Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Msaada Ulimwenguni Pote kwa Ajili ya Janga la Ulimwenguni Pote

Msaada Ulimwenguni Pote kwa Ajili ya Janga la Ulimwenguni Pote

JULAI 1, 2021

 Machi 2020, Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) lilipotangaza kwamba ugonjwa wa virusi vya corona (COVID-19) ni janga la ulimwenguni pote (tandavu), watu wengi hawakufikiria ugonjwa huo ungeendelea kwa zaidi ya mwaka mmoja. Mamilioni ya watu, kutia ndani Mashahidi wa Yehova wameathiriwa kimwili, kihisia, na kiuchumi na janga hili. Mashahidi wa Yehova wamefanya mipango gani ya kutoa msaada katika kipindi hiki?

Kutayarisha Misaada kwa Wanaohitaji

 Chini ya mwongozo wa Halmashauri ya Waratibu ya Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, zaidi ya Halmashauri 950 za Kutoa Msaada (DRC) zimeanzishwa ulimwenguni pote ili kukabiliana na COVID-19. Katika visa fulani, wamepanga misaada hiyo itolewe na wenyeji na katika visa vingine Mashahidi wamenufaika na misaada inayotoka kwa serikali. Pia, Halmashauri za Kutoa Msaada zimepanga msaada utolewe katika maeneo makubwa zaidi.

 Kwa mfano, fikiria hali ilivyokuwa huko Paraguai. Gazeti moja liliripoti kwamba madhara ya kiuchumi yaliyosababishwa na janga hilo “yamefanya idadi kubwa ya watu wanaoishi Paraguai wakose chakula.” Lakini Halmashauri ya Kutoa Msaada nchini Paraguai ilikuwa tayari imeanza kusambaza vifurushi ambavyo vingetumiwa kwa wiki mbili—chakula cha kutosha, sabuni, na vitu vinavyohitajika ili kudumisha usafi wa mtu binafsi. Kila kifurushi kiligharimu dola 30 za Marekani na kingetosha familia ya watu wanne.

 Watu wanaofanya kazi hiyo ya kutoa misaada wanajilindaje wasiambukizwe COVID-19? Wanavaa barakoa na kudumisha umbali unaofaa kati ya mtu mmoja na mwingine. Na pia wanahakikisha kwamba kampuni zinazowaletea bidhaa zinadumisha usafi unaohitajika na kwamba wanachukua tahadhari zote za usalama. Hii inatia ndani kuhakikisha kwamba wote wanaoshughulikia vifurushi vya msaada wanavaa mavazi ya kujilinda, wanasafisha na kuua vijidudu katika magari wanayotumia, na wanahifadhi vifurushi hivyo mahali paliposafishwa kwa dawa. Mwishowe, wale wanaowapelekea akina ndugu vifurushi hivyo wanahakikisha kwamba wamedumisha umbali unaofaa kati yao na wanaopokea.

Kutumia Michango kwa Hekima

 Kufikia Januari 2021, Halmashauri ya Waratibu ilikuwa imeidhinisha zaidi ya dola milioni 25 za Marekani zitumike kutoa msaada unaohusiana na COVID-19. Ofisi za tawi na Halmashauri za Kutoa Msaada hutumia michango hiyo kwa uangalifu na hutafuta bidhaa za bei nafuu zaidi. Kwa mfano, nchini Chile, ndugu wanaopanga misaada hiyo walitaka kununua kilo 750 za dengu. Lakini bei ya dengu ilikuwa imepanda kwa mara mbili katika mwezi mmoja tu! Saa mbili tu baada ya kukubali kununua mzigo wa dengu kwa bei hiyo ya juu, muuzaji akawaambia kwamba mnunuzi mwingine alikuwa amerudisha dengu alizokuwa amenunua. Kwa hiyo, badala ya kuwatoza bei ya juu waliyokuwa wamekubaliana, muuzaji huyo aliziuza tena kwa bei ile iliyokuwepo awali mwezi mmoja kabla ya bei kupanda!

 Hata hivyo, ndugu zetu walipoenda kuchukua dengu hizo, muuzaji alijaribu kuvunja makubaliano yao, akiwashutumu kuwa walikuwa na ubaguzi walipokuwa wakigawa chakula hicho, kama vile tu mashirika mengine yanavyofanya. Baada ya kutoa sala ya kimyakimya, mmoja kati ya ndugu zetu alimweleza muuzaji huyo kwamba kila kutaniko lilikuwa limefanya uchunguzi ili kujua wale walio na uhitaji zaidi. Kisha akaeleza kwamba kwa sababu ya tofauti za kitamaduni, kila kifurushi kiliwekwa vitu kulingana na mahitaji ya kila familia. Hatimaye, walimhakikishia muuzaji huyo kwamba michango yote ya pesa ni ya hiari na pia wahusika wote walifanya kazi hiyo kwa kujitolea. Jambo hilo lilimshangaza muuzaji huyo. Mbali tu na kukubali kuwauzia kwa ile bei ya chini, aliwaongezea kilo 400 za dengu kama mchango wake waliporudi kununua.

“Uthibitisho wa Upendo wa Kweli”

 Lusu, mwanamke mjane mwenye umri mkubwa nchini Liberia, anaishi na watu watano wa familia yake. Asubuhi moja walipokuwa wakila kiamsha-kinywa na kuzungumzia andiko la siku, mjukuu mmoja wa Lusu mwenye umri wa miaka saba aligundua kwamba hawakuwa na chochote cha kula kilichobaki nyumbani. Kisha akauliza, “Tutakula nini?” Lusu alimhakikishia kwamba tayari alisali na kumwomba Yehova msaada na alikuwa na uhakika kwamba Yehova angewasaidia. Alasiri hiyohiyo, Lusu alipokea simu kutoka kwa wazee wa kutaniko wakimwita aje kuchukua chakula cha msaada. Anasema hivi: “Mjukuu wangu alisema sasa anajua kwamba Yehova husikia na kujibu sala kwa sababu Yehova amejibu sala yangu.”

Watoto wanaoishi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo walichora picha kuwashukuru ndugu zao kwa chakula cha msaada

 Mwanamke mmoja katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ni jirani ya familia moja ya Mashahidi. Alipoona familia hiyo imepewa chakula na waamini wenzao, alisema hivi, “Baada ya janga hili, sisi pia tutakuwa Mashahidi wa Yehova kwa sababu wanawajali ndugu na dada zao wakati wa kipindi hiki kigumu.” Mume wake akamuuliza, “Kwa hiyo, unataka kuwa Shahidi wa Yehova kwa sababu tu ya mfuko wa mchele?” Mke wake akamjibu, “La hasha, ni kwa sababu mfuko huo wa mchele ni uthibitisho wa upendo wa kweli.”

 Mashahidi wa Yehova wamefaulu kuitikia haraka mahitaji ya akina ndugu na dada zetu wakati huu mgumu wa janga hili kwa sababu ya michango yako ya ukarimu. Asante kwa michango uliyotoa kwa kutumia njia zilizoonyeshwa kwenye donate.pr418.com.