Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mnamo 2017 darasa la Shule ya Gileadi likiendelea

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Shule ya Gileadi—Shule ya Kimataifa

Shule ya Gileadi—Shule ya Kimataifa

DESEMBA 1, 2020

 Kila mwaka, watumishi kadhaa wa pekee wa wakati wote kutoka ulimwenguni pote hualikwa kuhudhuria Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) inayofanyiwa kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York. a Kwenye shule hiyo, wanafunzi hujifunza jinsi ya kuwa wenye matokeo zaidi katika migawo yao mbalimbali katika tengenezo la Yehova. Mazoezi hayo huwasaidia kujenga na kuimarisha makutaniko na ofisi za tawi ulimwenguni pote.

 Kwa kweli, Gileadi ni shule ya kimataifa. Kwa mfano, darasa la 147 lililofanywa mwaka wa 2019, lilikuwa na wanafunzi 56, kutoka nchi 29. Wanafunzi wanaohudhuria Shule ya Gileadi wamekuwa wakitumikia katika aina fulani ya utumishi wa pekee wa wakati wote wakiwa Wanabetheli, waangalizi wa mzunguko, wamishonari, au mapainia wa pekee.

 Maandalizi kwa ajili ya shule huanza muda mrefu sana kabla ya kikao cha kwanza darasani. Kwa mfano, Idara ya Usafiri ya Makao Makuu ya Ulimwenguni Pote (WHQ Travel) hununua tiketi za ndege za wote waliokaribishwa kuhudhuria shule hiyo. Kwa ajili ya darasa la 147 la Gileadi, wastani wa gharama iliyotumiwa kumfikisha kila mwanafunzi Patterson na kumrudisha nyumbani ilikuwa dola 1,075 za Marekani. Wanafunzi kutoka Visiwa vya Solomon walihitaji kuunganisha safari nne za ndege ili kufika Patterson kisha safari tatu ili kurudi nyumbani—jumla ya kilomita 35,400! Gharama ya safari hizo za ndege ilikuwa dola 2,300 za Marekani kwa kila mwanafunzi. Ili kuokoa gharama, idara ya WHQ Travel hutumia programu ya kompyuta inayowasaidia kupata tiketi ya gharama nafuu. Na hata baada ya kupata tiketi, programu hiyo huendelea kutafuta kwa majuma na hata miezi kuona ikiwa bei itashuka. Pia idara ya WHQ Travel hutumia kilomita ambazo wengine wamezawadiwa na mashirika ya ndege ili kupata tiketi.

 Wanafunzi wengi wanahitaji viza ili kuingia nchini Marekani. Ili kushughulikia hilo, Idara ya Sheria ya Makao Makuu ya Ulimwenguni Pote huwasaidia kupata viza za wanafunzi. Viza hizo pamoja na ada ya kuwasajili ni wastani wa dola 510 kwa kila mwanafunzi.

 Tunanufaikaje kutokana na mazoezi ambayo wanafunzi wanapokea? Hendra Gunawan anatumikia akiwa mzee Kusini-Mashariki mwa Asia. Katika kutaniko lake kuna wenzi wa ndoa ambao walihitimu kutoka Shule ya Gileadi. Anasema hivi: “Hapo awali, kutaniko letu halikuwa na mapainia wa kawaida. Lakini baada ya wahitimu hao kufika, bidii yao na roho ya kujitolea iliwaambukiza wengine wakaamua kuanza kufanya upainia. Baadaye, dada mmoja katika kutaniko letu alihudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme!”

 Sergio Panjaitan anafanya kazi pamoja na wahitimu wa Shule ya Gileadi katika Betheli iliyoko Kusini-Mashariki mwa Asia. Anasema hivi: “Mazoezi waliyopata hayakuwa baraka kwao tu; yamekuwa baraka kwetu pia. Walijifunza mambo mengi! Lakini badala ya kujaribu kuonekana kuwa wa pekee, wanawaeleza wengine mambo waliyojifunza. Hilo hututia moyo, nasi pia tunawatia moyo wengine.”

 Gharama za shule hiyo hushughulikiwaje? Ni kutokana na michango ya kazi ya ulimwenguni pote, ambayo kiasi kikubwa hutolewa kupitia mojawapo ya mbinu zilizo kwenye donate.pr418.com. Tunakushukuru sana kwa michango yako ya ukarimu, ambayo hutegemeza shule hii ya kimataifa.

a Mtaala wa shule hii hutayarishwa na kudumishwa na Idara ya Shule za Kitheokrasi, chini ya usimamizi wa Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Walimu wa idara hiyo hufundisha shule hiyo, na pia walimu wengine, kutia ndani washiriki wa Baraza Linaloongoza.