Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HIFADHI YETU YA VITU VYA KALE

Idadi ya Watu Wanaojua Kusoma na Kuandika Yaongezeka Duniani

Idadi ya Watu Wanaojua Kusoma na Kuandika Yaongezeka Duniani

 Agostinho anayeishi nchini Brazili anasema hivi, “Nililelewa katika eneo la mashambani huko Brazili. Tulikuwa maskini sana, Ilibidi niache shule ili nifanye kazi na kusaidia kuandalia familia yetu mahitaji ya msingi.” Agostinho hakujua kusoma na kuandika hadi alipokuwa na umri wa miaka 33. Anasema hivi, “Kujifunza kusoma na kuandika kulinisaidia niheshimiwe na nijiheshimu zaidi.

 Agostinho ni mmoja kati ya watu zaidi ya 250,000 ambao Mashahidi wa Yehova wamewasaidia kusoma na kuandika kwa kipindi cha miaka 70 iliyopita. Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanawafundisha watu kusoma na kuandika? Watu wamenufaikaje na elimu hiyo?

Kutojua Kusoma na Kuandika Huzuia Watu Wasijifunze Mambo Mengi

 Kufikia katikati ya miaka ya 1930, Mashahidi wa Yehova walikuwa wakifanya huduma yao katika nchi 115. Ili kuwafikia watu wanaozungumza lugha mbalimbali, wamishonari walicheza rekodi za hotuba za Biblia zilizotafsiriwa, na nyakati nyingine waliweza kutoa machapisho katika lugha za kienyeji. Ijapokuwa watu wengi walipendezwa sana na ujumbe wa Biblia, wengi wao walishindwa kujifunza, kwa sababu ya kutojua kusoma na kuandika.

 Ilikuwa vigumu kwa watu wengi kutumia kanuni za Biblia kwa sababu hawakuweza kusoma Biblia wenyewe. (Yoshua 1:8; Zaburi 1:2,  3) Pia ilikuwa vigumu kwao kutimiza wajibu wao wa Kikristo. Kwa mfano, ikiwa wazazi hawakuweza kusoma, wangehitaji kufanya jitihada nyingi zaidi ili kuwafundisha watoto wao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7)Pia Mashahidi wapya ambao hawakuweza kusoma hawakuwa na uwezo mkubwa wa kutumia Biblia walipojaribu kuwafundisha wengine.

Kuanzisha Kampeni ya Kuwafundisha Watu Kusoma na Kuandika

 Katika miaka ya 1940 na 1950, wawili kati ya ndugu walioongoza wa Mashahidi wa Yehova, Nathan H. Knorr na Milton G. Henschel, walisafiri nchi mbalimbali ili kusaidia kupanga kazi ya kuhubiri. Walitia moyo ofisi za tawi katika nchi ambazo watu wengi hawakujua kusoma na kuandika, waanzishe madarasa ya kusoma na kuandika katika makutaniko.

Kifaa cha kujifunzia kusoma chatolewa katika kusanyiko lililofanyika Chingola, Zambia, mwaka 1954

 Ofisi za tawi zilituma miongozo ya jinsi ya kuendesha madarasa hayo katika makutaniko. Katika nchi fulani, tayari serikali za mitaa zilikuwa na programu kama hizo zilizoweza kutumika. Kwa mfano, nchini Brazili, ofisi ya tawi ilipokea vifaa na vitabu kutoka serikalini na kuvituma katika makutaniko mbalimbali. Katika nchi nyingine, Mashahidi walihitaji kuunda programu zao wenyewe.

 Watu wote wangeweza kuhudhuria madarasa hayo, wanaume, wanawake, vijana au wazee. Lengo lilikuwa kuwafundisha wanafunzi kusoma katika lugha yao ya mama—hata ikiwa hilo lilihusisha kufundisha lugha kadhaa katika kutaniko moja.

Programu Inayowasaidia Watu

 Watu wamenufaikaje na mpango huu wa kufundisha watu kusoma na kuandika? Shahidi mmoja kutoka nchini Mexico anasema hivi: “Sasa ninaweza kuelewa maana ya Biblia, na hilo limefanya ujumbe wake uniguse moyo sana. Kujua kusoma kumenisaidia kuzungumza kwa uhuru na majirani zangu, na nimeweza kufikia mioyo ya watu wengi na ujumbe wa Biblia.

 Faida za programu hizi za kujifunza ni nyingi zaidi ya kuwasaidia watu kuielewa Biblia. Isaac kutoka Burundi anasema hivi: “Kujifunza kusoma na kuandika kumenisaidia kujifunza stadi za ujenzi. Sasa ninafanya kazi ya ujenzi na ninasimamia miradi mikubwa ya ujenzi.”

Kichichewa kikifundishwa ndani ya Jumba la Ufalme huko Lilongwe, Malawi, mwaka 2014

 Jesusa kutoka Peru alikuwa na umri wa miaka 49 alipoanza kuhudhuria madarasa ya kujifunza kusoma na kuandika. Anasema hivi, “Nikiwa mama anayeshughulikia mahitaji ya familia, ninahitaji kujua bei na majina ya vyakula mbalimbali sokoni. Zamani kufanya hivyo hakukuwa rahisi. Lakini sasa, kwa sababu ya darasa la kujifunza kusoma na kuandika, ninajiamini zaidi ninapofanya ununuzi kwa ajili ya familia yangu.”

 Kwa miaka kadhaa, wenye mamlaka katika nchi mbalimbali wamewasifu Mashahidi wa Yehova kwa kazi waliyofanya ya kuongeza kiwango cha watu wanaojua kusoma na kuandika. Leo, bado Mashahidi wa Yehova wanaendesha madarasa ya kujifunza kusoma na kuandika, wakitumia programu na vifaa vilivyoboreshwa zaidi. Pia, wamebuni na kuchapisha nakala karibu milioni 224 za broshua katika lugha 720 ili kuwasaidia watu kujifunza kusoma na kuwasaidia wale wenye uwezo mdogo wa kusoma. a

a Kwa mfano, broshua Jitahidi Kusoma na Kuandika inapatikana katika lugha 123, na broshua Msikilize Mungu inapatikana katika lugha 610.