Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kazi kubwa inahitaji kufanywa ili kukarabati ofisi ya tawi ya Japani (kushoto) na kupanua majengo ya ofisi ya tawi ya Angola (kulia)

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Ujenzi Unaotusaidia Kuhubiri

Ujenzi Unaotusaidia Kuhubiri

OKTOBA 20, 2023

 Baraza Linaloongoza linajitahidi sana kutumia michango kuandaa majengo ambayo yatatusaidia kuendeleza kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Kwa mfano, katika mwaka wa utumishi wa 2023, mashirika ya kisheria yanayotumiwa na Mashahidi wa Yehova yalitumia zaidi ya dola milioni 500 kununua, kujenga, kukarabati na kudumisha Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko ulimwenguni pote. a Kiasi hicho hakitii ndani pesa ambazo makutaniko ulimwenguni pote hutumia kudumisha Majumba yao ya Ufalme.

 Kwa kuongezea, michango hutumiwa pia kwa ajili ya kujenga na kudumisha ofisi za tawi zinazosaidia kupanga na kusimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Tumerahisisha utendaji wa ofisi za tawi ili michango zaidi itumiwe kujenga na kukarabati Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko. Bado kuna uhitaji wa kukarabati, kujenga upya, au kuhamisha ofisi za tawi. Kwa nini miradi hiyo ni muhimu? Ofisi za tawi zinaunga mkono jinsi gani kazi muhimu inayofanywa shambani? Acheni tuone.

“Kuhakikisha Jengo Litadumu Zaidi”

 Ofisi nyingi za tawi zilijengwa zaidi ya miaka 30 au 40 iliyopita. Nicholas, anayefanya kazi katika Idara ya Usanifu Majengo na Ujenzi ya Makao Makuu anaeleza hivi: “Hata jengo linalotunzwa na kudumishwa vizuri huzeeka na kuharibika kadiri muda unavyopita. Ukarabati husaidia kuhakikisha jengo litadumu zaidi na kutumiwa kwa muda mrefu zaidi.”

 Ofisi za Betheli pia zinahitaji kubadilikana ili kutosheleza mahitaji yanayobadilika ya tengenezo. Ulimwenguni pote idadi ya wahubiri imeongezeka sana tangu ofisi nyingi za tawi zilipojengwa. Ili kushughulikia ukuzi huo, kumekuwa na uhitaji wa wajitoleaji wengi wanaofanya kazi katika ofisi hizi. Kwa sababu hiyo, majengo ya Betheli ambayo mwanzoni yalionekana kuwa na nafasi ya kutosha, sasa yanaonekana kuwa madogo!

 Pia, tunazingatia sana usalama. Kadiri siku za mwisho zinavyosonga, ndivyo tunavyokabili majanga mengi ya asili yanayohatarisha uhai wetu. (Luka 21:11) Kutumia mbinu mpya za ujenzi kunafanya majengo hayo yawe salama zaidi kwa wale wanaofanya kazi katika majengo hayo. Pia maboresho hayo hufanya majengo hayo yafae kuwa vituo vya kuratibu kazi ya kutoa msaada na kutegemeza kazi ya kuhubiri baada ya janga la asili kutokea.

“Yehova Amebariki Uamuzi Huu”

 Chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza, ujenzi muhimu umefanyika katika ofisi 43 za tawi, katika mwaka wa utumishi wa 2023. Hilo linamaanisha kwamba karibu nusu ya Betheli zote ulimwenguni zilifanyiwa aina fulani ya ujenzi. Ona mifano michache inayokazia umuhimu wa kazi ya ujenzi inayofanywa.

 Angola. Matt, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Angola, anasema hivi: “Tumepata pendeleo la kuona unabii wa Hagai 2:7 ukitimia kwa njia ya pekee. Ndani ya miaka kumi tu, tumejionea ongezeko la wahubiri la asilimia 60! Ili kuwategemeza wahubiri hao, familia ya Betheli ilihitaji kuongezeka mara tatu. Hata hivyo, kwa sababu ya kukosa nafasi katika majengo yetu ya Betheli hatukuweza kuwaalika watu wengi kuja kufanya kazi hapa kama tulivyohitaji. Hilo liliwafanya Wanabetheli wengi kubeba mzigo mzito na kufanya kazi mara nyingi baada ya muda wa kawaida.”

Ofisi mpya (kulia) zinasaidia kutokeza mazingira mazuri zaidi ya kufanyia kazi

 Akina ndugu walipewa mgawo wa kufanya utafiti ili kushughulikia uhitaji uliokuwa ukiongezeka. Mwanzoni, walihisi kwamba njia bora na ya haraka ya kushughulikia hilo ilikuwa ni kukarabati majengo yaliyopo ya ofisi ya tawi. Lakini baada ya kufanya utafiti wa kina, walitambua kwamba kufanya ukarabati huo kusingekuwa njia bora ya kutumia michango inayotolewa. Badala yake walipendekeza kununua na kukarabati jengo lililokuwa karibu na ofisi ya tawi. Matt anasema: “Wazo hilo lilipoletwa mbele ya Halmashauri ya Tawi kwa mara ya kwanza, tulihangaishwa sana na kuhisi kwamba huenda jengo hilo lisiwe na ubora kama ule wa majengo ambayo sisi wenyewe tunajenga. Lakini sasa tunaona jinsi jengo hilo linavyotosheleza uhitaji wetu. Yehova amebariki uamuzi huu.”

Majengo ya makazi yanayoweza kubadilishwa yatumiwe kwa njia tofauti baadaye yamesaidia kuwe na wafanyakazi wengi zaidi wa kutegemeza kazi inayozidi kuongezeka shambani

 Huenda ofisi ya tawi ya Angola ikahitaji nafasi zaidi wakati ujao. Hata hivyo, majengo hayo mapya pamoja na majengo ya makazi yanayoweza kubadilishwa yatumiwe kwa njia tofauti baadaye, na pia majengo ya kukodi yaliyo nje ya eneo la ofisi hiyo, yameisaidia ofisi hiyo ya tawi kuwa na nafasi ya kutosha na hivyo kutegemeza ukuzi mkubwa unaoendelea kutokea shambani.

Akina dada wengi wanafurahia kufanya kazi katika mradi wa ofisi ya tawi ya Angola

 Japani. Majengo ya kwanza ya ofisi ya tawi yalijengwa miaka 40 iliyopita na mengi kati ya majengo hayo hayajawahi kufanyiwa ukarabati mkubwa. Jitihada nyingi zimefanywa ili kudumisha majengo hayo, lakini licha ya jitihada hizo, majengo hayo tayari yametumiwa kwa muda mrefu na yamepita muda wake wa matumizi. Kwa sababu hiyo, mradi mkubwa wa ukarabati umeanza kushughulikiwa katika majengo hayo.

 Kwa miaka mingi pia, maisha ya Betheli yamebadilika. Kabla ya mwaka wa 2015, milo yote ilitayarishwa kwa ajili ya familia ya Betheli. Kwa sababu hiyo, vyumba vingi vya makazi katika Betheli ya Japani vilikuwa na “jiko dogo.” Lakini kwa sasa, Wanabetheli wanajitayarishia wenyewe milo mingi kati ya hiyo. Ukarabati huo umeongeza ukubwa wa eneo la jikoni kwenye vyumba vya Betheli, na hilo linawawezesha Wanabetheli kupika milo yao kwa urahisi zaidi. Kumiko, dada anayetumikia katika ofisi ya tawi ya Japani anasema hivi: “Jiko hilo linanifanya nijihisi nikiwa nyumbani, na linanisaidia kuunga mkono kikamili mipango ya Betheli.”

Majiko mapya (kulia) yanatosheleza kikamili mahitaji ya sasa ya familia ya Betheli

 Kazi ambayo inafanywa na ofisi ya tawi ya Japani ni sehemu muhimu kwa kazi ya ulimwenguni pote. (Mathayo 28:19, 20) Japani ni moja kati ya ofisi mbili tu za tawi ambazo zinachapisha Biblia nzima. Kwa hiyo, jambo moja linalofanywa wakati wa mradi wa ujenzi unaoendelea ni kuweka mifumo ya kukusanya vumbi ili kulinda afya ya wale wanaofanya kazi kwenye Kiwanda cha Uchapishaji. Kununua na kuweka mfumo huo kunagharimu karibu dola milioni moja, lakini kuwa na mfumo huo kumeisaidia ofisi ya tawi kuendelea kuchapisha na kusafirisha chakula cha kiroho.

Mfumo wa kukusanya vumbi utaboresha usalama wa afya ya wote wanaofanya kazi katika kiwanda cha uchapishaji

 Akina ndugu walihakikisha kwamba wangeendelea kuchapisha Biblia huku kazi ya ujenzi ikiendelea. Trey, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Japani anasema hivi: “Wakati wa ujenzi, tengenezo letu lilitokeza tafsiri nyingi za Biblia, na uhitaji wa kutokeza Biblia ulikuwa ukiongezeka ulimwenguni pote. Mkandarasi pamoja na idara nyingi zilihitaji kushirikiana ili kuweka vifaa vipya na wakati uleule kuhakikisha kazi ya uchapishaji inaendelea.” Licha ya changamoto hizo, karibu Biblia 220,000 zilichapishwa kila mwezi kuanzia Machi hadi Agosti 2023—wakati ambapo ujenzi ulikuwa ukiendelea kwa kasi katika kiwanda cha uchapishaji. Kazi hiyo yote ilikamilika bila gharama za ujenzi kuongezeka.

 Kupunguza matumizi ya nishati lilikuwa jambo lingine muhimu katika ukarabati huo. Vifaa vipya vya kunasa nishati ya jua vitawekwa ili kuokoa karibu dola 120,000 kila mwaka. Madirisha makubwa pia yatawekwa ili kupunguza matumizi makubwa ya nishati, na hilo litasaidia kuokoa dola 10,000 kila mwaka. Ingawa mifumo hiyo itaongeza gharama ya ukarabati wa majengo hayo, inakadiriwa kwamba mifumo hiyo itasaidia kuokoa zaidi ya dola milioni 3.5 kwa muda wote ambao vifaa hivyo vitafanya kazi katika majengo hayo. Pia, vifaa hivyo vitasaidia kupunguza athari za kimazingira ambazo zingesababishwa na majengo hayo.

Madirisha makubwa yanasaidia kupunguza kiwango cha nishati kinachotumiwa

“Bado Kuna Kazi Nyingi ya Kufanya”

 Miradi hiyo miwili ya ofisi za tawi inaonyesha jinsi ambavyo kazi kubwa inahitaji kufanywa ili kuhakikisha kwamba majengo yetu ya Betheli yanaweza kutegemeza na kutosheleza uhitaji ulio shambani. Hata hivyo, kazi bado haijaisha. Aaron anayefanya kazi katika Idara ya Usanifu Majengo na Ujenzi ya Makao Makuu anasema hivi: “Mengi yametimizwa lakini, bado kuna kazi nyingi ya kufanya.” Kazi hiyo itakamilishwa jinsi gani? Anaendelea kusema hivi: “Kwa kuongezea michango ya ukarimu ambayo inatusaidia kugharimia miradi hii muhimu, tunathamini pia roho ya utayari ya wale ambao walijitolea wakati uliopita na wale ambao wanafanya mipango ili wapatikane wakati ujao. Tunapoona ndugu na dada wakitumia nguvu na mali zao ni uthibitisho wa baraka za Yehova.”​—Zaburi 110:3.

 Miradi yote ya ujenzi na ukarabati inashughulikiwa kupitia michango ya hiari, na mingi kati ya michango hiyo hutolewa kupitia donate.pr418.com. Asante sana kwa kuendelea kutoa michango kwa ukarimu.

a Dola zinazotajwa katika makala hii ni za Marekani.