Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Kudumisha Majumba Yetu ya Ufalme

Kudumisha Majumba Yetu ya Ufalme

APRILI 1, 2024

 Nicole, dada mchanga nchini Kolombia alisema hivi: “Ninalipenda Jumba letu la Ufalme! Ni mahali ambapo ninaweza kuwa pamoja na familia yangu ya kiroho.” Je, wewe unahisi vivyo hivyo?

 Ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova hukutana katika Majumba 63,000 ya Ufalme. Majengo hayo hutuandalia mahali ambapo tunaweza kumwabudu Mungu kwa starehe. Lakini majengo hayo yanatimiza mengi zaidi. Painia wa kawaida anayeitwa David nchini Kolombia anasema hivi: “Jumba letu la Ufalme linalipamba fundisho letu. Wageni wengi hujiuliza tunawezaje kuendelea kulitunza jengo hilo katika hali nzuri kadiri hiyo.” Kwa kweli, tunafanya kazi kwa bidii kufanya usafi na kudumisha Majumba yetu ya Ufalme. Kazi hiyo inashughulikiwaje?

Udumishaji Unaratibiwa Jinsi Gani?

 Makutaniko yanayotumia Jumba la Ufalme yana jukumu la kulidumisha. Ndugu na dada hufanya usafi wa Jumba lao la Ufalme kwa ukawaida. Wao pia hufanya udumishaji wa kuzuia madhara na ukarabati mdogo.

 Ili kusaidia makutaniko kudumisha Majumba yao ya Ufalme, Idara ya Usanifu Majengo na Ujenzi (LDC) inawapa akina ndugu mgawo wa kutumikia wakiwa wazoezaji wa udumishaji. Kila mzoezaji wa udumishaji hushughulikia Majumba sita hadi kumi ya Ufalme. Anawatembelea na kuwazoeza wahubiri katika makutaniko kuhusu jinsi ya kutunza jumba lao. Baada ya kila miaka mitatu, anakagua kila jengo na kutambulisha ikiwa kuna matatizo kuhusiana na usalama au ikiwa kuna udumishaji unaohitaji kufanywa.

Wazoezaji wa udumishaji wanatusaidia kudumisha Majumba yetu ya Ufalme yakiwa katika hali nzuri

 Ndugu na dada zetu huthamini mazoezi yanayoandaliwa na wazoezaji hao wa udumishaji. Dada nchini India anayeitwa Indhumathi, anasema hivi: “Mazoezi hayo yalikuwa yenye kupendeza sana. Tulifurahi sana kujifunza jinsi ya kudumisha jumba letu kwa njia inayofaa.” Ndugu nchini Kenya anayeitwa Evans, anasema hivi: “Tulijifunza jinsi ya kuokoa pesa nyingi kwa kurekebisha matatizo madogo kabla ya kuyaruhusu yawe makubwa.”

Kushughulikia Gharama

 Kila mwaka, gharama za uendeshaji na udumishaji za Jumba moja la Ufalme zinaweza kuwa kati ya mamia na maelfu ya dola, a ikitegemea jumba hilo liko wapi, lilijengwa zamani kadiri gani, na linatumiwa na makutaniko mangapi. Gharama hizo zinashughulikiwaje?

 Udumishaji wa Jumba la Ufalme hushughulikiwa kupitia michango. Alexander, ndugu anayeishi nchini Kazakhstan anaeleza hivi: “Sehemu ya michango hiyo hutumiwa kwa ajili ya kulipia Intaneti na huduma nyingine kama za maji na umeme. Michango mingine hutumiwa kununua bidhaa muhimu kama vile shashi, glavu, bidhaa za kufanyia usafi, na rangi.” Michango yoyote ya ziada hutolewa kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote ili kusaidia katika miradi mingine mikubwa zaidi ya udumishaji inayofanywa ulimwenguni pote na ambayo huenda ikiwa ya gharama kubwa zaidi.

Miradi Mikubwa Zaidi ya Udumishaji

 Ikiwa Jumba la Ufalme linahitaji kufanyiwa udumishaji na gharama zake zitazidi pesa ambazo zinatumiwa katika uendeshaji wa miezi miwili au mitatu, wazee watawasiliana na mzoezaji wa udumishaji wa LDC. Iwapo LDC itaidhinisha mradi huo, kwa kawaida gharama zilitashughulikiwa kwa kutumia michango ya kazi ya ulimwenguni pote. Katika mwaka wa utumishi wa 2023, miradi 8,793 kama hiyo ilikamilishwa, na iligharimu dola 76.6. Fikiria miradi miwili kati ya hiyo.

 Nchini Angola, Jumba la Ufalme lililojengwa miaka 15 iliyopita lilikuwa na matatizo kadhaa. Mfumo wa umeme ulihitaji kubadilishwa kabisa, kuta zilikuwa na nyufa, na majirani walilalamika kwamba maji yalikuwa yakitiririka kuingia katika nyumba zao. Idara ya LDC ilipanga kuwe na mradi wa kurekebisha matatizo hayo. Mradi huo uligharimu dola 9,285. Majirani walishukuru sana na walivutiwa sana na jinsi kazi hiyo ilivyofanywa.

Jumba la Ufalme lililofanyiwa ukarabati nchini Angola

 Nchini Poland, paa la Jumba la Ufalme lilikuwa likivuja na zulia lilikuwa limeharibika sana hivi kwamba halingeweza kurekebishwa. Idara ya LDC ilipanga kuwe na mradi wa kurekebisha paa na kubadili zulia hilo. Mradi huo uligharimu dola 9,757. Kwa sababu hiyo, Jumba hilo la Ufalme halitahitaji kufanyiwa ukarabati mkubwa kwa miaka kadhaa ijayo.

Ukarabati wa Jumba la Ufalme nchini Poland

Udumishaji Unaomtukuza Yehova

 Kazi ya udumishaji humletea Yehova sifa na wakati huohuo inasaidia kuokoa michango yenye thamani sana. Shaun, ndugu anayeishi nchini Tonga, anasema: “Kazi yetu ya udumishaji inatusaidia kumwabudu Yehova katika Jumba la Ufalme lililo safi, nadhifu, na linalofanya kazi vizuri na ambalo linawafanya watu katika jamii waliheshimu jina lake. Tunajivunia kuwaalika watu katika Jumba letu la Ufalme.”

Unaweza Kusaidiaje?

 Sisi sote tunaweza kusaidia kufanya usafi na kudumisha majengo yetu ya ibada. Marino, mzoezaji wa udumishaji nchini Australia, anasema hivi: “Sisi sote tunaweza kushiriki katika pendeleo muhimu la kutunza Majumba yetu ya Ufalme. Tunapofanya hivyo, tunasaidia sana kuhifadhi michango ili iweze kutumiwa mahali inapohitajika zaidi.”

 Joel, ndugu nchini India, anafurahia kufanya udumishaji kwenye Jumba lao la Ufalme. Anasema hivi: “Kufanya kazi pamoja na ndugu zangu hunisaidia kuwazia jinsi hali itakavyokuwa katika ulimwengu mpya.” Nicole, aliyetajwa mapema, alisema hivi: “Hivi karibuni nilisaidia kusafisha sakafu huku akina ndugu waliporekebisha choo. Ingawa sikuhusika katika kazi hiyo ya urekebishaji, nilisaidia kuzuia aksidenti.”

 Ikiwa ungependa kujitolea kusaidia kudumisha Jumba lenu la Ufalme, zungumza na wazee wa kutaniko lenu. Mbali na hilo, michango yako inategemeza udumishaji wa Jumba lenu la Ufalme na pia Majumba mengine ya Ufalme ulimwenguni pote. Michango hiyo inaweza kutumbukizwa kwenye masanduku ya michango kwenye jumba lenu au kupitia donate.pr418.com. Tunathamini sana roho yako ya ukarimu.

Sisi sote tunaweza kusaidia kutunza Majumba yetu ya Ufalme

a Dola zinazotajwa katika makala hii ni za Marekani.