Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HIFADHI YETU YA VITU VYA KALE

Mashahidi wa Yehova Nchini New Zealand​—Wakristo Wenye Amani na Waliojitoa?

Mashahidi wa Yehova Nchini New Zealand​—Wakristo Wenye Amani na Waliojitoa?

 Oktoba 21, 1940, New Zealand iliwatangaza Mashahidi wa Yehova kuwa kikundi cha wachochezi na hatari kwa usalama wa umma. Ingawa walikabili hali ngumu baada ya tangazo hilo la serikali, Mashahidi wa Yehova hawakuvunjika moyo. Kwa mfano, waliendelea kukusanyika pamoja ili kuabudu licha ya hatari ya kuvamiwa na kukamatwa na wenye mamlaka.

 Andy Clarke, mume wa Shahidi wa Yehova anayeitwa Mary, aliona azimio la mke wake la kuhudhuria mikutano licha ya vitisho. Alihofu kwamba mke wake angekamatwa ikiwa angeendelea kuhudhuria mikutano. Ijapokuwa hakuwahi kufanya hivyo kabla ya tangazo hilo, Andy alianza kumsindikiza Mary na kumwambia, “Ikiwa watakukamata, itabidi wanikamate mimi pia!” Kuanzia wakati huo, Andy alihudhuria kila mkutano pamoja na mke wake. Baada ya muda, yeye pia alibatizwa na akawa Shahidi. Kama Mary, Mashahidi wengi nchini New Zealand waliazimia kuendelea kuwa washikamanifu licha ya mateso wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu.

Kudumisha Bidii Gerezani

 Siku moja, alipokuwa akihubiri ujumbe wa Biblia nyumba kwa nyumba, John Murray, aliyekuwa na umri wa miaka 78, alikamatwa na polisi. Mahakama ilimpata na kosa la kushiriki katika shughuli za kikundi cha wachochezi. Mashahidi wengi walifikishwa mahakamani; baadhi yao walitozwa faini, na wengine walifungwa gerezani miezi mitatu.

 Mashahidi walikataa utumishi wa kijeshi kwa msingi wa dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia. (Isaya 2:4) Kwa sababu hiyo, wakati wa vita, wengi wao waliteswa walipoitwa ili wajiunge na jeshi. Hivyo, badala ya kuzoezwa kuwa wanajeshi, Mashahidi 80 walifungwa gerezani wakati wa vita. Hata hivyo, ijapokuwa waliteswa na kulikuwa na majira ya baridi kali sana, ndugu hao waliendelea kumwabudu Yehova wakiwa na shangwe.

 Bila kukawia, Mashahidi waliofungwa gerezani walipanga ratiba ya shughuli za kiroho. Walitenda kama kutaniko, kwa kuwa na mikutano ya kawaida na kuwahubiria wafungwa wengine. Mashahidi hata waliruhusiwa kufanya makusanyiko katika kambi wakisimamiwa na mlinzi. Baadhi ya wafungwa walijifunza kweli za Biblia na kubatizwa gerezani.

Mashahidi waliokuwa gerezani waliendelea kufanya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi

 Bruce, mtoto wa mwisho wa Mary na Andy tuliowataja awali, aliona kifungo hicho kuwa fursa ya kuboresha hali yake ya kiroho. Anakumbuka hivi, “Kwangu ilikuwa kama niko shuleni kwa sababu nilizungumza kwa kina na ndugu wenye uzoefu waliofungwa kambini, na nilichota ujuzi wote waliokuwa nao.”

 Mwaka wa 1944, serikali ilitaka kuwaachilia huru baadhi ya wafungwa. Hata hivyo, wenye mamlaka katika jeshi walipinga wazo hilo kwa kuwa waliamini kwamba ikiwa Mashahidi wataachiwa huru, wataendelea kuzungumza na wengine kuhusu imani yao. Ripoti hiyo inasema: “Ingawa kuendelea kuwafunga gerezani kunasaidia kuzuia misimamo yao mikali, haitaweza kamwe kuwabadili.”

Si Hatari kwa Usalama wa Umma

 Kwa kuwa marufuku iliyowekwa ilijulikana sana, baadhi ya watu walitaka kuwafahamu Mashahidi wa Yehova. Muda si muda, watu wengi waligundua kwamba Mashahidi wa Yehova hawakuwa hatari kwa usalama wa umma. Waliona pia kwamba Mashahidi walikuwa Wakristo wenye amani. Kama matokeo, idadi ya Mashahidi New Zealand iliongezeka kutoka 320 mwaka wa 1939 hadi 536 mwaka wa 1945!

 Nyakati fulani, viongozi waliokuwa na mtazamo unaofaa walitambua kwamba kitendo cha kupiga marufuku Mashahidi wa Yehova hakikuwa cha haki. Hakimu mmoja, alifuta mashtaka dhidi ya ndugu aliyekamatwa akihubiri, baada ya kusikiliza ushahidi. Alisema hivi: “Ni jambo lisilopatana na akili na elimu yangu ya sheria kwamba kugawa nakala za Biblia ni kosa la jinai.”

 Mwishowe marufuku ilipoondolewa baada ya vita kwisha, Mashahidi waliazimia hata zaidi kuwasaidia majirani zao wajifunze kuhusu Ufalme wa Mungu. Barua kutoka ofisi ya tawi kwa makutaniko yote nchini New Zealand katika mwaka wa 1945 ilisema hivi: “Kila mtu na atende kwa busara, urafiki, na fadhili kwa watu wote. Epuka ubishi au ugomvi. Kumbuka kwamba watu tunaokutana nao wanaamini na kuishi kulingana na kile wanachojifunza katika dini zao. . . . Wengi wao ni ‘kondoo’ wa Bwana ambao tunapaswa kuwaelekeza kwa Yehova na ufalme wake.”

 Leo, Mashahidi wa Yehova nchini New Zealand wanaendelea kuwahubiria ujumbe wa Biblia wenyeji na watalii. Siku moja, kwa saa kadhaa, kikundi cha Mashahidi 4 katika eneo la Turangi waliwahubiria habari njema wageni 67 kutoka nchi 17!

 Ni wazi kwamba wenyeji wa New Zealand wanawatambua Mashahidi wa Yehova kuwa wenye amani na Wakristo wenye bidii na wanaoheshimu kweli za Biblia. Kila mwaka, mamia ya watu hubatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Kufikia mwaka wa 2019, zaidi ya Mashahidi 14,000 walikuwa wakimtumikia Yehova kwa shangwe katika nchi hiyo ya kusini.

Mkutano wa funzo la Biblia uliofanywa muda fulani baada ya marufuku kuweka mwaka wa 1940

Vyumba vidogo vya gereza vilivyotosha mtu mmoja katika eneo la North Island, New Zealand

Gereza la Hautu lililo katika eneo la North Island, New Zealand

Mwaka wa 1949, kusanyiko la Mashahidi waliofungwa kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote