Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

ENDELEA KUKESHA!

Kwa Nini Siasa Inasababisha Migawanyiko?​—Biblia Inasema Nini?

Kwa Nini Siasa Inasababisha Migawanyiko?​—Biblia Inasema Nini?

 Ulimwenguni pote watu wamegawanyika kwa sababu wana maoni tofauti ya kisiasa. Kulingana na utafiti uliofanywa mwaka wa 2022 na shirika la Pew Research Center, “Asilimia 65 ya watu wazima katika nchi 19 walisema kwamba nchini mwao watu wanaounga mkono vyama tofauti vya kisiasa hawakubaliani au hata hawaelewani kabisa.”

 Mahali unapoishi, je, watu wamekuwa na migawanyiko mingi zaidi kwa sababu ya siasa? Kwa nini inakuwa hivyo? Je, kuna suluhisho? Biblia inasema nini kuhusu jambo hilo?

Mitazamo inayosababisha migawanyiko

 Biblia ilitabiri kwamba katika siku zetu, yaani, “siku za mwisho,” watu wengi wangekuwa na mitazamo ambayo ingefanya iwe vigumu sana kuwa na umoja.

  •   “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, . . . wasiotaka makubaliano yoyote.”​—2 Timotheo 3:1-3.

 Licha ya jitihada ambazo watu wengi wanafanya, bado serikali zinashindwa kutimiza majukumu yake kikamili. Inakuwa vigumu kwa watu wenye maoni yanayotofautiana kushirikiana ili kutatua matatizo. Hilo linathibitisha ukweli wa jambo ambalo Biblia ilitaja miaka mingi iliyopita.

  •   “Mwanadamu amemtawala mwanadamu mwenzake kwa kumuumiza.”​—Mhubiri 8:9.

 Hata hivyo, Biblia inataja suluhisho—serikali inayoongozwa na mtu ambaye ana uwezo wa kuondoa matatizo yanayowasumbua wanadamu leo.

Kiongozi anayejali na mwenye uwezo

 Biblia inamzungumzia kiongozi mwenye uwezo wa pekee: Yesu Kristo. Yesu ana nguvu, mamlaka, na anatamani kuleta umoja na amani kwa wanadamu wote.

  •   “Katika siku zake mwadilifu atasitawi, na amani itakuwa nyingi.”​—Zaburi 72:7.

  •   “Mataifa yote yatamtumikia.”​—Zaburi 72:11.

 Yesu ni kiongozi bora kwa sababu anawajali watu na anataka kuwasaidia, hasa wale ambao wametendewa kwa njia isiyo ya haki.

  •   “Atamwokoa maskini anayelilia msaada, pia mtu wa hali ya chini na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamhurumia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataokoa uhai wa maskini. Atawaokoa kutoka katika ukandamizaji na ukatili.”​—Zaburi 72:12-14.

 Jifunze mengi zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu, serikali iliyo mbinguni ambayo kiongozi wake ni Yesu. Pata kujua jinsi unavyoweza kunufaika kutokana nayo na jinsi unavyoweza kuiunga mkono.