Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

KUTOKA KATIKA HIFADHI YA VITU VYETU VYA KALE

Walishikamana na Yehova Katika Nyakati Ngumu

Walishikamana na Yehova Katika Nyakati Ngumu

 Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, kila kitu kilivurugika katika sehemu nyingi barani Ulaya. Jambo zuri ni kwamba Mashahidi wa Yehova na watu wengine walikuwa wameachiliwa kutoka katika kambi za mateso za Wanazi. Hata hivyo, bado maisha yalikuwa magumu. Kama tu watu wengine, watu wa Yehova hawakuwa na mahitaji kama vile chakula, mavazi, makao, na vitu vingine vya lazima. Dada Karin Hartung anasema, “Kwa sababu kulikuwa na uhaba wa nyumba ilibidi watu waishi na watu wao wa ukoo au wakodishe vyumba vilivyo katika nyumba zao.” Dada Gertrud Poetzinger, mmoja kati ya watu waliokuwa katika kambi za mateso kwa miaka saba na nusu, baadaye aliishi katika stoo ndogo kwa muda fulani na alilala kwenye kiti. a

 Tengenezo la Yehova lilifanya nini ili kuwaandalia mahitaji ya kimwili ndugu walioishi katika maeneo yaliyokumbwa na vita? Na ni masomo gani tunayoweza kujifunza kutokana na wale walioishi katika nyakati ngumu baada tu ya vita kwisha?

Kushughulikia Mahitaji ya Kimwili ya Akina Ndugu

 Tengenezo la Yehova lilitenda kwa uharaka ili kuwaandalia watu wa Mungu msaada barani Ulaya. Nathan Knorr na Milton Henschel kutoka makao makuu waliwatembelea Mashahidi ili kukagua mahitaji yao. Walitembelea nchi za Uingereza, Uswisi, Ufaransa, Ubelgiji, Uholanzi, Denmark, Sweden, Finland, na Norway katika miezi ya Novemba na Desemba 1945. Ndugu Knorr alitoa ripoti hii, “Kwa mara ya kwanza, tulijionea uharibifu mkubwa uliosababishwa na vita katika bara la Ulaya.”

Nathan Knorr akizungumza na Mashahidi katika mji wa Helsinki, Finland, Desemba 21, 1945

 Wakati huo Ndugu Knorr hakuruhusiwa kuingia Ujerumani. Hata hivyo, Ndugu Erich Frost, ambaye alikuwa anasimamia ofisi ya tawi nchini Ujerumani alienda kukutana naye. b Ndugu Erich alitoa ripoti hii, “Ndugu Knorr alitupa ushauri hususa na kutuahidi kwamba tutapata chakula na nguo. Kisha baada ya muda mfupi, shehena kubwa ya unga, mafuta, shayiri, na vyakula vingine ilitumwa Ujerumani kwa meli. Kulikuwa na unga, mafuta, shayiri, na vyakula vingine. Pia, ndugu kutoka nchi nyingine walitutumia maboksi makubwa yaliyokuwa na nguo kama vile suti na viatu.” Akina ndugu na dada walipokea vitu hivyo huku wakitokwa na machozi ya shukrani. Ripoti moja ilisema, “Hawakuishia hapo, waliendelea kutuma misaada kwa muda wa miaka miwili na nusu!” c

Mashahidi nchini Marekani wakichambua nguo zilizotolewa kama mchango kabla ya kuzipeleka Ulaya

Waliendelea Kukazia Fikira Mambo ya Kiroho

 Hali ya maisha ilipoanza kuboreka, akina ndugu waliendelea kukazia fikira utumishi wao kwa Yehova. Ni nini kilichowasaidia?

Jürgen Rundel (aliye kushoto mbele) akiwa na ndugu waliotoka kutaniko la Spittal an der Drau, Austria mwaka 1954

 Walidumisha ratiba nzuri ya kiroho. (Waefeso 5:15, 16) Vita vilifanya iwe vigumu kupata machapisho ya Biblia na jambo hilo lilivuruga ratiba yao ya kiroho. Hata hivyo, baada ya vita walianza kufanya mikutano kwa ukawaida na pia kushiriki katika huduma. Jürgen Rundel anayeishi Austria anasema: “Tulitiwa moyo kuwa na ratiba nzuri ya kiroho na makala katika chapisho Informant d na pia waangalizi wetu wa mzunguko walitutia moyo kudumisha ratiba yetu ya kiroho. Tulimtanguliza Yehova, Yesu, funzo letu la Biblia la kibinafsi, na huduma. Vitu kama televisheni havikuwepo ili kutukengeusha fikira.”

 Dada Ulrike Krolop anasema: “Ninakumbuka shangwe niliyopata nilipofanya utafiti wa kina na kutafakari kuhusu habari fulani inayopatikana katika Biblia. Mume wangu aliniwekea mfano mzuri. Kila tulipopokea nakala mpya ya gazeti la Mnara wa Mlinzi, aliacha kile alichokuwa akifanya na kulisoma. Karin aliyetajwa hapo juu, anasema: “Tuliona jinsi vitu vya kimwili vinavyoweza kupotea haraka wakati wa vita. Lakini ingawa kulikuwa na upungufu wa machapisho yanayotegemea Biblia tuliweza kupata tulichohitaji ili kuimarisha imani yetu. Na Yehova aliwathawabisha watumishi wake washikamanifu.”

Ulrike Krolop

 Walianza tena kushiriki katika huduma. (Mathayo 28:19, 20) Watu wa Yehova hawakuwa na uhuru wa kushiriki katika kazi ya kuhubiri na kufundisha wakati wa vita. Ndugu anayeitwa Friedhelm anakumbuka kwamba baada ya vita “kila mtu alijiingiza mara moja katika kazi ya kuhubiri na kufundisha.” Ulrike anasema hivi: “Shahidi wa kwanza kuhubiria familia ya mume wangu alikuwa bado amevaa mavazi aliyotoka nayo kwenye kambi ya mateso! Ni wazi kwamba alianza kuhubiri mara tu alipotoka huko.” Jürgen anasema, “Karibu kila mtu alikuwa na bidii sana baada ya vita. Ndugu na dada wengi vijana waliingia katika utumishi wa wakati wote.”

 Ulrike anasema: “Hali ya maisha katika majiji yaliyopigwa mabomu ilikuwa mbaya sana.” Watu wengi waliishi ndani ya magofu! Mashahidi wa Yehova waliwafikiaje watu? Ulrike anasema: “Tulifuata mwanga wa taa au moshi uliotoka kwenye bomba la moshi.” Familia ya Ulrike ilipata kweli baada ya vita.

 Walitiana moyo. (1 Wathesalonike 5:11) Mashahidi wengi wa Yehova walitendewa kwa ukatili katika vita. Lakini baada ya vita hawakukazia fikira magumu waliyokabili bali walitiana moyo. Kwa kweli, walikuwa na shangwe tele kwa sababu ya “sifa iliyojaribiwa” ya imani yao. (Yakobo 1:2, 3) Johannes, ambaye sasa anaishi Marekani, anasema hivi: “Mwangalizi wetu wa mzunguko alitusimulia jinsi alivyoona mkono wa Yehova katika pindi mbalimbali alipokuwa kwenye kambi ya mateso. Ripoti hizo zilituimarisha sana.”

 Vita vilipokwisha, akina ndugu walidumisha uhusiano wao na Yehova. Johannes anasema walifanya hivyo kwa kujikumbusha “jinsi Yehova alivyowasaidia walipokuwa kambini na jinsi alivyojibu sala zao.” Kama tu ilivyotajwa hapo juu, Mashahidi hao waliopata uhuru walikuwa na ratiba nzuri ya kiroho kutia ndani kusoma Biblia kwa ukawaida, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kushiriki katika utumishi wa shambani. Elisabeth, dada ambaye alihudhuria kusanyiko lililofanyika Nuremberg mwaka 1946 anasema “bado walionekana wembamba na dhaifu lakini ‘waliwaka roho’ walipotusimulia mambo waliyopitia.”​—Waroma 12:11.

Karin Hartung

 Walishikamana na Wakristo wenzao. (Waroma 1:11, 12) Mashahidi hawakuwa na uhuru wa kushirikiana na wenzao wakati wa vita kwa sababu ya mateso hayo ya kikatili. Karin anasema, “Mashahidi walitembeleana mara mojamoja ili wasigunduliwe na wenye mamlaka na hivyo kuwahatarisha ndugu na dada zao.” Bila shaka, hali hiyo ilikoma vita vitlipokwisha. Friedhelm anasema: “Akina ndugu walifanya mambo yote pamoja. Sikuzote walitanguliza mikutano na huduma maishani mwao.”

 Dietrich, mzee anayeishi Ujerumani anasema, “Mashahidi wachache sana walikuwa na magari” baada ya vita. Anaendelea kusema, “Hivyo, tulitembea hadi sehemu tuliyokutanika lakini tulitembea katika makundi. Hilo lilitusaidia kuwa karibu zaidi. Tulihisi tukiwa kama familia moja.”

Mambo Tunayojifunza

 Leo, watumishi wengi wa Yehova wanavumilia hali ngumu kwa sababu ya majanga ya asili, magonjwa, vita, mateso, na matatizo ya kiuchumi. (2 Timotheo 3:1) Hata hivyo, hatupaswi kuwa na wasiwasi kupita kiasi. Kwa nini? Mifano ya ndugu na dada zetu waaminifu walioishi katika kipindi cha Wanazi nchini Ujerumani inatuhakikishia kwamba Mungu wetu ataendelea kututegemeza katika kipindi hiki kigumu cha siku za mwisho. Basi tuwe na mtazamo kama wa Paulo aliyeandika: “Tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. kMwanadamu atanifanya nini?’”​—Waebrania 13:6.

a Soma simulizi la maisha la Dada Poetzinger’s kwa Kiingereza, “Putting the Kingdom First in Postwar Germany.”

b Soma simulizi la maisha la Ndugu Frost kwa Kiingereza, “Deliverance From Totalitarian Inquisition Through Faith in God.”

c Ili kujua mengi zaidi kuhusu jitihada za kutoa msaada baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu ona makala yenye kichwa “Walitoa Kilicho Bora,” na pia masanduku kwenye ukurasa wa 211, 218, na 219 katika kitabu Ufalme wa Mungu Unatawala!

d Makutaniko sasa yanatumia Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo.