Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inasema Nini Kuhusu Tatizo la Maji Ulimwenguni?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Tatizo la Maji Ulimwenguni?

 Sisi sote tunahitaji maji safi ili tuendelee kuwa hai. Lakini kama anavyosema António Guterres, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa “maji safi yanazidi kupungua, kwa hiyo, tunakabili tatizo kubwa la maji ulimwenguni.” Tayari ulimwenguni pote mabilioni ya watu hawawezi kupata maji safi ya kunywa.

Strdel/AFP via Getty Images

 Je, kuna wakati ambapo kila mtu atakuwa na maji ya kutosha? Au je, sikuzote tutalazimika kupambana na matatizo ya maji? Biblia inasema nini?

Ahadi ya Biblia kuhusu maji

 Biblia inasema kwamba siku moja upungufu wa maji utakwisha. Kwa kweli, kutakuwa na maji safi, na yatakuwa mengi sana.

 “Maji yatabubujika nyikani, na vijito katika jangwa tambarare. Na ardhi iliyokaushwa na joto itakuwa kama dimbwi lenye matete, na ardhi yenye kiu itakuwa kama mabubujiko ya maji.”​—Isaya 35:6, 7.

 Kwa nini tunaweza kuamini ahadi hiyo ya Biblia? Fikiria kile ambacho Biblia inasema kuhusu jinsi sayari yetu ilivyoumbwa.

Kile ambacho Biblia inasema kuhusu dunia na mzunguko wa maji

 “[Mungu] hakuiumba [dunia] tu bila sababu, lakini aliiumba ili ikaliwe.”​—Isaya 45:18.

 Kwa kuwa Mungu aliumba dunia ili viumbe hai wakae ndani yake, alibuni mifumo ya asili ambayo ingetokeza maji mengi safi.

 “[Mungu] huvuta juu matone ya maji; yanaganda na kuwa mvua kutokana na ukungu wake; kisha mawingu huyamwaga chini; yanawanyeshea wanadamu.”​—Ayubu 36:27, 28.

 Kwa maneno rahisi, mistari hiyo inafafanua mfumo wa asili na unaotegemeka uliobuniwa na Mungu wa kusafisha na kusambaza maji. Maji yanavukizwa kutoka ardhini na baharini, yanagandamana, na kumwagika yakiwa mvua, na mzunguko huo unahakikisha wanadamu na wanyama wanapata maji safi kwa ukawaida.​—Mhubiri 1:7; Amosi 5:8.

 “Nitawaletea mvua katika majira yanayofaa, nayo nchi itazaa kwa wingi, na miti ya matunda itazaa matunda mengi.”​—Mambo ya Walawi 26:4.

 Kwa kuwa Waisraeli wa kale walikuwa taifa la wakulima, Mungu aliahidi kuwabariki kwa kuwapa maji ya kutosha ambayo yangewawezesha kuvuna chakula kingi. Mungu anajua kwamba ili mazao yapatikane kwa wingi, mvua za kutosha zinahitajika kwa wakati unaofaa.

 Mungu atahakikisha kwamba hivi karibuni mvua zinapatikana duniani pote kama ilivyokuwa kwa Waisraeli wa kale. (Isaya 30:23) Kwa sasa, tatizo la maji linaongezeka katika sehemu nyingi ulimwenguni, na tatizo hilo halisababishwi na ukosefu wa mvua peke yake. Biblia inasema nini kingine kuhusu kutatua tatizo la maji leo?

Jinsi tatizo la maji litakavyokwisha

 Biblia inafunua kwamba Mungu atatua matatizo yaliyopo duniani leo kupitia Ufalme wake, kutia ndani tatizo la maji. (Mathayo 6:9, 10) Ufalme wa Mungu ni serikali iliyo mbinguni ambayo itatawala dunia yote. (Danieli 2:44; Ufunuo 11:15) Isitoshe, Ufalme wa Mungu utafanya kile ambacho serikali za wanadamu zimeshindwa kufanya—utaondoa mambo yote yanayosababisha tatizo la maji.

 Tatizo: Mabadiliko ya hali ya hewa yanatokeza hitilafu katika mzunguko wa maji. Madhara yanayotokea yanatia ndani ukame mbaya na pia mafuriko, iwe ni kutokana na mvua kubwa kupita kiasi au kuongezeka kwa kiwango cha maji baharini.

 Suluhisho: Ufalme wa Mungu utarekebisha madhara katika mazingira ili sayari yetu irudie hali ya kawaida. Mungu ameahidi: “Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” (Ufunuo 21:5) Maeneo yenye ukame yatakuwa na maji mengi na hivyo kufanya viumbe vifurahie kuishi katika maeneo ambayo sasa hayakaliki. (Isaya 41:17-20) Chini ya Yesu Kristo, Ufalme wa Mungu utadhibiti nguvu za asili za dunia.

 Yesu alipokuwa duniani alituliza dhoruba kali na hilo linaonyesha kwamba Mungu alikuwa amempatia nguvu nyingi sana. (Marko 4:39, 41) Kristo, Mfalme wa Ufalme wa Mungu, atakomesha majanga yote ya asili. Watu watafurahia amani na usalama wa kweli, hawatahofu tena majanga ya asili.

 Tatizo: Leo kuna mashirika yenye pupa na pia baadhi ya watu hawafikirii madhara yanayotokana na mambo wanayofanya. Kwa hiyo, wanachafua mito, maziwa, na maji yaliyo ardhini na kufanya hivyo kunachangia ukosefu wa maji safi.

 Suluhisho: Mungu ataisafisha dunia na kuondoa madhara ambayo yameipata mito, maziwa, bahari, na ardhi. Dunia itakuwa paradiso. Biblia inasema hivi katika lugha ya kishairi: “Nyika na nchi iliyokauka zitafurahi, na jangwa tambarare litashangilia na kuchanua maua kama zafarani.”​—Isaya 35:1.

 Ni nini kitakachowapata wale ambao hawajali mazingira na pia wanadamu wenzao? Mungu ameahidi “kuwaangamiza wale wanaoiangamiza dunia.”​—Ufunuo 11:18, maelezo ya chini; Methali 2:21, 22.

 Tatizo: Maji ni rasilimali ambayo imekuwa ikitumiwa vibaya, kwa hiyo utumiaji umezidi sana kiwango cha maji ambacho dunia inatokeza.

 Suluhisho: Ufalme wa Mungu utahakikisha kwamba ni mapenzi ya Mungu—na si ya wanadamu wenye ubinafsi—ambayo ‘yatatendeka duniani.’ (Mathayo 6:9, 10) Ufalme wa Mungu utawapa raia zake hapa duniani elimu bora kabisa. Isaya 11:9 a inasema: “Kwa hakika dunia itajaa ujuzi kumhusu Yehova.” Ujuzi huo pamoja na upendo wao kwa Mungu na viumbe wake wote utawawezesha wanadamu kutunza kikamili sayari yetu maridadi na rasilimali zake.

  •   Ili kujua mengi zaidi kuhusu mambo ambayo Ufalme wa Mungu utafanya, soma makala yenye kichwa “Ufalme wa Mungu Utatimiza Nini?

  •    Nenda kwenye sura ya 35 ya kitabu cha Isaya kwenye Biblia, ujisomee jinsi dunia itakavyofanywa kuwa paradiso.

  •    Tazama video Kwa Nini Mungu Aliiumba Dunia? ili ujifunze mengi zaidi kuhusu kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia na wanadamu.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala “Yehova Ni Nani?