Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Habari Zenye Kutegemeka na Kuimarisha Imani

Habari Zenye Kutegemeka na Kuimarisha Imani

DESEMBA 1, 2021

 Mashahidi wa Yehova wanawajali sana waamini wenzao. (1 Petro 2:17) Wengi wetu tunahisi kama Dada Tannis nchini Kenya anavyohisi. Anasema hivi, “Ninafurahi kujua kinachowapata ndugu na dada zangu wapendwa ulimwenguni pote.” Tannis na mamilioni ya Mashahidi wengine wanapataje habari? Tangu 2013, tumekuwa tukipata habari hizo kupitia sehemu ya Habari kwenye tovuti yetu ya jw.org.

 Sehemu hiyo ya Habari inatoa ripoti zinazotegemeka kuhusu Mashahidi wa Yehova. Zinazungumzia mambo kama vile kutolewa kwa Biblia, kazi ya kutoa msaada wakati wa misiba, miradi ya ujenzi, na matukio mengine muhimu. Sehemu hiyo ina habari kuhusu ndugu na dada ambao wamefungwa kwa sababu ya imani yao. Sehemu hiyo ya Habari pia ina masimulizi yenye kutia moyo kuhusu kampeni za kuhubiri na mwadhimisho wa Ukumbusho. Ni nani wanaofanya utafiti wa makala hizo za habari, nazo zinatayarishwaje?

Kutambua na Kuripoti Habari Mbalimbali

 Sehemu ya Habari inashughulikiwa na Ofisi ya Habari za Umma (OPI). Idara hiyo iko kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote na inafanya kazi chini ya usimamizi wa Halmashauri ya Waratibu ya Baraza Linaloongoza. Kuna zaidi ya ndugu na dada 100 wanaofanya kazi katika idara ya OPI—wengi wao ni wafanyakazi wanaoishi nje—kutia ndani waandishi, watafiti, wachoraji, na watafsiri. Wengine huwasiliana na maofisa wa serikali, wasomi, na waandishi wa habari. Idara ya OPI inasaidiwa na zaidi ya Madawati 80 ya Habari za Umma (PID) katika ofisi za tawi ulimwenguni pote.

 Ili kutayarisha ripoti ya habari, OPI hufanya kazi kwa ukaribu na PID. Ndugu hao wanapotambua habari inayofaa, wanafanya utafiti na kukusanya habari inayotegemeka. Wanaweza kufanya hivyo kwa kuwahoji watu na kuzungumza na wataalamu. Baada ya kukusanya mambo hakika, makala ya habari inaandikwa, inahaririwa, inakaguliwa chapa, inaunganishwa na picha, na kutumwa kwa Halmashauri ya Waratibu ili iidhinishwe.

Maelezo ya Shukrani

 Mashahidi wenzetu wanahisije kuhusu sehemu hiyo ya Habari? Dada Cheryl, anayeishi nchini Filipino anasema hivi, “Ninapenda kuanza siku yangu kwa kusoma habari kuhusu tengenezo la Yehova na watu wa Yehova.”

 Wasomaji wengi wanasema kuna tofauti kubwa kati ya Habari za jw.org na habari kutoka vyanzo vingine. Tatiana, anayeishi nchini Kazakhstan, anasema hivi: “Ninashukuru kwamba ninaweza kuamini habari zilizo kwenye jw.org. Ni zenye kutegemeka na zinataja mambo hakika.” Dada Alma anayeishi nchini Mexico anasema hivi: “Habari zilizo kwenye vyombo vya habari zinahuzunisha, lakini habari zinazotoka kwenye tovuti yetu zinatia moyo sana.”

 Mbali tu na kutegemeka, habari kutoka kwenye tovuti yetu zinaimarisha imani. Bernard, anayeishi nchini Kenya, anasema hivi: “Sehemu ya Habari imenisaidia kuwaona ndugu na dada zangu ulimwenguni pote kuwa kama familia yangu, haidhuru wanaishi wapi. Ninaweza kutaja majina yao na hali hususa wanazokabili katika sala zangu.” Dada Bybron ambaye pia anaishi nchini Kenya anasema hivi: “Kila wakati ninapoona makala kuhusu kutolewa kwa Biblia katika lugha nyingine mimi husisimka! Makala hizo hunikumbusha kwamba Yehova hana ubaguzi.”

Sehemu ya Habari inatusaidia tutoe sala hususa kuhusu changamoto ambazo ndugu na dada zetu ulimwenguni pote wanakabili

 Habari kuhusu ndugu wanaokabili mateso zinaweza pia kututia moyo. Jackline anayeishi nchini Kenya anasema hivi: “Kutafakari ujasiri wanaoonyesha kunaimarisha imani yangu. Sikuzote mimi hujaribu kuona ni nini kinachowasaidia kuvumilia. Nimejifunza kwamba mambo yanayoonekana kuwa madogo—kama vile kusali, kusoma Biblia, na hata kuimba—yanawasaidia sana ndugu hao kuendelea kuwa imara.”

 Dada Beatriz anayeishi nchini Kosta Rika anathamini sana makala za habari kuhusu misiba ya asili. Anasema hivi: “Sehemu ya Habari hunisaidia kuona jinsi tengenezo letu linavyoandaa mahitaji ya ndugu zetu haraka, kwa utaratibu, na kwa upendo. Hilo hunisadikisha kwamba hili ni tengenezo la Yehova.”

 Tunashukuru sana kupata habari za karibuni kuwahusu ndugu zetu ulimwenguni pote. Hilo halingewezekana bila michango yenu kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote ambayo inatolewa hasa kupitia donate.pr418.com. Asante sana kwa michango yako yenye ukarimu.