Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

ENDELEA KUKESHA!

Dunia Inaharibiwa—Biblia Inasema Nini?

Dunia Inaharibiwa—Biblia Inasema Nini?

 “Hivi karibuni sana kutakuwa na janga la hali ya hewa. Majiji makubwa yatafunikwa na maji. Joto linalopita kiasi. Dhoruba zenye kutisha. Ukosefu mkubwa wa maji. Kutoweka kwa jamii milioni moja za mimea na wanyama. Haya si mambo ya kuwaziwa au yaliyotiliwa chumvi. Ni mambo ambayo sayansi inatueleza yatatokea kwa sababu ya sera zetu za sasa za kuzalisha nishati.”​—Hotuba ya António Guterres, katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, kuhusu Jopo la Serikali Mbalimbali Kuhusu Mabadiliko ya Hali ya Hewa ripoti iliyotolewa Aprili 4, 2022.

 “Wanasayansi wanatoa onyo kwamba katika miaka ijayo uharibifu unaotokana na mabadiliko ya hali ya hewa utaathiri mbuga zote 423 za wanyama [nchini Marekani], kwa kuwa zinaathiriwa zaidi na kupanda kwa joto ulimwenguni. Maonyo yanayotolewa tena na tena yanasikika kama yale tunayosoma katika Biblia: moto na mafuriko, kuyeyuka kwa miamba ya barafu, kupanda kwa kiwango cha maji baharini na mawimbi ya joto.”​—“Hali Mbaya ya Mafuriko Katika Yellowstone, Ishara ya Majanga Yatakayokuja,” The New York Times, Juni 15, 2022.

 Je, matatizo ya hali mbaya ya mazingira ya dunia yanaweza kutatuliwa? Ikiwa ndivyo, ni nani atakayeyatatua? Chunguza kile ambacho Biblia inasema.

Kuharibiwa kwa mazingira kulitabiriwa

 Biblia inasema kwamba Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Mstari huo wa Biblia unatufundisha mambo matatu:

  1.  1. Matendo ya wanadamu yataharibu dunia kwa kiwango kikubwa.

  2.  2. Kutakuwa na mwisho kwa uharibifu unaoendelea duniani.

  3.  3. Mungu ndiye atakayetatua matatizo ya mazingira ya dunia, si wanadamu.

Wakati ujao wa sayari yetu uko salama

 Biblia inasema kwamba “dunia inadumu milele.” (Mhubiri 1:4) Itakaliwa sikuzote.

  •   “Waadilifu wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.”​—Zaburi 37:29.

 Afya ya sayari yetu itarekebishwa kabisa.

  •   “Nyika na nchi iliyokauka zitafurahi, na jangwa tambarare litashangilia na kuchanua maua kama zafarani.”​—Isaya 35:1.