Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inasema Nini Kuhusu Upungufu wa Chakula Uliopo Duniani Leo?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Upungufu wa Chakula Uliopo Duniani Leo?

 “Kutokomeza tatizo la njaa!” Hilo ndilo lengo la viongozi ulimwenguni. Wanatamani kusuluhisha mojawapo ya matatizo makubwa zaidi ya wanadamu, yaani, ukosefu wa chakula na kuhakikisha kwamba kila mtu anapata chakula cha kutosha. a Lakini kweli jambo hilo linawezekana? Biblia inasema nini?

Biblia ilitabiri kungekuwa na upungufu wa chakula

 Biblia ilitabiri kwamba kungekuwa na upungufu wa chakula katika siku zetu, kipindi ambacho inakiita “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Hilo halimaanishi kwamba Mungu ndiye anayesababisha upungufu wa chakula lakini alikuwa anatoa onyo tu kwa kutueleza jinsi hali zitakavyokuwa. (Yakobo 1:13) Fikiria unabii huu unaotajwa katika Biblia.

 “Kutakuwa na upungufu wa chakula . . . sehemu mbalimbali.” (Mathayo 24:7) Unabii huo unaonyesha kwamba kungekuwa na njaa katika sehemu nyingi. Ripoti ya hivi karibuni ya mashirika yanayofuatilia upatikanaji na usambazaji wa chakula inasema hivi: “Licha ya jitihada ambazo zimefanywa kukomesha njaa na kuandaa chakula cha kutosha na chenye lishe bado hali imezidi kuwa mbaya ulimwenguni.” b Mamia ya mamilioni ya watu katika nchi nyingi hawapati chakula cha kutosha. Inasikitisha kwamba wengi hupoteza maisha yao kwa sababu ya tatizo hilo.

 “Tazama! farasi mweusi, na yule aliyeketi juu yake alikuwa na mizani mkononi mwake.” (Ufunuo 6:5) Farasi huyo wa mfano na yule aliyeketi juu yake wanawakilisha njaa katika siku za mwisho. c Yule aliyeketi juu ya farasi huyu amebeba mizani mkononi mwake ili kuwapimia watu chakula kidogo kinachopatikana. Punde si punde, sauti inasikika ikitangaza kwamba bei za chakula zitapanda sana na watu wanaambiwa wahifadhi chakula. Picha hiyo inaonyesha waziwazi jinsi hali ilivyo ulimwenguni leo. Mabilioni ya watu wanashindwa kupata chakula au hawana fedha za kununua chakula chenye lishe.

Tatizo la upungufu wa chakula litakomeshwaje?

 Wataalamu wanasema kwamba dunia yetu inatokeza chakula kingi sana na kinatosha kumlisha kila mtu duniani. Basi ni nini kinachosababisha upungufu wa chakula? Mungu wetu, Yehova, d atasuluhishaje tatizo hilo? Biblia inasema nini?

 Tatizo: Serikali hazina uwezo wa kuondoa umaskini na ukosefu wa haki, mambo ambayo yanachangia tatizo la ukosefu wa chakula.

 Suluhisho: Mungu ataondoa serikali za wanadamu kwa kuwa zimeshindwa kutatua matatizo ya wanadamu na badala yake ataweka serikali yake, yaani, Ufalme wa Mungu. (Danieli 2:44; Mathayo 6:10) Leo, watu wengi ni maskini na wanakosa pesa za kununua chakula, lakini chini ya Ufalme wa Mungu hakutakuwa na tatizo hilo. Biblia inasema hivi kumhusu Yesu Kristo, Mfalme wa Ufalme wa Mungu: “Atamwokoa maskini anayelilia msaada, pia mtu wa hali ya chini na yeyote ambaye hana msaidizi. . . . Kutakuwa na nafaka nyingi duniani; itafurika juu ya milima.”​—Zaburi 72:12, 16.

 Tatizo: Vita husabisha uharibifu na matatizo ya kiuchumi, matokeo ni kwamba watu wanashindwa kupata chakula wanachohitaji.

 Suluhisho: “[Yehova] anakomesha vita katika dunia yote. Anauvunja upinde na kuuvunja mkuki vipandevipande; anayateketeza magari ya vita motoni.” (Zaburi 46:9) Mungu ataharibu zana za vita na pia watu wanaochochea vita. Kwa hiyo, itakuwa rahisi kwa kila mtu kupata chakula. Biblia inatoa ahadi hii: “Mwadilifu atasitawi, na amani itakuwa nyingi.”​—Zaburi 72:7.

 Tatizo: Hali mbaya ya hewa na majanga ya asili yanayoharibu mimea na kuua mifugo.

 Suluhisho: Mungu atadhibiti mifumo ya asili na hivyo hakutakuwa na chochote kinachozuia chakula kukua. Biblia inasema: “[Yehova] huituliza dhoruba ya upepo; mawimbi ya bahari hunyamaza. . . . Yeye hulibadili jangwa kuwa madimbwi ya maji yenye matete, na nchi kavu kuwa chemchemi za maji. Huwafanya wenye njaa wakae humo . . . Wanapanda mbegu mashambani na kupanda mashamba ya mizabibu yanayozaa mazao mengi.”​—Zaburi 107:29, 35-37.

 Tatizo: Watu wenye pupa na ufisadi hutokeza chakula ambacho si salama au hata kuzuia chakula kuwafikia wale wanaokihitaji.

 Suluhisho: Ufalme wa Mungu utawaangamiza watu wote ambao si wanyoofu na ambao wana ufisadi. (Zaburi 37:10, 11; Isaya 61:8) Biblia inasema kwamba Yehova Mungu “[ndiye] anayetekeleza haki kwa ajili ya waliopunjwa, yeye [ndiye] anayewapa chakula wenye njaa.”​—Zaburi 146:7.

 Tatizo: Kila mwaka, theluthi moja ya chakula kinachotokezwa duniani kinatupwa tu.

 Suluhisho: Chini ya Ufalme wa Mungu, masuala ya chakula yatashughulikiwa vizuri. Yesu alipokuwa duniani, alikuwa makini sana ili asiharibu chakula. Kwa mfano, katika pindi moja aliwalisha zaidi ya watu 5,000 kimuujiza. Watu walipomaliza kula, aliwaagiza wanafunzi wake: “Kusanyeni vipande vilivyobaki, ili chochote kisipotee.”​—Yohana 6:5-13.

 Kwa kuwa Ufalme wa Mungu utaondoa mambo yanayosababisha njaa, wanadamu wote watakuwa na chakula kingi chenye lishe. (Isaya 25:6) Ili kujua ahadi hiyo itatimizwa lini, soma makala yenye kichwa “Ufalme wa Mungu Utaanza Kutawala Dunia Lini?

a Ajenda ya 2030 ya Maendeleo Endelevu iliyokubaliwa na Nchi Wanachama wa Umoja wa Mataifa mwaka wa 2015.

b Ripoti iliyokusanywa na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo, Shirika la Kuwahudumia Watoto la Umoja wa Mataifa, Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani, na Shirika la Afya Duniani.

c Ili kujifunza zaidi kuhusu wapanda farasi wanaotajwa kwenye kitabu cha Ufunuo, soma makala yenye kichwa “Wapanda Farasi Wanne—Jinsi Wanavyokuhusu

d Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?