Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

ENDELEA KUKESHA!

Vita Nchini Ukrainia Vimezidisha Upungufu wa Chakula Ulimwenguni

Vita Nchini Ukrainia Vimezidisha Upungufu wa Chakula Ulimwenguni

 Mei 19, 2022, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipokea ripoti kutoka kwa maofisa 75 wenye cheo cha juu, iliyoonyesha kwamba “tatizo la upungufu wa chakula ulimwenguni ambalo lilisababishwa na janga la COVID-19 na mabadiliko ya hali ya hewa, limeongezeka sana kwa sababu ya vita vinavyoendelea nchini Ukrainia, hivi kwamba baadhi ya maeneo yanakabili njaa.” Punde baada ya hapo, gazeti la The Economist lilitangaza kwamba “kwa sababu ya vita vinavyoendelea katika ulimwengu ambao tayari una matatizo mengi sana, watu wengi zaidi watakabili njaa.” Biblia ilitabiri kwamba katika siku zetu kungekuwa na upungufu wa chakula. Hata hivyo, inatupatia msaada wa kukabiliana na tatizo hilo.

Biblia ilitabiri kungekuwa na upungufu wa chakula

  •    Yesu alitabiri kwamba: “Taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme, kutakuwa na upungufu wa chakula.”​—Mathayo 24:7.

  •    Kitabu cha Ufunuo kinataja wapanda farasi wanne wa mfano. Mmoja wa wapanda farasi hao anawakilisha vita. Anafuatwa na mpanda farasi mwingine ambaye anawakilisha njaa, yaani, kipindi ambacho ingekuwa vigumu kupata chakula na kingeuzwa kwa bei ya juu sana. “Nami nikaona, na tazama! farasi mweusi, na yule aliyeketi juu yake alikuwa na mizani mkononi mwake. Nami nikasikia kitu kama sauti . . . ikisema: ‘Kibaba cha ngano kwa . . . mshahara wa siku moja na vibaba vitatu vya shayiri kwa . . . mshahara wa siku moja; na usidhuru divai na mafuta ya zeituni.’”​—Ufunuo 6:5, 6, maelezo ya chini.

 Unabii huo wa Biblia kuhusu upungufu wa chakula unatimia sasa katika kipindi ambacho Biblia inakiita “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu “siku za mwisho” na wapanda farasi wanne wa kitabu cha Ufunuo, tazama video Ulimwengu Umebadilika Tangu 1914 na usome makala “Wapanda Farasi Wanne—Jinsi Wanavyokuhusu.”

Jinsi Biblia inavyoweza kutusaidia

  •    Biblia ina ushauri mzuri unaoweza kukusaidia kukabiliana na changamoto maishani, kutia ndani kupanda kwa bei za chakula na pia upungufu wa chakula. Ona baadhi ya kanuni hizo katika makala “Jinsi ya Kuishi Ukiwa na Pesa Kidogo.”

  •    Biblia pia inatupa tumaini kwamba hali zitakuwa bora zaidi. Inaahidi kwamba “kutakuwa na nafaka nyingi duniani” na wakati huo kila mtu atakuwa na chakula kingi. (Zaburi 72:16) Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu ahadi ya Biblia ya wakati ujao na kwa nini unaweza kuiamini, soma makala “Tumaini Bora la Wakati Ujao.”