Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIKA

Usalama Katika Majumba ya Ufalme Wakati wa COVID-19

Usalama Katika Majumba ya Ufalme Wakati wa COVID-19

OKTOBA 1, 2022

 “Baraza Linaloongoza limeamua kwamba isipokuwa tu kuwe na vizuizi vya serikali, tunatia moyo makutaniko yote yaanze kufanya mikutano ya uso kwa uso kuanzia Aprili 1.” Tangazo hilo liliwekwa kwenye tovuti ya jw.org mwanzoni mwa Machi 2022 na liliwasisimua sana Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Hata hivyo, janga la COVID-19 halikuwa limeisha. a Ni marekebisho na vifaa gani vilivyohitajika ili kuwalinda wale wanaohudhuria mikutano wasiambukizwe na virusi hivyo? Kwa kuwa hatukuwa tumefanya mikutano ya uso kwa uso kwa miaka miwili, je, Majumba yetu ya Ufalme yangekuwa katika hali gani?

 Ukweli ni kwamba, ndugu zetu tayari walikuwa wameanza kufanya maandalizi ya kurudi katika Majumba ya Ufalme miezi kadhaa mapema.

Changamoto Mbalimbali Zatatuliwa

 Mwezi mmoja baada ya mikutano ya uso kwa uso kusitishwa mwaka 2020, Idara ya Ulimwenguni Pote ya Usanifu-Majengo na Ujenzi (WDC), iliyo Warwick, New York, ilianza kuchunguza jinsi janga la COVID-19 lingebadilisha utaratibu mbalimbali katika Majumba ya Ufalme na hatua zilizohitaji kuchukuliwa ili kufanya Majumba yetu yawe salama zaidi.

 Mabadiliko yaliyohitaji kufanywa yalitofautiana kutoka eneo moja hadi lingine. Matthew De Sanctis anayefanya kazi katika idara ya WDC, alisema hivi: “Katika baadhi ya nchi, changamoto ni sehemu za kunawia mikono. Majumba ya Ufalme hayana maji ya bomba au mifereji, na maji yanapatikana tu kwa kununua au kwa kuchota mtoni au kisimani. Katika nchi nyingine, serikali ziliweka sheria kuhusiana na mfumo wa kupooza hewa, mfumo wa kupitisha hewa, na alama zinazopaswa kubandikwa kuhusiana na afya na usafi.”

 Ndugu zetu walishughulikiaje changamoto hizo? Matthew anasema, “vitu vya kawaida, vyenye bei nafuu ndivyo vilivyotimiza uhitaji huo kwa njia bora zaidi” katika Majumba mengi ya Ufalme. Kwa mfano, nchini Papua New Guinea, ndoo za lita 20, zilizo na mabomba zilitumiwa kwa ajili ya kunawa mikono. Kwa njia hiyo, ndugu zetu walinunua bidhaa zilizohitajika kwa ajili ya kunawa mikono katika Majumba ya Ufalme yaliyo vijijini kwa dola 40 tu za Marekani. Zaidi ya matangi madogo 6000 yenye ubora wa hali ya juu yanayotumiwa kunawia mikono, yalinunuliwa kutoka kwa muuzaji mmoja barani Asia na kusambazwa kwenye Majumba ya Ufalme barani Afrika.

Wazazi waliwawekea watoto wao mfano mzuri ilipohusu usafi

 Marekebisho mengine yalitia ndani kuweka au kubadili feni na mifumo ya kupitisha hewa ili Majumba ya Ufalme yawe na hewa safi zaidi. Makutaniko mengi yalinunua vishikio virefu vya vikuza-sauti ili watu wasilazimike kugusa vikuza-sauti wanapotoa maelezo. Jitihada zilifanywa kusafisha kwa dawa inayoua vijidudu sehemu zinazoguswa mara kwa mara kama milango, mifereji au mabomba na pia mipango ilifanywa ili kupunguza uhitaji wa kugusa sehemu hizo. Baadhi ya makutaniko yaliweka kwenye vyoo mifereji inayotoka maji mtu anapoweka mikono yake ili kunawa. Nchini Chile, wastani wa dola 1,400 za Marekani zilitumika ili kufanya mabadiliko hayo katika kila Jumba la Ufalme.

Kikuza-sauti chenye kishikio kilitumiwa

 Ingawa lengo kuu lilikuwa kufanya Majumba ya Ufalme yawe salama, ndugu zetu pia walijitahidi sana kutumia kwa uangalifu michango ya hiari iliyotolewa. Kwa mfano, katika baadhi ya nchi, akina ndugu walitumia vizuri msamaha wa kodi kwa ajili ya matangi madogo ya kunawia mikono na pia vishikio vya vikuza-sauti. Ofisi za tawi mbalimbali zilishirikiana pamoja ili kununua bidhaa hizo kwa wingi na hivyo kuokoa pesa. Ofisi za tawi pia zilishirikiana na Idara ya Ununuzi ya Ulimwenguni Pote kununua bidhaa hizo moja kwa moja kutoka viwandani ili kupata bei ya chini zaidi na kupata bidhaa hizo mapema zaidi.

Sehemu yenye dawa ya kuua vijidudu

“Nilijihisi Nikiwa Salama”

 Marekebisho hayo yaliyofanywa katika Majumba ya Ufalme yamewafanya wengi wajihisi wakiwa salama wanapohudhuria mikutano. Dulcine, dada anayeishi Peru, anakiri kwamba alikuwa na “woga kidogo” alipojua kwamba tutarudi kwenye Majumba ya Ufalme. Alisema hivi: “Nilipata COVID-19 muda mfupi tu baada ya janga hilo kuanza, kwa hiyo nilikuwa na wasiwasi wa kwenda kwenye Jumba la Ufalme, kwa sababu niliogopa kupata virusi hivyo tena. Nilipofika kwenye Jumba la Ufalme nilitambua kwamba wazee walikuwa wamefanya mipango mingi ili kulinda usalama wetu. Kulikuwa na dawa za kuua vijidudu hasa kwa ajili ya mikono, vishikio vya vikuza-sauti, isitoshe, kulikuwa na mpango wa kusafisha Jumba kwa dawa ya kuua vijidudu kabla na baada ya mikutano. Nilijihisi nikiwa salama.” b

Kusafisha Jumba la Ufalme kwa dawa ya kuua vijidudu

 Sara, dada anayeishi Zambia, alikabiliana na changamoto tofauti. Anasema hivi: “Miezi michache iliyopita, mume wangu alikufa kutokana na COVID-19. Hivyo, nilikuwa na wasiwasi kuhusu jinsi ambavyo ningehisi iwapo ningehudhuria mikutano ya uso kwa uso kwa mara ya kwanza bila kuwa naye.” Mambo yaliendaje? Anasema: “Kuhudhuria mikutano ya uso kwa uso kumenihakikishia kwamba Yehova yupo pamoja nasi katika siku hizi za mwisho. Sasa, kuliko wakati mwingine wowote, ninahisi upendo wa pekee kupitia kitia moyo na utegemezo ninaopata kutoka kwa wazee na ndugu na dada zangu.”

Walifurahi kukutana tena uso kwa uso

 Ndugu na dada zetu ulimwenguni pote wamefurahi sana kupata fursa ya kurudi tena kwenye Majumba yao ya Ufalme. Tunashukuru sana kwa michango yenu. Michango mingi inatolewa kupitia donate.pr418.com. Michango hiyo inatusaidia kuhakikisha kwamba vituo vya ibada safi ni salama na nadhifu kwa ajili ya mikutano.

a Ilipowezekana, wale waliohitaji kuendelea kuhudhuria mikutano kupitia video au simu waliweza kufanya hivyo.

b Kwa kuongezea, wote walihimizwa kuvaa barakoa walipohudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme.