Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Kifaa cha Aina Tofauti cha Kujifunzia Biblia

Kifaa cha Aina Tofauti cha Kujifunzia Biblia

APRILI 1, 2022

 Januari 2021, Baraza Linaloongoza lilitangaza kutolewa kwa kifaa kipya cha kujifunzia Biblia, yaani, Furahia Maisha Milele! a Ulihisije uliposikia tangazo hilo? Matthew anayeishi nchini Kanada, anasema hivi: “Nilifurahi sana. Nilisisimuka hata zaidi niliposikiliza hotuba na kutazama video zilizoeleza kwa nini chapisho hilo liliandaliwa na jinsi lilivyofanyiwa majaribio. Nilitamani sana kuliona na kulitumia.”

 Kitabu Furahia Maisha Milele! kilianzisha njia mpya ya kuongoza mafunzo ya Biblia. Hata hivyo, hiyo si tofauti pekee kati ya kitabu hiki kipya na vitabu tulivyotumia zamani. Ukitumia nakala iliyochapishwa ya kitabu Furahia Maisha Milele! utatambua kwamba karatasi zake zina tofauti fulani na za vitabu vingine. Ili kuona jambo hilo, acheni tujifunze mengi zaidi kukihusu.

Kitabu Kipya Kilicho Tofauti

 Karatasi ngumu. Kwa nini hilo lilifaa? Kitabu Furahia Maisha Milele! kina picha maridadi zaidi ya 600, mara kumi zaidi ya kitabu Biblia Inatufundisha Nini! Kitabu hiki kina nafasi zaidi ambazo hazina maneno au michoro yoyote kwenye kurasa. Mambo haya mawili yanatokeza changamoto: Karatasi inapokuwa nyepesi, picha kwenye ukurasa mwingine zinaweza kuonekana kwa urahisi. Ili kuepuka hilo, ndugu kwenye Idara ya Uchapishaji wa Kimataifa (IPD), iliyo Wallkill, New York, Marekani, walijaribu aina nne za karatasi ambazo tunatumia kwa sasa kwenye viwanda vyetu vya uchapishaji. Halmashauri ya Uandikaji ya Baraza Linaloongoza ilikagua kila karatasi na kuchagua iliyo nzito zaidi. Hata ingawa karatasi hii inagharimu asilimia 16 zaidi ya karatasi tunazotumia kwenye machapisho mengine, inawasaidia wanafunzi wa Biblia kusoma kila ukurasa wa kitabu Furahia Maisha Milele! bila kukengeushwa na picha zilizo katika ukurasa mwingine.

Ukurasa kwenye upande wa kulia unaonyesha karatasi iliyotumiwa kuchapa kitabu Furahia Maisha Milele!

 Jalada tofauti. Jalada la kitabu hiki kipya ni tofauti na majalada ya vitabu vyetu vingine kwa sababu limetengenezwa kwa njia isiyoharibika kirahisi. Badala ya jalada la kawaida, kitabu kipya kina jalada linalowezesha picha kuonekana vizuri kwa kuwa haling’ai sana. Jalada hili pia linasaidia kisiharibike haraka kwa sababu ya kutumiwa kwa muda mrefu. Hata hivyo, jalada hili linagharimu mara tano zaidi ya lile tulilozoea kutumia. Hivyo, ofisi kadhaa za tawi zilishirikiana ili kupata jalada lisilogharimu sana.

Kutengeneza majalada

 Kwa nini jalada hili la bei ghali linatumiwa? Ndugu mmoja anayefanya kazi katika IPD anaeleza hivi: “Tunatumaini kwamba kitabu hiki kitatumiwa vizuri, hivyo tungependa kidumishe mwonekano mzuri hata kinapotumiwa kwa muda mrefu.” Eduardo, anayefanya kazi katika Idara ya Uchapishaji wa Kimataifa katika ofisi ya tawi nchini Brazili, anasema: “Tunafurahi kuona jinsi tengenezo la Yehova linavyotumia vifaa vyenye ubora ili kitabu hiki kiwe maridadi, kitumiwe kwa muda mrefu, na kiwe chenye kupendeza, na wakati huohuo tukihakikisha michango inatumika vizuri.”

Uchapishaji Wakati wa Janga la COVID-19

 Machi 2021, tulianza kuchapisha kitabu Furahia Maisha Milele! Tulifanya hivyo katika kipindi cha janga la COVID-19 ambacho kilikuwa na changamoto. Kwa sababu ya vizuizi vilivyowekwa Betheli, hatungeweza kupata msaada kutoka kwa ndugu wanaoishi nyumbani ambao wanajitolea kufanya kazi kwenye viwanda vyetu vya uchapishaji, wala hatungeweza kuwakaribisha Wanabetheli wapya. Hivyo, viwanda vyetu havikuwa na wafanyakazi wa kutosha, na viwanda vingine vilifungwa kwa muda kwa sababu ya maagizo ya serikali.

 Changamoto hizo zilishughulikiwa jinsi gani? Viwanda vyetu vilipokuwa tayari kuanza kazi, ndugu na dada fulani wanaofanya kazi katika idara nyingine za Betheli walipata mgawo wa muda wa kusaidia katika uchapishaji huo. Joel anayefanya kazi katika IPD anasema hivi: “Roho yao ya kujidhabihu na utayari wao wa kujifunza migawo yao mipya imefanya iwe rahisi kwetu kufanya kazi iliyohitajika.”

 Licha ya changamoto mbalimbali, tayari tumechapisha mamilioni ya nakala za kitabu Furahia Maisha Milele! Ili kutokeza vitabu hivyo, tunahitaji vitu mbalimbali, kutia ndani mabamba ya kuchapishia, karatasi za majalada, karatasi za kurasa, wino, na gundi. Katika miezi mitano ya kwanza ya uchapishaji, zaidi ya dola milioni 2.3 (za Marekani) zilitumiwa kununua vifaa tu. Ili kutumia pesa vizuri, tumechapisha tu idadi ya vitabu ambavyo vinahitajika na makutaniko.

“Kazi ya Sanaa”

 Walimu wa Biblia na wanafunzi wanahisije kuhusu kitabu hiki cha kujifunzia? Paul, ndugu kutoka Australia anasema hivi: “Ninafurahi sana kutumia kitabu Furahia Maisha Milele! kuongoza mafunzo ya Biblia. Habari katika kitabu hiki zimepangwa kwa njia nzuri inayochochea mazungumzo. Kitabu hicho kina ujumbe unaoeleweka vizuri, maswali yanayogusa moyo, pamoja na video, picha, chati, na malengo mbalimbali yatakayomsaidia mwanafunzi. Ni kazi ya sanaa inayonichochea kuboresha ufundishaji wangu.”

 Mwanafunzi mmoja wa Biblia nchini Marekani anasema hivi: “Ninakipenda kitabu hiki kipya. Picha zilizomo zinanisaidia kuelewa mambo makuu. Video hunigusa moyo na kunichochea kuchukua hatua.” Mwanafunzi huyo wa Biblia hujifunza mara mbili kwa juma naye anahudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida.

 Bado mamilioni ya nakala za kitabu Furahia Maisha Milele! zinahitaji kuchapishwa katika lugha nyingi. Isitoshe, kufikia sasa, Baraza Linaloongoza limeidhinisha kitabu hiki kichapishwe katika lugha 710, hiyo ni zaidi ya lugha 340 kuliko zile ambazo kitabu Biblia Inatufundisha kilichapishwa!

 Gharama za uchapishaji zinashughulikiwaje? Kupitia michango inayotolewa kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Michango mingi inatolewa kupitia donate.pr418.com. Tunathamini ukarimu wenu unaosaidia kutokeza vifaa vya kujifunzia Biblia kwa wale wanaotaka kujifunza kumhusu Yehova na ‘kufurahia maisha milele.’​—Zaburi 22:26.

a Kitabu hicho kilitolewa katika programu ya kiroho iliyokuwa sehemu ya mkutano wa kila mwaka.