengi kwa sababu ya kuwa mwenye fadhili. Alikuwa tayari kusikiliza yeyote aliyetaka kuongea naye, na aliwatendea kwa heshima. Alikuwa pia bingwa wa mashindano ya mkoa ya kukata kuni kwa kutumia shoka, baada ya kushinda mara 18 katika mashindano hayo kwa miaka 12.

Hata hivyo, Arthur hakufurahi wakati mwana wake mwenye umri wa miaka miwili, Ronald (8) (babu yangu), alipokata kwa shoka mti mdogo wa mtofaa uliokuwa karibu na nyumba. Mama ya Ronald aliufunga kwa uangalifu mti huo ili kuunganisha tena pamoja, nao ulizaa matofaa matamu sana. Matofaa hayo yaliyokuja kuitwa matofaa ya Mama Williams yalikuja kuwa mwanzo wa matofaa maarufu sana duniani yanayoitwa Cripps Pink.

Ronald, au Babu, kama ninavyomwita, alianza kufuatilia mambo ya maana zaidi. Babu na Nyanya yangu walitumika kwa miaka mingi wakiwa wajitoleaji katika miradi ya ujenzi ya Mashahidi nchini Australia na Visiwa vya Solomon. Sasa akiwa na umri unaokaribia miaka 80, Babu bado anatumika akiwa mzee wa kutaniko na anasaidia kujenga na kukarabati Majumba ya Ufalme katika Australia Magharibi.

KUHESHIMU URITHI WANGU

Wakiwa wanafuata urithi wa familia yetu, wazazi wangu, Geoffrey (9) na Janice (10) Williams, walijitahidi sana kumlea dada yangu Katharine na mimi kulingana na kanuni za Kikristo. Nilipokuwa na umri wa miaka 13, niliruhusu kanuni hizo ziongoze maisha yangu. Nilipohudhuria kusanyiko la Kikristo, John E. Barr, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alitoa hotuba na kuwachochea vijana waliohudhuria kusanyiko hilo kwa kusema hivi: “Msipoteze kitu chenye thamani sana mlicho nacho, yaani, nafasi ya kumjua na kumpenda Yehova.” Usiku huohuo nilijiweka wakfu kwa Yehova. Baada ya miaka miwili, nilianza kufanya upainia.

Leo, mimi (12) ninafurahia sana kuhubiri wakati wote pamoja na mke wangu, Chloe, (11) huko Tom Price, mji wenye migodi ulio kaskazini-magharibi mwa Australia Magharibi. Tunafanya kazi ya muda ili kujiruzuku. Wazazi wangu na dada yangu, Katharine na mume wake, Andrew, wanafanya upainia katika mji wa Port Hedland, ulio kilomita 420 kaskazini. Mimi na baba yangu tunatumika tukiwa wazee wa kutaniko.

Vizazi saba vilivyopita, babu yangu Thomas Williams aliazimia kumtumikia Yehova Mungu. Urithi huo wa imani na utumishi umepitishwa kwangu. Ninahisi kwamba nimebarikiwa sana kuwa na urithi huo mwingi wa kiroho.

^ Nambari hiyo inaonyesha mhusika aliye katika picha zinazofuata.

^ Kisiwa hicho ambacho zamani kiliitwa Lakemba, kinapatikana miongoni mwa Kikundi cha visiwa vya Lau vilivyo mashariki mwa Fiji.

^ John Hunt aliyekuwa mmishonari, alitafsiri kwa kiasi kikubwa Agano Jipya katika Kifiji na kuichapisha mwaka wa 1847. Tafsiri hiyo inajulikana kwa sababu inatumia jina la Mungu, “Jiova” katika lugha ya Kifiji.

^ Ona nyongeza yenye kichwa “1914—Mwaka Muhimu Katika Unabii wa Biblia” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova na kinachopatikana pia katika www.pr418.com/sw.