Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

sinceLF/E+ via Getty Images

ENDELEA KUKESHA!

Ni Nani Atakayewaokoa Raia?​—Biblia Inasema Nini?

Ni Nani Atakayewaokoa Raia?​—Biblia Inasema Nini?

 Shirika la Umoja wa Mataifa linaripoti hivi:

  •   Kuanzia Oktoba 7 hadi Oktoba 23, 2023, vita kati ya Gaza na Israel vimesababisha vifo vya watu 6,400 na watu 15,200 wamejeruhiwa, na wengi wao ni raia. Kwa kuongezea, mamia ya maelfu ya watu wamelazimika kuhama makao yao.

  •   Kufikia Septemba 24, 2023, vita kati ya Urusi na Ukrainia vimesababisha vifo vya raia 9,701 nchini Ukrainia, na raia 17,748 wamejeruhiwa nchini humo.

 Biblia inatoa tumaini gani kwa wale walioathiriwa na vita?

Sababu ya kuwa na tumaini

 Biblia inatabiri kwamba Mungu ‘atakomesha vita katika dunia yote.’ (Zaburi 46:9) Serikali yake ya mbinguni, au ufalme, itatawala badala ya serikali za wanadamu. (Danieli 2:44) Ufalme wa Mungu utawaletea wanadamu kitulizo.

 Ona kile ambacho Yesu Kristo, Mfalme wa Ufalme wa Mungu, atafanya:

  •   “Atamwokoa maskini anayelilia msaada, pia mtu wa hali ya chini na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamhurumia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataokoa uhai wa maskini. Atawaokoa kutoka katika ukandamizaji na ukatili.”​—Zaburi 72:12-14.

 Kupitia kwa Ufalme wake, Mungu ataondoa kabisa matatizo na kuteseka ambako kunaletwa na vita na jeuri.

  •   “Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”​—Ufunuo 21:4.

 Hivi karibuni Ufalme wa Mungu utarekebisha mambo duniani. Biblia ilitabiri “kuhusu vita na habari za vita” ambazo tunaona zikiendelea leo. (Mathayo 24:6) Matukio hayo na mengine yanaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za utawala wa wanadamu.​—2 Timotheo 3:1.