Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Kutoa Msaada kwa Walioathiriwa na Misiba

Kutoa Msaada kwa Walioathiriwa na Misiba

FEBRUARI 1, 2021

 Mwaka wa 2020 ulikuwa na misiba mingi ya asili pamoja na mlipuko wa ugonjwa wa virusi vya corona (COVID-19) unaoathiri dunia nzima. Mashahidi wa Yehova wamewasaidiaje walioathiriwa?

 Katika mwaka wa utumishi wa 2020, a Halmashauri ya Waratibu ya Baraza Linaloongoza iliidhinisha dola milioni 28 b zitumiwe katika kutoa msaada. Kiasi hicho kilitumika kuwasaidia walioathiriwa na majanga zaidi ya 200—kutia ndani ugonjwa wa COVID-19, vimbunga kadhaa, mafuriko barani Afrika, ukosefu wa chakula nchini Venezuela, na ukame nchini Zimbabwe. Michango iliyotolewa ilisaidia kulipia chakula, maji, makao, nguo, na matibabu, pamoja na vifaa vya kufanyia usafi, ukarabati, na kujenga upya nyumba zilizoharibiwa. Fikiria mifano michache ya jinsi kazi ya kutoa msaada ilivyofanywa.

 COVID-19. Ulimwenguni pote, ugonjwa wa corona uliwaathiri ndugu na dada zetu kimwili, kihisia, na kiuchumi. Ili kuwasaidia, zaidi ya Halmashauri 800 za Kutoa Msaada zilianzishwa ulimwenguni pote. Halmashauri hizo zilichunguza mahitaji ya ndugu zetu na kutayarisha ripoti haraka iwezekanavyo zilizosaidia Halmashauri ya Waratibu kutambua njia bora ya kutoa msaada.

 Katika mwaka wote, Halmashauri za Kutoa Msaada ziliwasaidia wengi kupata chakula, maji, bidhaa za usafi, na dawa. Katika maeneo fulani, Halmashauri za Kutoa Msaada zilifanya kazi pamoja na wazee ili kuwasaidia akina ndugu kupata msaada wa serikali.

 Watu ambao si Mashahidi wametambua kazi yetu ya kutoa msaada. Kwa mfano, Field Simwinga, mkuu wa wilaya ya Nakonde, Zambia, aliwaambia ndugu zetu hivi: “Tuna deni kubwa kwenu kwa jinsi mlivyosaidia familia zilizoathiriwa kwa wakati unaofaa.”

 Upungufu wa Chakula Nchini Angola. Kwa sababu ya ugonjwa wa COVID-19, chakula kilipungua sana nchini Angola na bei zikapanda sana. Ilikuwa vigumu sana kwa ndugu na dada zetu kununua chakula.

Vifurushi vya chakula vilivyosafirishwa kutoka Brazili kwenda Angola

 Ofisi ya tawi ya Brazili iliombwa itoe msaada kwa kutuma vifurushi vya chakula kwa akina ndugu wa Angola. Ili kutumia pesa za msaada kwa njia bora, akina ndugu walifanya uchunguzi ili kupata njia bora zaidi ya kununua na kusafirisha chakula, kisha wakanunua chakula kingi. Hivyo, kununua na kusafirisha kila kifurushi kuligharimu dola 22 hivi lakini kilikuwa na kilogramu 20 hivi za chakula kama vile mchele, maharagwe, na mafuta ya kupikia. Kufikia sasa, vifurushi 33,544 vimesafirishwa—jumla ya tani 654. Ukijumlisha bidhaa zilizonunuliwa nchini Angola, maandalizi hayo yalisaidia kuwalisha zaidi ya watu 50,000!

 Ndugu zetu wanahisije kuhusu msaada huo? Alexandre, anayeishi katika eneo la mbali la Angola, anasema hivi: “Ninaona yote haya kuwa uthibitisho kwamba Yehova ananipenda na siko peke yangu. Ninathaminiwa na tengenezo la Yehova!” Mariza, mama asiye na mwenzi, anasema hivi: “Yehova alisikia kilio changu. Ninamshukuru yeye pamoja na tengenezo lake!”

Ndugu nchini Angola wanashukuru kupata msaada

 Msaada wa Ukame Nchini Zimbabwe. Katika mwaka wa utumishi wa 2020, Zimbabwe ilikumbwa na ukame mbaya sana, na mamilioni ya watu walipatwa na njaa kali sana. Maelfu ya Mashahidi nchini Zimbabwe walikosa chakula cha kutosha.

 Halmashauri tano za Kutoa Msaada zilianzishwa ili kusaidia kuwaandalia ndugu zetu chakula. Mamia ya wahubiri walisaidia kupakia chakula, mahitaji mengine, au walitoa magari yao yatumiwe katika kazi hiyo. c Katika mwaka wa utumishi wa 2020, dola 691,561 zilitumiwa kulisha zaidi ya watu 22,700!

Ndugu nchini Zimbabwe wakipokea msaada wa chakula (kabla ya janga la corona)

 Katika visa fulani, akina ndugu walikuwa wamemaliza akiba yao yote ya chakula kufikia wakati ambapo msaada uliwafikia. Chakula hicho kilipofika, ndugu zetu walimsifu Yehova. Baadhi yao hata walianza kuimba nyimbo za Ufalme.

 Katika eneo moja, Mashahidi wawili wajane walihudhuria mkutano katika jamii uliopangwa kuzungumzia chakula cha msaada kilichokuwa kikiandaliwa na shirika fulani ambalo si la serikali (NGO). Hata hivyo, mkutano huo ulianza kuhusisha mambo ya kisiasa, kwa hiyo, dada zetu waliamua kwamba hawatakubali masharti yaliyotolewa ya kupokea msaada. Walipokuwa wakiondoka kwenye mkutano huo, walidhihakiwa na kuambiwa, “Msije nyumbani kwetu kutuomba chakula!” Hata hivyo, majuma mawili baadaye, ndugu zetu walifika katika eneo hilo na kuwapa dada hao msaada wa chakula—muda mrefu kabla ya shirika hilo lisilo la serikali kufika!

Prisca anasema, “Yehova hajawahi kamwe kushindwa kuwatunza watumishi wake”

 Kazi ya kutoa msaada nchini Zimbabwe imesaidia pia kutoa ushahidi mzuri. Kwa mfano, fikiria kisa cha Prisca, anayeishi katika kijiji kidogo. Licha ya hali ngumu zilizoletwa na ukame, Prisca alitenga kila Jumatano na Ijumaa ili kushiriki katika huduma, hata wakati wa msimu wa kulima. Watu katika kijiji chake walimdhihaki na kumwambia: “Familia yako itakufa njaa ukihubiri tu.” Prisca aliwajibu hivi: “Yehova hajawahi kamwe kushindwa kuwatunza watumishi wake.” Baada ya muda mfupi, alipokea msaada kutoka kwa tengenezo letu. Hilo liliwashangaza baadhi ya jirani zake ambao walimwambia Prisca hivi: “Mungu hajawahi kushindwa kukutunza, kwa hiyo, tungependa kujifunza mengi zaidi kumhusu.” Sasa jirani zake saba wanasikiliza mikutano ya kutaniko inayopeperushwa kupitia redio.

 Tunapozidi kukaribia mwisho, tutaendelea kupatwa na misiba ya asili. (Mathayo 24:3, 7) Michango yako yenye ukarimu inayotolewa kupitia njia mbalimbali zinazoonyeshwa kwenye donate.pr418.com inathaminiwa sana. Inatoa msaada kwa wakati unaofaa na kwa njia inayofaa.

a Mwaka wa utumishi wa 2020 unatia ndani mwezi wa Septemba 2019 hadi Agosti 2020.

b Dola zinazotajwa katika makala hii ni za Marekani.

c Kwa sababu ya vizuizi vinavyohusiana na ugonjwa wa COVID-19, ndugu zetu walihitaji kupata vibali vya kusambaza chakula. Pia, walichukua tahadhari za kupunguza uwezekano wa kuambukizwa ugonjwa huo.