Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sean Gladwell/Moment via Getty Images

ENDELEA KUKESHA!

Ulimwengu Watumia Zaidi ya Dola Trilioni 2 kwa Ajili ya Matumizi ya Kijeshi—Biblia Inasema Nini?

Ulimwengu Watumia Zaidi ya Dola Trilioni 2 kwa Ajili ya Matumizi ya Kijeshi—Biblia Inasema Nini?

 Ulimwenguni pote matumizi ya kijeshi yalifikia kilele kipya cha dola za Marekani trilioni 2.24 katika mwaka wa 2022, hasa kwa sababu nchi ya Urusi ilivamia Ukrainia. Ripoti iliyotolewa mwezi wa Aprili 2023 na taasisi ya Stockholm International Peace Research Institute (SIPRI), inasema hivi kuhusu mwaka wa 2022:

  •   Matumizi ya kijeshi ya Ulaya “yaliongezeka kwa asilimia 13 katika mwaka huo, hilo ndilo ongezeko kubwa zaidi kufanyika ndani ya mwaka mmoja tangu vita baridi vilipokwisha.”

  •   “Urusi…iliongeza matumizi yake kwa asilimia 9.2 na ikatoka nafasi ya tano na kuchukua nafasi ya tatu kati ya mataifa yanayotumia pesa nyingi zaidi kwa ajili ya matumizi ya kijeshi.”

  •   Marekani imebaki kuwa nchi inayotumia pesa nyingi zaidi kwa ajili ya matumizi ya kijeshi, “kwa sababu pesa walizotumia ni asilimia 39 ya pesa zilizotumiwa ulimwenguni pote kwa ajili ya matumizi ya kijeshi.”

 Dakt. Nan Tian, ambaye alishiriki kuandika ripoti ya SIPRI alisema: “Matumizi ya kijeshi yamekuwa yakiongezeka katika miaka ya karibuni na hiyo ni ishara ya kwamba tunaishi katika ulimwengu ambao usalama wake unazidi kuzorota.”

 Biblia ilitabiri kwamba katika siku zetu serikali zenye nguvu zingekuwa na mizozo, pia inafunua njia pekee ya kupata amani ya kweli.

Kuongezeka kwa Mizozo ya Kijeshi Kulitabiriwa

  •   Biblia inakiita kipindi tunachoishi ‘wakati wa mwisho.’Danieli 8:19.

  •   Katika kitabu cha Danieli ilitabiriwa kwamba wakati wa mwisho serikali zenye nguvu ulimwenguni zingekuwa zikishindana. Serikali hizo ‘zingesukumana” au kwa maneno mengine zingegombania mamlaka. Mapambano hayo yangehusisha kutumia “hazina” au rasilimali nyingi za kifedha.​—Danieli 11:40, 42, 43.

 Ili tujifunze mengi kuhusu unabii huu wa Biblia wenye kusisimua, tazama video Unabii Uliotimizwa—Danieli Sura 11.

Jinsi amani ya kweli itakavyopatikana

  •   Biblia inasema kwamba Mungu ataondoa serikali za wanadamu. Mungu “atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa kamwe. Na ufalme huo hautakabidhiwa watu wengine wowote. Utazipondaponda na kuzikomesha falme hizi zote, nao pekee utasimama milele.”​—Danieli 2:44.

  •   Yehova a Mungu atafanya jambo ambalo wanadamu hawana uwezo wa kufanya, yaani, kuleta amani ya kweli itakayodumu milele. Jinsi gani? Ufalme wake ambao ni serikali iliyo mbinguni utaondoa silaha zote na kukomesha vita na ukatili.​—Zaburi 46:8, 9.

 Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu mambo ambayo Ufalme wa Mungu utatimiza, soma makala “Wakati Huo ‘Amani Itakuwa Nyingi.’

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu.​—Zaburi 83:18.