Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HIFADHI YETU YA VITU VYA KALE

Kuwa na Umoja Katika Nchi Iliyogawanyika

Kuwa na Umoja Katika Nchi Iliyogawanyika

 Kuanzia mwaka wa 1948 hadi miaka ya 1990, mfumo wa kisiasa nchini Afrika Kusini ulikuwa na ubaguzi wa rangi. a Katika kipindi hicho, wengi waliwatendea watu wa rangi tofauti isivyo haki. Wakati huo wa ubaguzi, Kallie alihesabiwa kwenye kundi la “machotara” (wazazi wake wametoka jamii mbili tofauti), naye anasema hivi: “Watu ambao hawakuwa weupe walikuwa wakibaguana wenyewe kwa wenyewe pia.”

 Nchini Afrika Kusini Mashahidi wa Yehova wanatoka katika jamii na malezi mbalimbali. Walikabilianaje na ubaguzi? Tunajifunza nini kutokana na historia yao?

Kukabiliana na Hatari Zinazotokana na Migawanyiko

 Baadhi ya watu waliopinga ubaguzi wa rangi walikuwa wakifanya maandamano nchini. Wengi kati ya wale waliopinga sera za serikali walifungwa, na baadhi yao waliuawa. Hivyo, wale waliopinga serikali wakawa na jeuri hata zaidi. Kwa upande mwingine, Mashahidi wa Yehova walitii sheria zilizowekwa na hawakujihusisha na maandamano au kujaribu kupindua serikali. Kwa njia hiyo, waliwaiga Wakristo wa karne ya kwanza ambao waliendelea “[kujitiisha] kwa mamlaka zilizo kubwa.”​—Waroma 13:1, 2.

 Mara nyingi, Mashahidi wa Yehova walishinikizwa wavunje msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote. Lakini, ikiwa wangeunga mkono upande fulani, hilo lingewafanya wajihusishe na migogoro ya kisiasa iliyokuwa ikiendelea au hata wangejipata wakipigana na ndugu zao wa kiroho. Kwa mfano, Thembsie anaeleza hivi: “Mwaka 1976, wanafunzi wengi wa sekondari walilazimishwa kushiriki katika ghasia za kisiasa. Wanafunzi waliojihusisha katika ghasia hizo walienda kila mlango wakiwatafuta wanafunzi wengine ili wajiunge nao. Ikiwa mtu angekataa kujiunga nao, basi huenda wangechoma nyumba yake moto au hata wangempiga kufikia hatua ya kumwua.” Kiongozi mmoja wa chama cha upinzani alimwambia hivi Shahidi anayeitwa Theophilus, “Tukishamshinda mzungu, tutakuua kwa sababu hukupigana kwa ajili ya nchi yako.”

Kukutanika Pamoja Katika Nchi Iliyogawanyika

 Licha ya magumu yaliyosababishwa na ubaguzi, Mashahidi wa Yehova nchini Afrika Kusini waliendelea kukutana pamoja kwa ajili ya ibada. (Waebrania 10:24, 25) Baadhi ya makutaniko hayakuweza kujenga Majumba ya Ufalme kwa sababu watu wengi hawakuwa na uwezo wa kujikimu chini ya mfumo wa ubaguzi wa rangi. b Enver anasema hivi: “Kwa miaka mingi, tulilazimika kukodi majengo ambayo yalikuwa katika hali mbaya sana. Hivyo, baba yangu aliruhusu mikutano ya kutaniko ifanywe nyumbani kwetu. Nyumba yetu ilitumika kama Jumba la Ufalme mara mbili kwa juma. Pindi nyingine, nyumba yetu ilijaa watu hata zaidi ya watu 100. Baada ya mikutano, tulifurahia kuwaonyesha ukarimu wote waliohudhuria.”

Mashahidi weupe na weusi wakiwa wamekutanika pamoja, Aprili 1950

Mkutano wa watu wa rangi tofauti, katika Uwanja wa Rand, Johannesburg, mwaka 1980

 Akina ndugu walitafuta njia za kushinda ubaguzi kwa werevu. Kwa mfano, katika Mkoa wa Limpopo, ndugu mweupe ambaye aliombwa atoe hotuba kwenye kusanyiko la mzunguko lililofanywa katika eneo la watu weusi hakuruhusiwa kuingia humo. Basi, alimwendea mtu mweupe aliyemiliki shamba lililopakana na eneo la watu weusi na kufanya makubaliano. Hivyo, kusanyiko lilifanywa huku msemaji akiwa ndani ya ua la shamba hilo na wahudhuriaji wakiwa upande wa pili.

Kutoa Ushahidi Katika Maeneo Yaliyotengwa

 Wakati wa ubaguzi, watu wa jamii mbalimbali watenganishwa kulingana na rangi zao. Hata maeneo ya makutaniko yalipangwa kulingana na jamii ya watu walioishi katika eneo hilo. Kwa sababu ya ubaguzi Mashahidi walihitaji kubadilikana na hali walipopanga wahubiri kwa ajili ya utumishi wa shambani. Kwa mfano, haikuwa rahisi kuhubiri katika eneo ambalo halijagawiwa kutaniko. “Kwa kawaida hakukuwa na maeneo ambayo watu ambao si weupe waliruhusiwa kulala. Krish, ambaye wakati wa ubaguzi alihesabiwa kwenye kundi la “Wahindi” anasema: “Hivyo, tulilala ndani ya magari yetu au chini ya miti. Kisha asubuhi, tulienda kwenye kituo cha mafuta na kuoga chooni. Nyakati nyingine hata vyoo hivyo vilikuwa vimeandikwa ‘Weupe Pekee.’ Ingawa hivyo, wahubiri waliunga mkono utumishi na walifurahia sana kuwahubiria watu wengi waliopendezwa katika maeneo ya vijijini.”

Kikundi cha Mashahidi wa rangi tofauti wakihubiri katika eneo la vijijini, mwaka 1981

 Licha ya magumu hayo, idadi ya watu wa Yehova iliendelea kuongezeka. Sera ya ubaguzi wa rangi ilipoanzishwa mwaka wa 1948, kulikuwa na wahubiri 4,831 Afrika Kusini. Lakini sera hiyo ilipokomeshwa mwaka wa 1994, idadi ya wahubiri ilikuwa imefikia watu 58,729. Idadi hiyo ya wahubiri imeendelea kuongezeka. Mwaka wa 2021, Afrika Kusini ilifikia kilele kipya cha wahubiri 100,112.

Ingawa Walizungukwa na Chuki, Waliunganishwa na Upendo

 Wakati wa ubaguzi, Mashahidi wa Yehova nchini Afrika Kusini walikuwa wakiishi katika nchi ambayo ilikuwa na sifa ya kuwalazimisha watu wawabague wengine. Katika hali hiyo, Mashahidi walifanya yote wanayoweza kusitawisha upendo na umoja kati ya watu wa rangi zote. Walifanya hivyo kwa kufundisha na kufuata kanuni za Biblia. (Matendo 10:34, 35) Ingawa walizungukwa na chuki, waliunganishwa na upendo.​—Yohana 13:34, 35.

 Mwaka wa 1993, Mashahidi wa Yehova walifanya kusanyiko nchini Afrika Kusini lililokuwa na watu kutoka jamii mbalimbali. Kiongozi maarufu wa kisiasa aliwatazama Mashahidi wa Afrika Kusini wakiwasalimu kwa uchangamfu na kuwakaribisha wajumbe wa kimataifa walipowasili katika uwanja wa ndege. Kisha akasema hivi: “Kama tungekuwa na roho kama yenu, tungesuluhisha matatizo yetu kitambo.”

Milton Henschel, kutoka Makao Makuu ya Mashahidi wa Yehova, akizungumza katika kusanyiko kubwa la Mashahidi wa rangi tofauti, mwaka 1955

Ndugu mweupe na ndugu mweusi wakifanya kazi pamoja katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Afrika Kusini, mwaka 1986

Kikundi cha Mashahidi wa rangi tofauti wakipakua chakula katika kusanyiko, mwaka 1985

Kikundi cha Mashahidi wa rangi tofauti wakipakua chakula katika kusanyiko, mwaka 1985

Umati mkubwa wa Mashahidi wa rangi tofauti wakiwa wamekusanyika pamoja katika uwanja wa FNB, Johannesburg, mwaka 2011

a Mfumo wa sera ya ubaguzi wa rangi uliwalazimisha watu wa rangi tofauti kutengana. Rangi ya mtu iliamua elimu ambayo mtu angeweza kupata, kazi ya kimwili ambayo angeweza kufanya, mahali ambapo angeweza kuishi, na mtu ambaye angeweza kufunga ndoa naye. Ili kupata habari zaidi, ona makala “Sera ya Ubaguzi wa Rangi” kwenye 2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova.

b Tangu mwaka wa 1999, michango inayotolewa na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote imewawezesha kujenga na kukarabati Majumba ya Ufalme mahali palipo na uhitaji.