Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushoto: Wafanyakazi wa kutoa msaada nchini Chile walisaidia kujenga upya nyumba ya wenzi wa ndoa iliyoharibiwa na moto. Kulia: Dada wawili nchini Nigeria walipokea bidhaa baada ya eneo lao kukumbwa na mafuriko mabaya

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Kutoa Msaada Katika 2023—⁠“Tumejionea Wenyewe Upendo wa Yehova”

Kutoa Msaada Katika 2023—⁠“Tumejionea Wenyewe Upendo wa Yehova”

JANUARI 26, 2024

 Biblia ilitabiri kwamba “taifa litapigana na taifa” na kutakuwa na misiba wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, 7) Tumeona maneno hayo ya kiunabii yakitimizwa katika mwaka wa utumishi wa 2023. a Lakini licha ya vita na misiba ya asili katika karibu nchi 100, Mashahidi wa Yehova wameonyesha kwamba wana upendo kama wa Yehova. Jinsi gani?

 Katika mwaka wa utumishi wa 2023, ndugu zetu waliathiriwa na misiba zaidi ya 200 ya asili na pia iliyosababishwa na mwanadamu. Kwa ujumla mashirika ya kisheria yanayotumiwa na Mashahidi wa Yehova yametumia zaidi ya dola milioni kumi b zilizotolewa kama michango ya kazi ya ulimwenguni pote ili kutoa msaada wakati wa msiba. Hiyo inatia ndani michango ambayo ilitolewa na ndugu na dada wengi waliojitolea katika maeneo yao. Ona jinsi ambavyo michango ilivyotumiwa kuwasaidia watu walioathiriwa na misiba miwili tu kati ya mingi iliyowapata ndugu zetu.

“Upendo wa Kweli Ni Halisi”

 Maeneo fulani nchini Nigeria hupatwa na mafuriko mara kwa mara. Lakini, Oktoba 2022 kulikuwa na mafuriko mabaya zaidi kuwahi kutokea katika kipindi cha miaka 10. Zaidi ya ekari 1,670,432 za mashamba ziliharibiwa, na zaidi ya watu milioni mbili walilazimika kuhama makao yao. Upesi ofisi ya tawi ya Nigeria iliweka rasmi Halmashauri za Kutoa Msaada ili kupanga jitihada hizo na pia kuandaa msaada wa kiroho.

Akina ndugu nchini Nigeria walivuka barabara na mito iliyofurika ili kupeleka misaada

Athari Ambazo Ndugu na Dada Zetu Wamepata

  •   Wahubiri 7,505 wamelazimika kuhama makao yao

  •   Nyumba 860 zimepata uharibifu mdogo au zimeharibiwa kabisa

  •   Majumba ya Ufalme 90 yalipatwa na mafuriko kutia ndani Jumba moja la Kusanyiko

Jinsi Michango Ilivyotumiwa

 Zaidi ya dola 250,000 zilitumiwa katika kutoa msaada, ambayo ilitia ndani:

  •   Chakula kama vile mchele, maharagwe na tambi

  •   Bidhaa kama vile magodoro na neti za mbu

  •   Marekebisho au ujenzi wa nyumba zilizoharibika

 Akina ndugu walihakikishaje kwamba michango ilitumiwa kwa hekima? Njia moja ni kukagua kwa uangalifu kila jengo na kuona ikiwa linaweza kurekebishwa. Ikiwa ingekuwa lazima kujenga jengo jipya, lilijengwa kwa njia rahisi kulingana kawaida ya eneo hilo.

 Ndugu na dada zetu ambao wamepokea msaada huo wameshukuru sana. Dada mmoja alisema hivi: “Mafuriko yalivuruga maisha yetu kwa sababu mashamba yetu yote yaliharibiwa na tukakosa makao. Tulipata kitulizo ndugu na dada zetu walipokuja siku hiyohiyo kutusaidia na kutuandalia makao salama. Tulipata msaada mkubwa chakula kutoka kwenye ofisi ya tawi. Tulipigwa na butwaa tulipojionea wenyewe utimizo wa andiko la Yohana 13:34, 35 katika maisha yetu. . . . Upendo wa kweli ni halisi. Mimi na familia yangu yote tunasema asante sana kutoka moyoni, kwa kutusaidia kwa wakati unaofaa.”

 Wengine katika jamii waliiona kazi yetu ya kutoa msaada. Chifu wa eneo la Sabagreia, katika Jimbo la Bayelsa, alisema hivi: “Ulimwenguni pote kuna mashirika na makanisa mengi, lakini ni Mashahidi wa Yehova tu ndio wamefanya jambo kama hili. . . . Shirika [lenu] ndilo bora zaidi ulimwenguni.”

“Tumejionea Wenyewe Upendo wa Yehova”

 Februari 2023, mioto zaidi ya 400 ilisababisha uharibifu mkubwa sana nchini Chile. Mashamba zaidi ya ekari 1,062,553 pamoja na miundombinu muhimu iliharibiwa nchini humo. Watu wapatao 8,000 walihamishwa. Punde tu baada ya msiba huo kutokea, ofisi ya tawi ilianza kufanya mipango ya kutoa msaada.

Nchini Chile, wafanyakazi wa kutoa misaada walijenga upya nyumba ya familia moja ambayo haingeweza kurekebishwa

Athari Ambazo Ndugu na Dada Zetu Wamepata

  •   Wahubiri 222 walihamishwa

  •   Nyumba 20 ziliharibiwa

Jinsi Michango Ilivyotumiwa

 Zaidi ya dola 200,000 zilitumiwa katika kutoa msaada, ambayo ilitia ndani:

  •   Chakula na maji

  •   Petroli, bidhaa za kusafishia, na dawa

  •   Ujenzi wa nyumba zilizoharibika

 Familia moja ilishtuka kuona kwamba vitu vyao vyote viliharibiwa, kutia ndani nyumba yao na biashara yao. Hilo liliwaacha bila njia ya kujipatia riziki. Katika siku chache za mwanzoni, familia ilihuzunika sana kuona eneo tupu ambapo nyumba yao ilikuwa imesimama hapo awali. Lakini kadiri ujenzi ulivyoendelea, ndivyo walivyoanza kujihisi vizuri. Upendo walioonyeshwa na wajitoleaji hao uliwawezesha kukabiliana na hali yao. Familia hiyo ilichochewa sana na jambo hilo hivi kwamba wakajiunga na wajitoleaji hao kumjengea upya ndugu mwingine nyumba yake.

 Ndugu na dada zetu wengi waliguswa moyo sana na kazi ya kutoa msaada. Ndugu mmoja alisema hivi: “Uandalizi wa Yehova wa Halmashauri za Kutoa Msaada ni mzuri ajabu. Siku moja baada ya msiba huo, tayari walikuwa hapo wakiandaa mahitaji ya msingi. Inatia moyo kusoma kuhusu kazi ya kutoa msaada katika sehemu nyingine za dunia. Lakini jambo hilo linapokupata, inakuwa tofauti kabisa. Unakuja kuthamini tengenezo zaidi; jinsi akina ndugu wanavyoiga sifa za Yehova; na jinsi wanavyohangaikia mahitaji yetu ya kimwili, kiroho, na kihisia. Tumejionea wenyewe upendo wa Yehova.”

 Kadiri huu mfumo unavyokaribia kwisha, ndivyo tutakavyojionea ongezeko la misiba. (Luka 21:10, 11) Hata hivyo, kupitia kutaniko la Kikristo, tutajionea pia kwamba Mfalme wetu mwenye upendo, Kristo Yesu yuko pamoja nasi “sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Michango yako ya ukarimu kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote kupitia donate.pr418.com na njia nyingine, pamoja na kutoa wakati wako na nguvu zako, kunaonyesha kwamba unaunga mkono Ufalme na Mfalme wake mwenye upendo.

a Mwaka wa utumishi wa 2023 ulianza Septemba 1, 2022, na kwisha Agosti 31, 2023.

b Kiwango cha dola katika makala hii kinarejezea dola za Marekani.