Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Viziwi Hawajasahauliwa

Viziwi Hawajasahauliwa

JULAI 1, 2022

 Yehova Mungu anataka watu wote wajifunze kumhusu na kuhusu Ufalme wake wa mbinguni, bila kujali wana hali gani maishani. (1 Timotheo 2:3, 4) Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova hutokeza Biblia na machapisho ya kujifunzia Biblia kwa ajili ya watu wengi kadiri iwezekanavyo, kutia ndani viziwi. Kwa kweli, tengenezo letu limetokeza maelfu ya video za lugha ya ishara, a ambazo zinapatikana katika zaidi ya lugha 100 za ishara! Tunatokezaje na tunasambazaje machapisho hayo? Na kadiri ambavyo muda umepita, tumeboreshaje kazi hiyo?

Video za Lugha ya Ishara Zinatayarishwaje?

 Machapisho ya lugha ya ishara yanatokezwa na vikundi vya utafsiri ulimwenguni pote. Washiriki wa kila kikundi huchunguza kwa makini chapisho wanachohitaji kutafsiri. Kisha, wanaamua njia bora ya kuwasilisha habari hiyo katika lugha ya ishara. Wanapomaliza kufanya hivyo, wanarekodi chapisho hilo katika video. Kwa sasa, vikundi 60 vinatafsiri kwa ukawaida machapisho ya kujifunzia Biblia katika lugha ya ishara, na vikundi vingine 40 vinafanya hivyo mara kwa mara.

 Hapo awali, ilikuwa gharama kubwa kutokeza video za lugha ya ishara. Kamera za video na vifaa vingine vilikuwa bei ghali sana kuliko ilivyo leo. Pia, zilirekodiwa katika studio, ambayo tulihitaji kujenga wenyewe, nyakati nyingine kwa kukarabati jengo lililokuwepo. Kwa ujumla, tulihitaji zaidi ya dola 30,000 b ili kutayarisha kila kitu kwa ajili ya kikundi kimoja cha utafsiri cha lugha ya ishara.

 Ili kutumia michango kwa njia bora zaidi, tengenezo letu limetafuta njia za kuboresha na kurahisisha kazi ya kutafsiri. Hivyo, tumetumia vifaa vya kisasa ambavyo vinafaa na ni vya gharama ya chini zaidi. Badala ya kutumia studio, vikundi vya utafsiri vinaweza kuweka kitambaa cha kijani upande wa nyuma na kurekodi video ndani ya ofisi yao. Kunapohitajika kuwa na watu kadhaa wanaorekodi kwa lugha ya ishara, ndugu na dada wanaweza kurekodi sehemu yao kwenye chapisho wakiwa ofisini au nyumbani; hawahitaji tena kwenda kwenye studio.

 Pia, tumetokeza programu za kompyuta za kuwasaidia wanaorekodi kufanya kazi yao. Njia hizo za kuboresha kazi zimepunguza kwa nusu muda ambao vikundi vya utafsiri vinahitaji kutokeza machapisho ya lugha ya ishara. Ndugu zetu wanathamini jinsi kazi hiyo ilivyoboreshwa. Ndugu anayeitwa Alexander anasema hivi: “Siku hii video za lugha ya ishara zinatolewa mara nyingi zaidi kuliko zamani. Ninafurahi sana kwa sababu ya hilo. Ninatazama video hizo kila siku.”

 Siku hizi, tunahitaji tu kiasi kisichozidi dola 5,000 kuandaa vitu vyote vinavyohitajika kwa ajili ya kikundi cha utafsiri. Kwa sababu hiyo, tunaweza kutokeza video za lugha ya ishara katika lugha nyingi zaidi.

Video za Lugha ya Ishara Zinasambazwaje?

 Kikundi cha utafsiri kinapomaliza kurekodi chapisho la lugha ya ishara, lazima video hizo ziwafikie wale wanaozihitaji. Zamani, tulitokeza kaseti za video na DVD, lakini hiyo ilikuwa gharama kubwa, ilichukua muda mwingi, na ilikuwa kazi kubwa. Rekodi hizo zilitumwa kwenye kampuni fulani ili kutokeza nakala nyingi. Hatimaye, kaseti za video na DVD zilisafirishwa hadi kwenye makutaniko. Mwaka wa 2013 tu, tulitumia zaidi ya dola 2,000,000 kutokeza DVD za lugha ya ishara.

 Viziwi walithamini sana maandalizi hayo. Hata hivyo, haikuwa rahisi sikuzote kutumia video hizo, hasa kwa kuwa idadi ya kaseti na DVD iliongezeka. Katika visa fulani, DVD kadhaa zilihitajika ili kurekodi kitabu kimoja tu cha Biblia. Ndugu nchini Brazili anayeitwa Gilnei anakumbuka hivi: “Wakati wowote tulipohitaji kusoma andiko, tulihitaji kutafuta kaseti inayofaa ya video kisha tutafute andiko hilo. Ilikuwa vigumu sana.” Dada anayeitwa Rafayane, ambaye alitumia DVD za lugha ya ishara, anasema hivi: “Ilichosha kufanya funzo la kibinafsi. Tulitumia muda mwingi kutafuta tu maandiko au marejeo.” Na ndugu na dada walipokuwa katika kazi ya kuhubiri, mara nyingi walibeba DVD au kaseti za video, ambazo wangeweza kuwaonyesha watu wanaopendezwa kwenye TV zao. Ndugu fulani hata walibeba vifaa vyao wenyewe vya kuonyeshea DVD. Hata hivyo, baada ya muda fulani, vifaa vya kuonyeshea DVD vilivyo na skrini na vinavyoweza kubebeka kwa urahisi vikaanza kupatikana, na ndugu wengi wakaanza kutumia vifaa hivyo. Bobby, anayeishi nchini Marekani, anasema hivi: “Ikiwa baada ya kuonyesha andiko moja ulitaka kuonyesha andiko lingine, mara nyingi ulihitaji kubadili DVD. Hilo lingechukua muda mwingi na lilifanya iwe vigumu zaidi kwetu kutumia Biblia katika mazungumzo yetu.”

 Mwaka wa 2013, tengenezo la Yehova lilitokeza programu ya JW Library Sign Language, inayowawezesha ndugu na dada kupakua na kuonyesha video za lugha ya ishara katika simu-janja au kwenye tablet zao. Programu hiyo ilitolewa kwanza katika Lugha ya Ishara ya Marekani. Kisha katika mwaka wa 2017, ilisasishwa ili iweze kutegemeza lugha zote za ishara. Ndugu na dada ulimwenguni walishangilia. Juscelino, ndugu nchini Brazili, anasema hivi: “Sikuamini! Niliwazia jinsi ambavyo Baraza Linaloongoza linavyotuonyesha upendo sisi viziwi na jinsi wanavyotaka tufanye maendeleo katika kweli kama tu wale wanaotumia lugha inayozungumzwa. Nilisisimka sana na programu hiyo ilinichochea kujifunza Biblia hata zaidi.”

Kutumia programu ya JW Library Sign Language

 Leo tunatokeza video zote za lugha ya ishara kidijitali na kuzisambaza kupitia tovuti yetu na pia programu ya JW Library Sign Language. Kwa sababu hiyo, inachukua siku chache tu kutafsiri, kurekodi, na kusambaza machapisho ya lugha ya ishara badala ya kuchukua miezi au miaka. Kwa kweli, katika lugha nyingi za ishara, machapisho hutolewa wakati uleule pamoja na lugha zinazozungumzwa.

 Ona baadhi ya maelezo kutoka kwa ndugu na dada zetu ambao ni viziwi. Dada anayeitwa Klízia anasema: “Ni tengenezo gani linalowajali sana viziwi hivi kwamba liko tayari kuandaa chakula cha kiroho kwa njia inayopatikana kwa urahisi hivyo? Hakuna chochote ulimwenguni kinachoweza kulinganishwa na mambo ambayo tengenezo la Yehova linatufanyia.” Vladimir anasema: “Video hizo zinanionyesha kwamba Yehova anawajali sana viziwi kama tu anavyowajali walio na uwezo wa kusikia.”

 Mara nyingi video zetu za lugha ya ishara husema maneno yafuatayo: “Chapisho hili ni sehemu ya kazi ya elimu ya Biblia ya ulimwenguni pote inayotegemezwa kwa michango ya hiari.” Tunathamini sana michango yenu. Michango mingi kati ya hiyo hupatikana kupitia tovuti ya donate.pr418.com. Michango hiyo hutusaidia kutokeza Biblia na machapisho ya kujifunzia Biblia kwa ajili ya watu wote, kutia ndani wale wanaotumia lugha ya ishara.

a Kwa kuwa lugha ya ishara huwasilisha mawazo kwa kutumia ishara za mikono na uso, machapisho ya lugha ya ishara hutolewa kwa njia ya video badala ya kupitia vitabu vilivyochapishwa.

b Makala hii inapotaja dola, inarejelea dola za Marekani.