Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

ENDELEA KUKESHA!

Viwango vya Juu Zaidi vya Joto Ulimwengu Pote—Biblia Inasema Nini?

Viwango vya Juu Zaidi vya Joto Ulimwengu Pote—Biblia Inasema Nini?

 Julai 2022, viwango vya juu zaidi vya joto kuliko wakati mwingine katika historia viliripotiwa ulimwenguni pote:

  •   “Kwa mara ya pili mwezi huu, China imetangaza kiwango cha juu zaidi cha joto katika majiji 70 hivi.”​—Julai 25, 2022, CNN Wire Service.

  •   “Mioto ya msituni yaenea katika maeneo mengi ya Ulaya baada ya kiwango cha joto kupanda sana.”​—Julai 17, 2022, The Guardian.

  •   “Majiji katika maeneo yote ya Marekani yamerekodi kiwango cha juu zaidi cha joto Jumapili baada ya joto la kiangazi kuenea katika Pwani ya Mashariki na maeneo fulani ya Kusini na Magharibi ya Kati.”​—Julai 24, 2022, The New York Times.

 Mambo yote hayo yanamaanisha nini? Je, hatimaye uhai hautaweza kustahimili kuishi duniani? Biblia inasema nini?

Je, viwango vya juu sana vya joto vilitabiriwa katika Biblia?

 Ndiyo. Viwango vya juu sana vya joto ulimwenguni vinapatana na matukio ambayo Biblia ilitabiri yangetukia katika siku zetu. Kwa mfano, Yesu alitabiri kwamba tungeona “mambo yenye kuogopesha” au “mambo ya kutisha.” (Luka 21:11; Union Version) Kupanda kwa joto ulimwenguni kumewafanya watu wengi kuogopa kwamba wanadamu wataiharibu dunia kabisa.

Je, hatimaye uhai hautaweza kuwepo duniani?

 Hapana. Mungu aliiumba dunia iwe makao ya kudumu ya wanadamu. (Zaburi 115:16; Mhubiri 1:4) Badala ya kuwaruhusu wanadamu kuiharibu dunia, ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia,’ kama alivyoahidi.​—Ufunuo 11:18.

 Fikiria maandiko mawili tu yanayotoa unabii kuhusu kile ambacho Mungu ameahidi:

  •   “Nyika na nchi iliyokauka zitafurahi, na jangwa tambarare litashangilia na kuchanua maua kama zafarani.” (Isaya 35:1) Mungu hatairuhusu dunia kuwa jangwa ambalo haliwezi kukaliwa, bali atarekebisha sehemu ambazo zimeharibiwa.

  •   “Unaitunza dunia, unaifanya izae kwa wingi na kuitajirisha sana.” (Zaburi 65:9) Kwa baraka za Mungu, dunia itakuwa paradiso.

 Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu jinsi mabadiliko ya hali ya hewa yanavyotimiza unabii wa Biblia, soma makala yenye kichwa “Biblia Inasema Nini Kuhusu Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Wakati Wetu Ujao?

 Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu ahadi ya Biblia kwamba mazingira yatarekebishwa, ona makala yenye kichwa “Ni Nani Atakayeiokoa Dunia?