Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ahmad Gharabli/AFP via Getty Images

ENDELEA KUKESHA!

Je, Mataifa Yanaweza Kuepuka Msiba Mkubwa wa Hali ya Hewa?​—Biblia Inasema Nini?

Je, Mataifa Yanaweza Kuepuka Msiba Mkubwa wa Hali ya Hewa?​—Biblia Inasema Nini?

 Kongamano la Umoja wa Mataifa la Mabadiliko ya Tabianchi COP27 lilifikia tamati Jumapili, Novemba 20, 2022. Ingawa makubaliano muhimu yalifikiwa ambayo yatasaidia kiuchumi nchi zinazokabili hatari ya kukumbwa na majanga yanayotokana na hali ya hewa, watu wengi wanatambua kwamba huo si utatuzi wa kiini cha tatizo.

  •   Novemba 19, 2022, António Guterres, katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa alisema hivi: “Ninaunga mkono uamuzi wa kuanzisha mfuko wa madhara na uharibifu. Hata hivyo, ni wazi kwamba hilo halitoshi . . . Bado sayari yetu iko katika hali mahututi.”

  •   “Ulimwengu bado unakabili msiba mkubwa wa hali ya hewa.”​—Mary Robinson, aliyekuwa rais wa Ireland na pia Kamishna Mkuu wa Haki za Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa, Novemba 20, 2022.

 Vijana hasa wanahangaishwa na wakati ujao wa sayari yetu. Hata hivyo, je, mataifa yanaweza kushirikiana ili kutimiza ahadi yao ya kushughulikia tatizo la mabadiliko ya tabianchi? Biblia inasema nini?

Je, mataifa yataungana na kufanikiwa?

 Biblia inaonyesha wazi kwamba licha ya kazi ngumu na jitihada za unyoofu za wote wanaohusika, maendeleo yoyote ambayo mataifa yanafanya ili kusuluhisha tatizo la hali ya hewa yatakuwa machache sana. Ona sababu mbili za kusema hivyo:

  •   “Kilichopinda hakiwezi kunyooshwa.”​—Mhubiri 1:15.

     Maana: Serikali zina upungufu kwa sababu wanadamu hawakukusudiwa kujitawala. (Yeremia 10:23) Hata ikiwa mataifa yangeweza kuungana na hata ikiwa yangetia jitihada nyingi sana, bado hayawezi kutatua matatizo ya ulimwengu.

  •   “Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasiotaka makubaliano yoyote.”​—2 Timotheo 3:2, 3.

     Maana: Biblia ilitabiri kwa usahihi kwamba watu wengi katika siku zetu wangekuwa wenye ubinafsi na hawangetaka kushirikiana na wengine ili kuboresha maisha ya wote.

Sababu ya kuwa na tumaini

 Hata hivyo, wakati ujao wa sayari yetu hautegemei ahadi za serikali za wanadamu. Mungu amemweka Mtawala anayefaa wa ulimwengu huu, Yesu Kristo. Biblia inasema hivi kumhusu:

  •   “Serikali [itakaa] juu ya bega lake. Jina lake litakuwa Mshauri wa Ajabu, Mungu Mwenye Nguvu, Baba wa Milele, Mkuu wa Amani.”​—Isaya 9:6, maelezo ya chini.

 Yesu ndiye Mfalme wa Ufalme wa Mungu, au serikali ya mbinguni. (Mathayo 6:10) Ana nguvu, hekima, na hamu ya kuitunza sayari yetu na wanadamu. (Zaburi 72:12, 16) Chini ya uongozi wake, serikali hiyo ya mbinguni itawakomesha wale “wanaoiangamiza dunia” nayo itarekebisha mazingira ya sayari yetu.​—Ufunuo 11:18, maelezo ya chini; Isaya 35:1, 7.

 Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu suluhisho la kudumu la mabadiliko ya tabianchi, soma makala “Biblia Inasema Nini Kuhusu Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Wakati Wetu Ujao?