Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Nyimbo Zinazotusaidia Kumkaribia Mungu Zaidi

Nyimbo Zinazotusaidia Kumkaribia Mungu Zaidi

NOVEMBA 1, 2021

 Muziki ni zawadi ya pekee kutoka kwa Yehova. Unaweza kuathiri mawazo yetu, kubadili hisia zetu, na kutuchochea kutenda. Nyimbo zetu zilizotungwa hutuathiri kwa njia hiyo. Kwa kweli, nyimbo hizo zinaweza kutimiza mengi zaidi: zinaweza kutusaidia kumkaribia Yehova zaidi.

 Tangu mwaka wa 2014, zaidi ya nyimbo 70 zilizotungwa zimetokezwa, na sasa angalau wimbo mmoja unapatikana katika zaidi ya lugha 500! Lakini huenda umejiuliza, ‘Ni nani wanaotokeza nyimbo hizo, na kazi hiyo inafanywaje?’

Jinsi Kazi Inavyofanywa

 Nyimbo zilizotungwa hutokezwa na timu ya muziki kwenye Idara ya Huduma za Sauti na Video, iliyo chini ya usimamizi wa Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza. Timu hiyo ya muziki imefanyizwa na ndugu na dada 13 wanaosaidia kutunga, kutokeza muziki, kuratibu, na kazi nyingine muhimu. Mbali na hilo, Halmashauri ya Ufundishaji imeidhinisha wajitoleaji wanaofanya kazi wakiwa nyumbani kusaidia katika kazi hiyo. Wajitoleaji hao walio ulimwenguni pote wanatia ndani watungaji, wanamuziki, na waimbaji. Ndugu na dada hao hutumia vipawa vyao kwa unyenyekevu bila kujitafutia sifa.

 Wimbo uliotungwa hutokezwaje? Kwanza, Halmashauri ya Ufundishaji huamua wimbo huo utategemea maandiko gani na ni hisia gani ambazo wasikilizaji wanapaswa kupata kutokana nao. Baada ya hapo, timu hiyo ya muziki hutoa migawo ya kutunga muziki na kuandika maneno ya wimbo. Kisha rekodi ya majaribio hutayarishwa. Halmashauri ya Ufundishaji husikiliza rekodi hiyo na kutoa mapendekezo ya jinsi ya kuiboresha. Kisha, timu ya muziki hufanya marekebisho na kutokeza wimbo utakaotolewa kwa wote. Nyimbo hizo hurekodiwa katika maeneo mbalimbali, kutia ndani majengo ya ofisi za tawi na studio za nyumbani.

 Ili kutunga na kurekodi nyimbo zilizotungwa, ndugu zetu hutumia kompyuta za kunasa sauti, zinazoweza kuandika alama za muziki, na mkusanyo wa sauti zilizohifadhiwa, na mambo mengine. Pia kazi hiyo hufanywa kwa kutumia vifaa kama vile ala za muziki, mashine za kuchanganya na kukuza sauti, spika, na maikrofoni. Kila moja ya maikrofoni hizo inaweza kugharimu kuanzia dola 100 hadi zaidi ya dola 1,000 hivi (za Marekani). Katika mwaka wa 2020, tulitumia dola 116,000 (za Marekani) kununua vifaa vya kurekodi muziki.

 Ni jitihada gani zinazofanywa ili kuhifadhi pesa? Badala ya kuwa na timu kubwa ya muziki Betheli, tunatumia wajitoleaji wengi wanaoishi nyumbani. Mbali na hilo, badala ya wanamuziki wengi kukutana pamoja ili kurekodi muziki wa okestra, mara nyingi ndugu zetu hutunga na kutokeza muziki kwa kutumia kompyuta.

“Zinanisaidia Kuendelea Kuwa Hai Kiroho”

 Ndugu na dada hupenda kusikiliza nyimbo zilizotungwa. Tara anayeishi nchini Ujerumani, anasema hivi: “Nyimbo hizo hunisaidia kutulia ninapohisi nina mkazo. Ninapozisikiliza katika lugha yangu ya asili, ninahisi ni kama Yehova ananikumbatia.” Ndugu Dmitry anayeishi nchini Kazakhstan anasema hivi: “Ninafurahi kwamba ninaweza kusikiliza nyimbo hizo bila kuwa na wasiwasi ikiwa zinapatana na kanuni za Biblia. Isitoshe, nyimbo hizo zimenisaidia kukazia fikira mambo ya kiroho.”

 Delia, anayeishi nchini Afrika Kusini, anaeleza jinsi anavyohisi kuhusu nyimbo zilizotungwa: “Zinanisaidia kuendelea kuwa hai kiroho. Ninapokuwa na huzuni au ninapokabili changamoto fulani, sikuzote mimi hupata wimbo unaofaa hali yangu kabisa. Mara nyingi, mdundo wa nyimbo hizo tu unatosha kunifanya nijihisi vizuri!”

 Ndugu na dada fulani wanapenda sana baadhi ya nyimbo hizo. Lerato, ambaye pia anaishi nchini Afrika Kusini, anasema hivi: “Wimbo wenye kichwa ‘Paradiso Ipo Karibu Sana’ na ‘Ulimwengu Mpya’ hunisaidia kuwazia wakati ambapo nitakuwa tena na mama yangu mpendwa. Kila mara ninaposikiliza nyimbo hizo, mimi humwona akinikimbilia akiwa amenyoosha mikono yake ili anikumbatie.”

 Wimbo mmoja uliotungwa ulimsaidia sana kijana nchini Sri Lanka. Anasema hivi: “Mwalimu wa sayansi alinikemea kwa ukali mbele ya darasa lote kwa sababu mimi ni Shahidi wa Yehova. Niliingiwa na woga na sikujua niseme nini. Niliporudi nyumbani, mama yangu alinitia moyo nisikilize wimbo wenye kichwa ‘Funzo Hujenga.’ Wimbo huo ulinisaidia kuona uhitaji wa kufanya utafiti na kutayarisha majibu. Siku iliyofuata, nilizungumza na mwalimu wangu. Alinisikiliza na kusema kwamba sasa anaelewa imani ya Mashahidi wa Yehova. Ninalishukuru tengenezo la Yehova kwa kutuandalia nyimbo hizo zenye kutia moyo.”

 Gharama za kutokeza nyimbo hizo zinashughulikiwaje? Kupitia michango inayotolewa kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Michango mingi hutolewa kupitia mbinu zinazoonyeshwa kwenye donate.pr418.com. Asante sana kwa michango yako ya ukarimu.