Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

kovop58/stock.adobe.com

ENDELEA KUKESHA!

Je, Kweli Michezo ya Olimpiki Inaweza Kutokeza Umoja?​—⁠Biblia Inasema Nini?

Je, Kweli Michezo ya Olimpiki Inaweza Kutokeza Umoja?​—⁠Biblia Inasema Nini?

 Inakadiriwa kwamba watu bilioni tano hivi ulimwenguni watawatazama wanariadha kutoka nchi 206 wakishiriki katika Michezo ya Olimpiki ya 2024. Thomas Bach, rais wa Shirikisho la Kimataifa la Olimpiki alisema hivi: “Sisi ni sehemu ya tukio linalounganisha ulimwengu katika amani. Acheni sote tuheshimu wazo linaloendelezwa na michezo ya Olimpiki kwamba wanadamu wote wanapaswa kuishi kwa amani na umoja, licha ya kwamba tumetoka katika nchi tofauti-tofauti.”

 Je, michezo ya Olimpiki inaweza kutimiza malengo hayo makubwa? Je, tutawahi kuwa na amani na umoja wa kweli?

Je, michezo hiyo itatokeza amani na umoja?

 Michezo ya Olimpiki ya mwaka huu imewafanya watu wafikirie kuhusu mengi zaidi ya michezo tu. Michezo hiyo imekazia masuala ya kijamii na ya kisiasa inayowatenganisha watu. Masuala hayo yanatia ndani haki za kibinadamu, ubaguzi wa rangi, ubaguzi wa kidini, na ukosefu wa usawa.

 Michezo ya kimataifa kama vile Olimpiki huandaa nafasi ya watu kujiburudisha. Hata hivyo, matukio hayo hutokeza pia nafasi ya kuonyesha na kuendeleza mitazamo na matendo yanayowatenganisha watu badala ya kutokeza amani na umoja.

 Biblia ilitabiri kuhusu mitazamo ambayo watu wangekuwa nayo inayofanya iwe vigumu sana kuwe na umoja leo. (2 Timotheo 3:1-5) Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu unabii huo wa Biblia, soma makala yenye kichwa “Je, Biblia Ilitabiri Mitazamo na Matendo ya Watu Leo?

Tumaini la kweli la kupata amani na umoja ulimwenguni

 Biblia inatoa tumaini linaloweza kuaminika la kupata amani na umoja ulimwenguni. Inaahidi kwamba watu wote duniani wataunganishwa chini ya serikali ya mbinguni inayoitwa “Ufalme wa Mungu.”​—Luka 4:43; Mathayo 6:10.

 Yesu Kristo, Mfalme wa Ufalme huo, ataleta amani ulimwenguni pote. Biblia inasema:

  •   “Mwadilifu atasitawi, na amani itakuwa nyingi.”​—Zaburi 72:7.

  •   “Atamwokoa maskini anayelilia msaada . . . Atawaokoa kutoka katika ukandamizaji na ukatili.”​—Zaburi 72:12, 14.

 Hata leo, mafundisho ya Yesu yamewaunganisha mamilioni ya watu katika nchi 239. Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wamejifunza kuishi kwa amani wakiwa Wakristo. Ili ujifunze jinsi wamefaulu kufanya hivyo, soma toleo la gazeti Mnara wa Mlinzi lenye kichwa “Jinsi ya Kushinda Chuki.”