Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kituo cha redio cha WBBR, mwaka wa 1924

HIFADHI YA VITU VYETU VYA KALE

Kupeperusha Habari Njema

Kupeperusha Habari Njema

 Jumapili jioni, Februari 24, 1924, kituo kipya cha redio cha Wanafunzi wa Biblia, a WBBR, kilipeperusha kipindi chake cha kwanza. Kipindi hicho cha kwanza kilikuwaje? Ni nani waliosikiliza? Na Mashahidi wa Yehova wameendelea kutumiaje teknolojia za karibuni zaidi kutangaza “habari njema ya Ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa”?​—Mathayo 24:14.

Mtaalamu wa mitambo kwenye kituo cha WBBR

“Kipindi Kikaanza”

 Kipindi cha uzinduzi kilipeperushwa kuanzia saa 2:30 usiku na kipindi hicho kiliendelea kwa saa mbili. Programu hiyo ilipeperushwa kutoka kwenye studio mpya iliyokuwa imejengwa huko Staten Island, New York. Ndugu Ralph Leffler, aliyekuwa msimamizi mkuu wa mfumo wa sauti alisema kwamba kila mtu ndani ya studio “alikuwa amesisimka na alikuwa na wasiwasi.” Alijiuliza, “Je, kweli kuna mtu atakayetusikiliza? Niliwasha mitambo, kipindi kikaanza, nasi tukatumaini tu kwamba mambo yatakuwa shwari.”

 Mtangazaji wa kipindi hicho cha kihistoria alikuwa Ndugu Victor Schmidt, aliyekuwa msimamizi kituo hicho cha redio. Alianza kwa kuwatambulisha wanamuziki kadhaa stadi sana, ambao wote walikuwa Wanafunzi wa Biblia. Kwanza ndugu mmoja alicheza muziki mtamu kwenye piano. Kisha, Cora Wellman akaimba wimbo wenye kichwa “The Ninety and Nine” (Wale Tisini na Tisa), uliotegemea mfano wa Yesu wa kondoo aliyepotea. (Luka 15:4-7) Wengine walifuata baada yake kutia ndani Frederick W. Franz, ambaye aliimba “The Penitent,” wimbo uliozungumzia simulizi la yule mwana mpotevu.​—Luka 15:11-25.

Siku ya kipindi cha kwanza cha WBBR

 Joseph F. Rutherford, ndugu aliyekuwa akiongoza kazi ya Wanafunzi wa Biblia kipindi hicho, alitoa hotuba ya kuweka wakfu kituo hicho “ili kiendeleze masilahi ya ufalme wa Masihi.” Alisema hivi: “Kwa kuwa Bwana ameruhusu wanadamu wabuni redio, tuna uhakika ni mapenzi yake kwamba tuitumie kuwafundisha watu kuhusu utimizo wa unabii Wake mbalimbali.”

“Hatujakosa Silabi Hata Moja”

 Wasikilizaji wengi wa Marekani kaskazini-mashariki walisikiliza kipindi hicho cha kwanza. Msikilizaji mmoja aliyekuwa Morrisville, Vermont, umbali wa zaidi ya kilomita 320 kutoka kwenye kituo hicho, alisema hivi: “Ninafurahi kuripoti kwamba tunawasikia vizuri tu sasa hivi. . . . Sauti ya Rutherford ilisikika vizuri kabisa. . . . Hatujakosa silabi hata moja.” Kipindi hicho kilisikilizwa na mwanamume fulani aliyekuwa Monticello, Florida! Kituo chetu kipya cha redio kilifanikiwa sana, na barua nyingi za shukrani zilianza kumiminika.

Joseph Rutherford akizungumza kwenye kikuza-sauti ndani ya kituo cha WBBR. Victor Schmidt alikuwa mtangazaji

 Kituo hicho kiliendelea kutangaza ujumbe wa Ufalme kwa miaka 33, b kipeperusha hasa habari zake kwa watu waliokuwa kaskazini-mashariki mwa Marekani. Hata hivyo, pindi fulani WBBR iliunganishwa na vituo vingine vya redio na kufikia mamilioni ya watu nchini Marekani, Kanada, na sehemu za mbali zaidi. Inapendeza kwamba Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1975 kilikuwa na ripoti hii: “Kufikia 1933, mwaka wenye kilele, stesheni 408 zilikuwa zikitumiwa kupeleka ujumbe kwenye mabara sita, na hotuba 23,783 zilizotegemea Biblia zilipeperushwa . . . Zamani hizo, mtu alipotafuta stesheni kwenye redio angeweza kusikiliza vipindi vilivyotayarishwa na Watch Tower kwa kutegemea vituo vilivyokuwa katika sehemu mbalimbali. Huwa mawimbi hayo ya redio yalijaa maneno ya kweli yaliyomtukuza Mungu.”

Huduma ya Nyumba kwa Nyumba Yachukua Nafasi ya Redio

 Wanafunzi wa Biblia walipoanza kutumia WBBR, inakadiriwa kwamba kulikuwa na wastani wa wahubiri 1,064 nchini Marekani. Redio hiyo ilisaidia sana kikundi hicho kidogo kuwafikia watu. Kufikia 1957, kulikuwa na wastani wa wahubiri 187,762 wa Ufalme nchini Marekani na 653,273 duniani pote. Kwa kuongezea, akina ndugu na dada hao wenye bidii walizoezwa kwenye mikutano ya kutaniko, nao wakawa na matokeo zaidi katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba na pia katika aina nyingine za huduma.

 Ndugu wanaoongoza walipoona maendeleo hayo katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba waliamua kufikiria upya manufaa ya kuwa na kituo cha redio wakati huo. Walifikia mkataa gani? Uamuzi ulifanywa wa kuuza WBBR, kituo pekee ambacho bado kilikuwa kikimilikiwa na kutumiwa na Watchtower Society. Kiliuzwa Aprili 15, 1957. Siku moja kabla, kipindi cha pekee cha kuaga kilipeperushwa, na Nathan H. Knorr aliulizwa kwa nini kituo hicho kilikuwa kikiuzwa. Alisema kwamba ongezeko la Mashahidi wa Yehova lililokuwepo wakati huo lilitokana hasa na kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Alisema hivi: “Kuna wengi waliochochewa na vipindi vya WBBR. Lakini ongezeko lililopo katika maeneo ambayo redio hii inafika si tofauti na ongezeko katika maeneo mengine ulimwenguni.” Hivyo, akina ndugu waliona kwamba kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba inatimiza mengi zaidi kuliko kutangaza habari njema kupitia redio. Hata hivyo, hiyo haikuwa mara ya mwisho ya Mashahidi wa Yehova kupeperusha vipindi vyao. Miaka mingi baadaye walianza kufanya hivyo tena, lakini katika njia tofauti.

Utangazaji Leo

 Oktoba 6, 2014, jambo lenye kusisimua sana lilitokea katika tengenezo la Yehova. Kituo kipya kilianzishwa kinachopeperushwa vipindi kwenye Intaneti kinachoitwa JW Broadcasting. Mashahidi wa Yehova na watu wengine wanaweza kutazama na kusikiliza vipindi hivyo vinavyopeperushwa kila mwezi kwenye kivinjari cha Intaneti, programu ya JW Library, king’amuzi, au kupitia satelaiti. c Hata hivyo, katika sehemu fulani za ulimwengu, watu wa Yehova bado wanatumia redio au televisheni katika kazi ya kuhubiri. Jinsi gani?

Kipindi cha kwanza cha JW Broadcasting, Oktoba 2014

 Katika miaka ya hivi karibuni, tengenezo la Yehova limetumia vituo vya redio na televisheni kupeperusha mikutano ya kutaniko ya kila juma na pia makusanyiko ya eneo katika sehemu ambazo hazina Intaneti nzuri. Vipindi hivyo vinavyopeperushwa na stesheni za kibinafsi, vimewafikia watu wengi ambao si Mashahidi kutia ndani watu wanaopendezwa. Kwa mfano, katika mwaka wa 2021 na 2022, meneja wa vituo vya redio waliiambia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova iliyo Afrika Mashariki kwamba watu wengi ambao si Mashahidi walifurahia sana mikutano yetu. Hata baadhi ya wasikilizaji hao walio Kenya, Sudan Kusini, na Tanzania waliomba wafundishwe Biblia kibinafsi.

 Hata hivyo, njia ya msingi ambayo Mashahidi wa Yehova hutumia kutangaza ujumbe wa Ufalme ulimwenguni pote ni kupitia kazi ya nyumba kwa nyumba, vigari vya machapisho, na kupitia tovuti ya jw.org. Tovuti yetu huwapa watu wanaopendezwa fursa ya kupata Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha zaidi ya 1,080—bila malipo yoyote. Pia, wanaweza kupata majibu ya maswali ya Biblia na wanaweza kutafuta mahali ambapo mikutano ya Kikristo inafanyiwa. Jitihada na mbinu hizo za Mashahidi wa Yehova zimefanya iwe rahisi zaidi kwa watu kujifunza habari njema ya Ufalme wa Mungu kuliko wakati mwingine wowote! Kwa kweli, habari njema inatangazwa “katika dunia yote inayokaliwa” kama tu Biblia ilivyotabiri.​—Mathayo 24:14.

a Wanafunzi wa Biblia walibadili jina lao na kuitwa Mashahidi wa Yehova mwaka 1931.

b Kwa muda fulani, Mashahidi wa Yehova walikuwa na vituo vya redio katika nchi nyingine kutia ndani Australia na Kanada.