Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

fcafotodigital/E+ via Getty Images

Mtindo wa Kuepuka Chochote Kinachotokana na Wanyama—Biblia Inasema Nini?

Mtindo wa Kuepuka Chochote Kinachotokana na Wanyama—Biblia Inasema Nini?

 Watu wengi ulimwenguni wameanza kuvutiwa na mtindo wa maisha wa kuepuka bidhaa zozote zinazotokana na wanyama.

  •   “Mtindo huu wa maisha unahusisha njia ya kufikiri na kuishi. Watu wanaofuata mtindo huo wanajitahidi kadiri wawezavyo kuepuka kuwatendea wanyama kikatili au hata kuwatumia kwa ajili ya chakula, mavazi, au sababu nyingine yoyote.”​—The Vegan Society.

 Watu wengine wanafuata mtindo huo si kwa sababu tu wanawajali wanyama bali pia, ili kulinda mazingira, kulinda afya yao, au kwa sababu za kidini.

  •   Mtindo huu wa kutokula nyama na kuepuka chochote kinachotokana na wanyama ni wa pekee kwa sababu watu wengi wanauona kama imani fulani au uamuzi fulani ambao unaonyesha mtu anachukua kwa uzito jukumu lake la kuifanya sayari yetu iwe bora zaidi.”​—Britannica Academic.

 Je, mtindo huu utasuluhisha matatizo ya sayari yetu? Biblia inasema nini?

Mungu ana maoni gani kuwahusu wanadamu na wanyama?

 Biblia inaonyesha kwamba Muumba wetu, Yehova Mungu a aliwapa wanadamu mamlaka ya kuwatawala wanyama na anawaona wanadamu kuwa bora kuliko wanyama. (Mwanzo 1:27, 28) Mungu aliwaruhusu wanadamu kula wanyama ingawa mwanzoni haikuwa hivyo. (Mwanzo 9:3) Hata hivyo, hapendi wanyama watendewe kwa ukatili.​—Methali 12:10.

 Biblia haikatazi kula au kutokula nyama, huo ni uamuzi wa mtu binafsi. b Uamuzi wetu katika suala hilo hauathiri uhusiano wetu na Mungu kwa njia yoyote ile. (1 Wakorintho 8:8) Mtu yeyote hapaswi kuhukumu mwingine kwa sababu ya uamuzi anaofanya kuhusu chakula.​—Waroma 14:3.

Suluhisho ni nini?

 Biblia inaonyesha kwamba mtindo wa maisha tunaochagua hautasuluhisha matatizo yaliyopo ulimwenguni. Matatizo mengi yanatokana na mifumo inayozorota ya kisiasa, kiuchumi, na pia ya kijamii ambayo hakuna mwanadamu anayeweza kurekebisha. Biblia inasema:

  •   “Kilichopinda hakiwezi kunyooshwa.”​—Mhubiri 1:15.

 Muumba wetu ndiye atakayesuluhisha matatizo tuliyo nayo leo. Biblia inatumia lugha ya mfano kufafanua kile ambacho Mungu atafanya.

  •   “Nami nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali, na bahari haipo tena.”​—Ufunuo 21:1.

 Mungu ataondoa serikali za wanadamu, au “mbingu ya kwanza,” na mahali pake ataweka “mbingu mpya,” yaani, serikali au Ufalme wake ulio mbinguni. Ufalme wake utaondoa “dunia ya kwanza,” yaani, waovu na utatawala juu ya “dunia mpya,” au wale ambao wanajitiisha kwa hiari chini ya utawala wa Mungu.

 Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu wanadamu watajifunza jinsi ya kuishi kwa amani na wanyama na jinsi ya kutunza mazingira kwa njia bora kabisa.​—Isaya 11:6-9.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu.​—Zaburi 83:18.

b Biblia inatuamuru “[tuendelee] kujiepusha . . . na damu.” (Matendo 15:28, 29) Hili linamaanisha hatupaswi kunywa damu au kula nyama ya mnyama ambaye amenyongwa; isitoshe hatupaswi kula chakula ambacho kimewekwa damu.