Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Maisha Yatarudia Hali ya Kawaida Tena? Biblia Inaweza Kutusaidiaje Kuishi Katika Ulimwengu Uliobadilishwa na Janga?

Je, Maisha Yatarudia Hali ya Kawaida Tena? Biblia Inaweza Kutusaidiaje Kuishi Katika Ulimwengu Uliobadilishwa na Janga?

 “Sote tunataka maisha yetu yarudie hali ya kawaida.”—Angela Merkel, Kansela wa Ujerumani.

 Huenda ukakubaliana na maneno yake kwa sababu janga la COVID-19 linaendelea kuwaathiri watu ulimwenguni pote. Lakini hiyo inayoitwa “hali ya kawaida” ndiyo ipi? Watu wana matumaini gani?

  •   Kurudia maisha yao ya awali. Baadhi ya watu wanatamani kuchangamana na wengine, kuwakumbatia, kuwasalimu kwa mkono, na pia kuweza kusafiri. Dakt. Anthony Fauci a anasema watu wanahisi kwamba “kurudia hali ya kawaida” kunahusisha kuweza kutembelea “mikahawa, kumbi za sinema, [na] mambo kama hayo.”

  •   Kuboresha maisha yao. Watu fulani wanaona kwamba huenda wakawa na maisha bora kuliko awali. Wanahisi kwamba mabadiliko yanahitajika katika masuala mbalimbali, kama vile kuhusiana na kazi zinazodai muda na nguvu nyingi, ukosefu wa haki na usawa, na kuzorota kwa afya ya akili. Klaus Schwab, mwanzilishi wa Mkutano wa Baraza la Uchumi wa Dunia anasema hivi, “Janga hili linatupatia nafasi ya pekee ya kutafakari na kufanya mabadiliko ulimwenguni.”

 Watu wengine wamefadhaishwa sana na janga hili hivi kwamba wanahisi maisha hayatawahi kuwa ya kawaida tena. Kwa mfano, wengi wamepoteza kazi, makao, afya nzuri, na kwa kusikitisha hata zaidi, wamepoteza wapendwa wao katika kifo.

 Bila shaka, hakuna mtu anayeweza kusema jinsi ulimwengu utakavyokuwa baada ya janga hili kwisha. (Mhubiri 9:11) Hata hivyo, Biblia inaweza kutusaidia kuona mambo kwa njia halisi na kukabiliana na hali zozote zitakazojitokeza. Isitoshe, Biblia inazungumzia jinsi ambavyo wakati ujao utakuwa kihalisi, kwa njia ambayo huenda hukutarajia.

Kuwa na maoni yanayofaa kuhusu janga la COVID-19

 Zamani, Biblia ilitabiri kwamba magonjwa ya kuenea, au “tauni,” yangetokea katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Luka 21:11, Union Version; Mathayo 24:3) Tukikumbuka jambo hilo tunapofikiria kuhusu COVID-19, tutaiona kuwa moja kati ya matukio makubwa ambayo Biblia ilitabiri—yanayotia ndani vita, matetemeko makubwa ya ardhi, na upungufu wa chakula.

 Jinsi kujua hilo kunavyotusaidia: Ingawa huenda makali ya janga hili yakapungua, Biblia inaonya kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Kujua hilo kunaweza kutusaidia kuwa na matarajio halisi kuhusu maisha katika nyakati hizi ngumu.

 Biblia inatusaidia kuwa na maoni yanayofaa: Ulimwengu wetu unaokabiliwa na changamoto nyingi zaidi kila siku, hivi karibuni utapatwa na badiliko kubwa sana. Badiliko gani?

Maisha ya wakati ujao

 Mbali tu na kutabiri kuhusu matatizo makubwa tunayoona sasa, Biblia ilitabiri pia kuhusu hali nzuri ambazo zitakuja hivi karibuni. Inafafanua kuhusu wakati ujao bora kuliko ule ambao serikali za wanadamu zinaweza kutokeza. Unaweza kutokezwa tu na Mungu. “Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.

 Yehova b Mungu anaahidi hivi: “Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” (Ufunuo 21:5) Atatatua matatizo yote ya ulimwengu, kutia ndani yale yaliyofanywa kuwa mabaya zaidi na janga hili. Ataandaa mambo yafuatayo:

  •   Afya kamilifu ya mwili na akili, na hakutakuwa tena na magonjwa wala kifo.—Isaya 25:8; 33:24.

  •   Kazi yenye kuridhisha inayowafanya watu kuridhika kabisa, si kazi zenye kuchosha na zinazosababisha mkazo.—Isaya 65:22, 23.

  •   Watu wote watakuwa na hali nzuri bila umaskini na njaa.—Zaburi 72:12, 13; 145:16.

  •   Maumivu ya kihisia ambayo umewahi kupata yatasahaulika, na utawaona wapendwa waliokufa wakifufuliwa.—Isaya 65:17; Matendo 24:15.

 Jinsi kujua hilo kunavyotusaidia: Biblia inasema: “Tuna tumaini hilo kama nanga ya uhai wetu.” (Waebrania 6:19, maelezo ya chini) Kuwa na tumaini la wakati ujao mzuri kunaweza kutusaidia kuwa na usawaziko. Kunaweza kutusaidia kukabiliana na matatizo ya leo, kupunguza wasiwasi, na kuwa na hali nzuri ya kihisia.

 Lakini je, kweli unaweza kuamini ahadi za Biblia? Ona makala yenye kichwa “Biblia—Chanzo Kinachotegemeka cha Kweli.”

Kanuni za Biblia za kutusaidia kukabiliana na hali baada ya janga hili

  •   Thamini uhai

     Andiko: “Hekima humhifadhi hai yule aliye nayo.”—Mhubiri 7:12.

     Hilo linamaanisha nini kwako? Fanya maamuzi yenye hekima ili kupunguza uwezekano wa kuwa mgonjwa. Changanua hatari iliyopo katika eneo lenu. Zingatia miongozo ya afya na usalama, kiwango cha maambukizi katika eneo lenu, na asilimia ya watu waliopata chanjo kamili.

  •   Endelea kuwa na tahadhari

     Andiko: “Mwenye hekima hujihadhari na kuepuka uovu, lakini mpumbavu hajali, naye anajiamini kupita kiasi.”—Methali 14:16.

     Hilo linamaanisha nini kwako? Endelea kuchukua tahadhari zinazofaa za kulinda afya yako. Wataalamu wanakadiria kwamba ugonjwa wa corona utakuwepo kwa muda mrefu.

  •   Zingatia habari zinazotegemeka

     Andiko: “Mjinga huamini kila neno, lakini mwerevu hutafakari kila hatua.”—Methali 14:15.

     Hilo linamaanisha nini kwako? Chagua kwa uangalifu utafuata ushauri gani. Maamuzi unayofanya ni muhimu. Unaweza kudhuru afya yako kwa kufanya maamuzi yanayotegemea habari zisizo za kweli.

  •   Dumisha mtazamo mzuri

     Andiko: “Usiulize: ‘Mbona siku za zamani zilikuwa bora kuliko hizi?’ kwa maana hukuuliza hivyo kwa hekima.”—Mhubiri 7:10.

     Hilo linamaanisha nini kwako? Jitahidi kuishi kwa njia bora zaidi kadiri hali zako zinavyoruhusu. Epuka kukazia fikira wazo la kwamba maisha yalikuwa mazuri kabla ya janga hili, wala usifikirie mambo ambayo hukuweza kufanya kwa sababu ya vizuizi vilivyoletwa na janga hili.

  •   Waheshimu wengine

     Andiko: “Waheshimuni watu wa namna zote.”—1 Petro 2:17.

     Hilo linamaanisha nini kwako? Watu wametenda kwa njia tofauti kwa sababu ya janga hili na madhara ambayo limesababisha. Heshimu maoni yao, lakini ushikamane na maamuzi mazuri ambayo umefanya. Waonyeshe ufikirio wale ambao hawajapata chanjo, wenye umri mkubwa, na walio na magonjwa sugu.

  •   Jizoeze kuwa na subira

     Andiko: “Upendo ni wenye subira na fadhili.”—1 Wakorintho 13:4.

     Hilo linamaanisha nini kwako? Waonyeshe fadhili wengine wanapokuwa na wasiwasi wa kurudia utendaji ambao ulikuwa wa kawaida kabla ya janga hili. Unapopanga utendaji wako mwenyewe, uwe na subira kadiri vizuizi vinavyozidi kupunguzwa.

Jinsi Biblia inavyowasaidia watu kukabiliana na janga hili

 Mashahidi wa Yehova wanafarijiwa na ahadi za Biblia kwamba kutakuwa na wakati ujao mzuri, na hilo linawasaidia wasikazie fikira janga hili tu. Pia, wanategemezana kwa kutii amri ya Biblia ya kukutana pamoja kwa ajili ya ibada. (Waebrania 10:24, 25) Kila mtu anakaribishwa kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova inayofanywa kupitia mtandao wakati wa janga hili.

 Watu wengi wamesema kwamba kukutana pamoja na Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya ibada kumewasaidia sana wakati huu mgumu. Kwa mfano, mwanamke aliyeambukizwa COVID-19 alikubali mwaliko wa kujiunga na Mashahidi wa Yehova katika mikutano kupitia mtandao. Mikutano hiyo ilimsaidia kihisia licha ya kwamba alikuwa na matatizo ya afya yaliyosababishwa na kirusi hicho. Baadaye alisema hivi: “Ninahisi mimi ni sehemu ya familia hii pia. Kusoma Biblia kunanisaidia kuwa na amani ya akili na utulivu wa ndani. Kunanisaidia kukazia fikira tumaini langu la wakati ujao badala ya matatizo yangu. Asanteni kwa kunisaidia kumkaribia Mungu, jambo ambalo nimejaribu kufanya maisha yangu yote.”

a Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Mizio na Magonjwa ya Kuambukiza ya Marekani.

b Yehova ni jina la Mungu kama linavyopatikana katika Biblia.—Zaburi 83:18.