Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Majengo Yanayomtukuza Mfundishaji Wetu Mkuu

Majengo Yanayomtukuza Mfundishaji Wetu Mkuu

JULAI 1, 2023

 Yehova anapenda kuwaelimisha watu wake. Kwa sababu hiyo, tengenezo letu limeanzisha shule kadhaa zinazowazoeza wanafunzi kutimiza migawo yao. Mojawapo ya shule hizo ni Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme (SKE). Katika miaka ya karibuni, tengenezo la Mungu limekazia uangalifu kuboresha, si mtaala tu, bali pia kuboresha majengo ambayo hutumiwa kuendesha shule hizo za kitheokrasi. Lengo kuu ni kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa ajili ya wanafunzi na walimu. Michango yako inatusaidiaje kutimiza lengo hilo?

Wanafunzi Wengi Zaidi Katika Mazingira Bora Zaidi

 Kwa miaka mingi, shule za kitheokrasi zimeendeshwa kwenye Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko. Basi, kwa nini hivi karibuni tumejenga au kufanya ukarabati wa majengo mengi zaidi ambayo sasa yanatumiwa hasa kwa ajili ya shule za kitheokrasi? Fikiria sababu tatu.

 Mahitaji makubwa zaidi. Christopher Mavor, msaidizi wa Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza anaeleza hivi: “Ofisi za tawi zimeripoti kwamba kuna uhitaji mkubwa sana shambani. Kwa mfano, katika mwaka wa 2019, ofisi ya tawi ya Brazili ilikadiria kwamba wahitimu 7,600 hivi wa SKE walihitajika ili kushughulikia mahitaji ya eneo la ofisi yao ya tawi.” Ofisi ya tawi ya Marekani inaripoti kwamba kuna uhitaji mkubwa wa mapainia wanaostahili wanaoweza kuwazoeza wengine katika kazi ya mahubiri ya hadharani ya pekee katika miji mikubwa, mahubiri ya bandarini, na mahubiri ya gerezani. Pia kuna uhitaji wa ndugu wanaoweza kutumikia katika Idara ya Usanifu-Majengo na Ujenzi na pia kwenye Halmashauri za Uhusiano na Hospitali. Wahitimu wa SKE wanaweza kusaidia kujazia uhitaji huo.

 Wanafunzi wengi. Ofisi nyingi za tawi zimepokea maombi kutoka kwa wanafunzi wengi kuliko wanavyoweza kuwaalika. Kwa mfano, nchini Brazili ofisi ya tawi ilipokea maombi 2,500 katika mwaka mmoja tu. Kwa sababu ya majengo machache ya shule, ofisi ya tawi ingeweza kuwaalika wanafunzi 950 peke yake.

 Mahali pa kulala panapofaa. Wanafunzi wanapohudhuria shule kwenye Jumba la Ufalme au Jumba la Kusanyiko, kwa kawaida wanapata mahali pa kulala kwenye nyumba za ndugu na dada wenyeji. Mpango huo hufanikiwa katika maeneo ambako kuna madarasa machache kila mwaka. Lakini mahali ambapo kuna madarasa kadhaa, huenda isiwezekane kwa wahubiri kuwaalika wanafunzi kwa miezi mingi katika mwaka. Kwa hiyo, majengo huandaliwa karibu na darasa ambayo yametengenezwa kwa njia inayowafaa wanafunzi.

 Jengo lililo na darasa moja, kutia ndani makao ya walimu na wanafunzi 30 hivi pamoja na huduma nyingine za lazima, linaweza kugharimu dola milioni kadhaa za Marekani, kwa kutegemea eneo na mambo mengine.

Sehemu Mbalimbali Zinazofanyiza Jengo la Shule

 Kwa kawaida shule huendeshwa katika eneo lenye ukimya nje ya jiji kubwa lakini mahali ambapo usafiri unapatikana kwa urahisi. Maeneo yanayochaguliwa mara nyingi huwa na wahubiri wengi wanaoweza kusaidia katika uendeshaji wa shule na udumishaji wa majengo na vifaa.

 Majengo hayo yanakuwa na maktaba, maeneo ya kujifunzia, kompyuta, printa, na vifaa vingine. Mara nyingi, kunakuwa na chumba cha kulia chakula ambapo wanafunzi na walimu wanaweza kula pamoja. Pia kunakuwa na nafasi ya kutosha kwa ajili ya mazoezi ya kimwili na burudani.

 Darasa lenyewe hushughulikiwa kwa njia ya pekee. Troy anayefanya kazi pamoja na Idara ya Usanifu-Majengo na Ujenzi ya Ulimwenguni Pote ya Warwick, New York anaeleza hivi: “Tuliwasiliana na Idara ya Shule za Kitheokrasi ili kupata msaada wa kutayarisha madarasa ambayo yangefanya iwe rahisi zaidi kwa wanafunzi kujifunza. Ndugu hao walitupatia miongozo kuhusu ukubwa wa madarasa, mpangilio wake, kutia ndani mahitaji ya mwangaza na mfumo wa sauti na video.” Zoltán, mwalimu wa SKE nchini Hungaria alisema hivi kuhusu mfumo wa sauti: “Mwanzoni hatukuwa na vipaza sauti vyovyote, kwa hiyo mara nyingi tulihitaji kuwakumbusha wanafunzi wainue sauti. Lakini sasa kwa kuwa kuna maikrofoni kwenye kila dawati, tatizo hilo limetatuliwa!”

“Wageni wa Pekee wa Yehova”

 Majengo hayo yaliyoboreshwa yamekuwa na matokeo gani kwa walimu na wanafunzi? Angela, aliyehudhuria SKE huko Palm Coast, Florida, Marekani anasema hivi: “Ni mazingira matulivu sana. Kila kitu kilifikiriwa kwa uangalifu sana, kutia ndani darasa na vyumba vyetu ili tuweze kukazia fikira masomo yetu na kujifunza.” Csaba, mwalimu nchini Hungaria, anathamini sana nafasi za kula pamoja na wanafunzi. Anasema kwamba katika pindi hizo, “mara nyingi wanafunzi hufunguka na kutueleza mambo waliyojionea. Kwa njia hiyo, tunawafahamu wanafunzi hao vizuri zaidi. Hivyo, tunaweza kufundisha mtaala huu kwa njia inayofaa mahitaji yao zaidi.”

 Wanafunzi pamoja na walimu wanaona majengo ya shule yaliyoboreshwa kuwa baraka kutoka kwa ‘Mfundishaji wetu Mkuu,’ Yehova. (Isaya 30:20, 21) Dada mmoja nchini Filipino ambaye alihudhuria shule ya SKE katika jengo ambalo lilibadilishwa na kuwa darasa alisema hivi: “Mazingira ya shule yalitukumbusha kwamba sisi si wanafunzi tu bali ni wageni wa pekee wa Yehova. Anataka tujifurahishe kabisa tunapojifunza Neno lake kikamili.”

 Majengo ya shule yanafaulu kujengwa, kukarabatiwa, na kudumishwa kwa sababu ya michango yenu. Michango mingi kati ya hiyo hutolewa kupitia donate.pr418.com. Asante sana kwa ukarimu wako.

Mwingilio wa jengo la Palm Coast, Florida, Marekani

Kigezo cha hekalu katika siku za Yesu lililo kwenye mapokezi ya shule, Palm Coast, Florida, Marekani

Wanafunzi wakiwasili kwenye Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, Brazili

Darasa likiendelea, Brazili

Wanafunzi wakiwasili kwenye Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, Filipino

Kufurahia chakula cha mchana pamoja kwenye chumba cha kulia chakula cha shule, Filipino