Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

KUTOKA KATIKA HIFADHI YA VITU VYETU VYA KALE

Shirika la Kitamaduni Lililofundisha Kweli za Biblia

Shirika la Kitamaduni Lililofundisha Kweli za Biblia

 Mwaka wa 1917, International Bible Students, ambao baadaye walikuja kuitwa Mashahidi wa Yehova, walifanya mipango yao ya kwanza ya kuwahubiria watu wa Mexico. Mamia ya watu wanyoofu walijiunga na ibada ya kweli katika miaka iliyofuata. Hata hivyo, katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, serikali ya Mexico haikufurahia sehemu tulizohubiri na majengo ambayo tulifanyia mikutano yetu.

 Wakati huo, sheria ya Mexico ilisema kwamba utendaji wowote wa hadharani unaohusu ibada unapaswa kufanywa katika majengo yaliyomilikiwa na serikali. Hilo lilikuwa tatizo kubwa kwa sababu makusanyiko yetu yalifanywa katika maeneo ya umma na mikutano yetu ya kila juma mara nyingi ilifanywa katika nyumba binafsi za Mashahidi wa Yehova. Isitoshe, tuliwahubiria watu barabarani na nyumba-kwa-nyumba.

 Ili kutii sheria ya nchi, mwaka wa 1943, tulisajiliwa kama shirika la kitamaduni lisilo la kibiashara linalowaelimisha watu ili kuboresha maisha yao katika jamii. Hilo lilimaanisha kwamba tulikuwa na haki za shirika la kitamaduni na si la kidini. Baada ya kufanya hivyo, hatukulazimika kukutana na kuhubiri katika majengo yaliyomilikiwa na serikali.

 Utendaji wetu ulitia ndani programu za kitamaduni na zilizowaelimisha watu. Hivyo, tulitimiza matakwa ya kisheria yaliyowekwa na serikali kwa ajili ya mashirika ya kijamii na kitamaduni. (Waroma 13:1) Bila shaka, kusudi letu la kufundisha watu kweli za Biblia halikubadilika. (Isaya 48:17, 18) Punde si punde, tulianza kuona jinsi Yehova alivyokuwa akibariki mpango huo. Mashahidi wengi leo wanakumbuka vizuri jinsi mpango huo ulivyowasaidia wengi kupata kweli.

Kubadilikana na Hali Katika Huduma

 Siku zote, kazi yetu muhimu zaidi nchini Mexico imekuwa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Hata hivyo, kama mtume Paulo alivyofanya, tulibadilikana na hali katika huduma. (1 Wakorintho 9:20-23) Kwa mfano, Paulo alipozungumza na wanaume wa Athene akiwa Areopago hakutaja Maandiko moja kwa moja. (Matendo 17:22-31) Vivyo hivyo, tulipoenda kuhubiri hatukubeba Biblia na hatukurejelea Biblia tulipoanzisha mazungumzo na watu.

Mashahidi wakishiriki katika kazi ya kuhubiri hadharani bila Biblia, 1945

 Isabel anasema: “Tulijitambulisha kama wawakilishi wa sosaiti ya kitamaduni inayoelimisha watu. Mara nyingi, nilitumia makala za Amkeni! ambazo hazikutaja Maandiko moja kwa moja.” Ingekuwaje ikiwa mwenye-nyumba alitaka kujifunza mengi zaidi kumhusu Mungu? Basi tuliwaeleza kweli za Biblia. Aurora anasema: “Kwa kuwa hatukubeba Biblia, tulilazimika kukariri maandiko mengi.” Wenye-nyumba walifurahi pia tulipotumia Biblia zao.

Kutetea Kazi Yetu ya Kuhubiri Nyumba-kwa-Nyumba

 Tulikuwa tumejiandaa kumweleza yeyote ambaye angekuwa na maswali, kwamba kazi yetu ilikuwa imetambuliwa kisheria. (Wafilipi 1:7) Vitambulisho kutoka kwa serikali vilitusaidia. a María anasema:“Siku zote tulibeba kadi ya utambulisho iliyotiwa sahihi na Waziri wa Mambo ya Nje.” Samuel anasema: “Wenye mamlaka walipotusimamisha na kutuuliza tunachofanya, tuliwaonyesha kadi zetu.”

 Kadi hizo za utambulisho zilitusaidia kukabiliana na upinzani. Kwa mfano, Jesús, ambaye alitumikia katika Jimbo la Jalisco anasema: “Mwaka wa 1974, kikundi cha watu kikiongozwa na kasisi walinipeleka mimi pamoja na wenzi wa ndoa ambao ni Mashahidi kwa wenye mamlaka ili tuzuiwe kuhubiri. Tuliwaonyesha kadi zetu za utambulisho na kila mtu akawa mtulivu. Baada ya kupata msaada wa kisheria, tuliendelea kuwasaidia wale waliopendezwa katika eneo hilo. Leo, kuna makutaniko kadhaa katika jiji hilo.”

Kujifunza Biblia na Kuwafundisha Watu Kusoma na Kuandika

 Kwa kuwa tulikuwa shirika la kijamii lililoelimisha, tulitoa mafunzo kwa umma ya kusoma na kuandika.  b Ariel anasema: “Mpango huo ulikuja wakati unaofaa kabisa. Miaka hiyo, watu wengi hawakuwa wameenda shule lakini walitamani sana kusoma Biblia. Tuliwafundisha jinsi ya kusoma na kuandika kisha wengi wao walianza kujifunza Biblia pamoja na sisi.”

 Ruth alisema: “Mara tu walipoanza kujifunza kusoma, walifanya maendeleo upesi katika funzo lao Biblia. Kuwa na uwezo wa kusoma kuliwapa uradhi na furaha. Sote tulijionea jinsi walivyofanya maendeleo ya kiroho baada ya hapo.”

 Mashahidi wa Yehova walikuwa wamesajiliwa kama shirika la kijamii na kitamaduni kuanzia mwaka wa 1943 hadi 1993. Katika kipindi hicho, tulisaidia zaidi ya watu 127,000 kujifunza kusoma na kuandika na wengine 37,000 kuboresha uwezo wao wa kufanya hivyo. Maofisa wa serikali walitupongeza kwa mchango wetu katika kazi ya kuwasaidia watu kujifunza kusoma na kuandika. (Waroma 13:3) Kwa mfano, katika mwaka wa 2010, walitupatia tuzo kwa sababu ya “kazi ngumu tuliyofanya kwa miongo mingi ya kuwaelimisha maelfu ya watu katika jimbo la Mexico na nchini kote ili kuboresha maisha yao.”

Kukutanika Pamoja

 Kwa sababu tulikuwa tumesajiliwa kama shirika la kijamii na kitamaduni, sehemu zetu za mikutano zilipangwa kama madarasa na ziliitwa Majumba ya Masomo ya Kitamaduni. Tulifanyia mikutano yetu hapo na pia tulitumia sehemu hizo kuwafundisha watu kusoma na kuandika.

 Angel anasema: “Majumba hayo mara nyingi yalikuwa nyumba za ndugu na dada na wengi wao hawakuwa na uwezo mkubwa wa kifedha. Niliwaheshimu sana. Walikuwa tayari kuishi katika sehemu ndogo tu ya nyumba yao ili sehemu nyingine itumike kwa ajili ya mikutano.”

 Dhabihu za aina hiyo zilisaidia sana. Angel anasema hivi kuhusu mikutano ya kutaniko: “Nyakati fulani, watu wengi sana walihudhuria hivi kwamba wengi wetu tulilazimika kusimama nje. Tulichungulia dirishani ili kutoa maelezo. Lakini tulifurahia sana mikutano.”

 Ili kuepuka matatizo, hatukuimba au kusali kwa sauti. Edmundo anasema: “Wasemaji walipotoa Hotuba ya Kitamaduni, ambayo sasa inaitwa hotuba ya watu wote, walizungumzia mashauri ya Biblia yanayohusu maisha ya kila siku ili kuwasaidia wahudhuriaji kuboresha utamaduni wao na kuwa na maisha mazuri zaidi.” Baada ya muda, hata tuliacha kutaja majina ya vitabu vya Biblia. Tulitumia njia gani kurejelea Maandiko? Manuel anatoa mfano huu: “Badala ya kusema Ufunuo sura ya 21, mstari wa 3 na wa 4, tulisema kitu kama, ‘Kitabu cha 66, 21, 3 na 4.’” Shahidi mwingine anayeitwa Moises anasema: “Hilo lilimaanisha kwamba tulipaswa kujifunza mpangilio wa vitabu vya Biblia kwa namba ili tufaulu kupata maandiko.”

Mambo Tunayojifunza Kutokana na Historia Yetu Nchini Mexico

 Kwa ujumla, tengenezo letu liliongoza kazi nchini Mexico kama tu lilivyoongoza kazi katika sehemu nyingine ulimwenguni. Ingawa ibada yetu iliwekewa vizuizi mbalimbali, ilikuwa wazi kwamba Yehova alikuwa akiwabariki watu wake. Tuliposajiliwa kama shirika la kitamaduni mwaka wa 1943 kulikuwa na wahubiri 1,565 nchini Mexico. Tulisajiliwa kisheria kama dini mwaka wa 1993. Katika mwaka huo, wastani ya idadi ya wahubiri iliongezeka na kufika 366,177. Kazi ambayo wahubiri hao walifanya imetokeza ukuzi mkubwa hata zaidi. Kufikia mwaka wa 2021, wahubiri nchini humo walikuwa wameongezeka na kwa wastani kulikuwa na wahubiri 864,633. Tunaweza kujifunza masomo gani kutokana na historia ya nchi ya Mexico?

 Kubadilikana na hali matatizo yanapotokea. Kufanya hivyo nchini Mexico, kulisaidia kazi yetu kutambuliwa kisheria kwa miaka 50. Mario anasema: “Pindi fulani, nilijiuliza kwa nini hatungeweza kufuata utaratibu wa kitheokrasi uliofuatwa katika nchi nyingine. Hata hivyo, sikuwahi kusikia mtu yeyote akitilia shaka mwongozo uliotolewa na tengenezo. Sote tuliamini kwamba Yehova alikuwa akiwaongoza watu wake. Kwa hiyo, tulikuwa watiifu kabisa.”

 Kaza fikira kwenye kazi ya Yehova. Guadalupe anasema: “Tulikuwa na bidii katika kazi ya kufanya wanafunzi hivi kwamba hatukuwa na wasiwasi kuhusu jambo lingine lolote. Tulipata furaha nyingi kwa kumtumikia Yehova. Kumtumikia Yehova ndilo jambo tuliloona kuwa muhimu zaidi.”

 Kaa karibu na Wakristo wengine. Anita anasema: “Mambo ambayo hatukuweza kufanya katika Majumba ya Masomo ya Kitamaduni kama vile kuimba nyimbo za Ufalme, tuliyafanya nyumbani. Tulikuwa na umoja na hata tulitumia wakati pamoja mara kwa mara. Tulipokuwa na tafrija tulitanguliza mambo ya kiroho sikuzote.”

 Florentino anasema hivi kuhusu kipindi hicho: “Ninapotazama nyuma, ninatambua kwamba mambo yote yaliyotokea yalitimiza kusudi fulani na yalitufundisha jambo fulani muhimu. Ninaona waziwazi kwamba licha ya mambo yote kutia ndani kazi yetu kupingwa, Yehova alikuwa akiongoza mambo.”

a Kadi hiyo ilitumiwa kwa ajili ya kujitambulisha tu. Maandiko hayasemi kwamba Mkristo anahitaji kibali cha kisheria ili kuzungumza na majirani wake kuhusu kweli za Biblia. Sasa, Mashahidi wa Yehova hawatafuti tena vibali au usajili wa kibinafsi.

b Kulingana na takwimu rasmi, karibu nusu ya idadi ya watu walioishi Mexico katika miaka ya 1940 na 1950 hawakujua kusoma na kuandika.

Mashahidi huko Chihuahua, Mexico, wakiwa mbele ya sehemu waliyofanyia mikutano ya Kikristo. Kuna bango lenye maandishi ya Kihispania linalosema: “Jumba la Masomo ya Kitamaduni,” 1952

Kikundi cha Mashahidi katika ofisi ya tawi iliyo Mexico City, kuna bango lenye maandishi ya Kihispania linalosema: “Mnara wa Mlinzi, Shirika la Kijamii,” 1947

Mashahidi wawili wakitoa nakala ya Kihispania ya gazeti la Mnara wa Mlinzi katika maeneo ya mbali ya Hidalgo, Mexico, 1959

Mashahidi walipata kadi ya utambulisho kutoka kwa serikali na waliitumia katika huduma ilipohitajika

Mwaka wa 2010, Katibu wa Elimu ya Umma nchini Mexico aliwapa tuzo Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya jitihada walizofanya katika kufundisha watu kusoma na kuandika

Mashahidi walikuwa wamesajiliwa kama shirika la kitamaduni na hilo liliwawezesha kufanya mikutano mikubwa kama Kusanyiko hili la Kimataifa la Kitamaduni la mwaka wa 1969