Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

ASTER PARKER | SIMULIZI LA MAISHA

Nilitaka Kumtumikia Yehova Kikamili

Nilitaka Kumtumikia Yehova Kikamili

 Ninawashukuru sana wazazi wangu kwa sababu walinifundisha kweli tangu utotoni. Walitumia picha na hadithi zilizokuwa kwenye kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana na zilinigusa moyo sana. Nilipenda mambo niliyojifunza na hata niliwaeleza mambo hayo watoto wa jirani na pia babu yangu alipotutembelea. Wazazi wetu walidumisha ratiba nzuri ya kiroho, na kufanya hivyo kuliisaidia familia yetu kuzoea maisha mapya haraka tulipohama Asmara, Eritrea, na kwenda Addis Ababa, Ethiopia.

 Tangu nilipokuwa mdogo niliipenda kweli. Nilitamani kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Nilifikia lengo hilo na kubatizwa nikiwa na umri wa miaka 13. Nilifurahi sana. Nikiwa na umri wa miaka 14, Ndugu Helge Linck a aliniuliza ikiwa nimewahi kufikiria kuwa painia. Ninakumbuka mazungumzo hayo kana kwamba ilikuwa jana tu. Pindi kwa pindi, wazazi wangu walitumikia wakiwa mapainia wa muda (ambao sasa wanaitwa mapainia wasaidizi) hata hivyo, kwa kweli sikuelewa kuhusu upainia wa kawaida. Ndugu Linck alikuwa amepanda mbegu moyoni mwangu, swali lake liliamsha tamaa yangu ya kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova.

Mimi pamoja na mdogo wangu, Josiah

Kutayarishwa kwa Ajili ya Mateso

 Mwaka wa 1974 kulikuwa na machafuko ya kisiasa nchini Ethiopia, watu walikamatwa na wengine kuuawa. Baada ya muda, hata hatukuweza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Isitoshe, tulikutana tu katika vikundi vidogo-vidogo. Wazazi wetu waliona kwamba kuna uwezekano wa kupata upinzani zaidi kwa hiyo, wakaanza kututayarisha. Walitufundisha kanuni za Biblia zilizotusaidia kuelewa kwa nini Wakristo hawaungi mkono upande wowote wa kisiasa. Isitoshe, walituhakikishia kwamba ikiwa maofisa wa polisi wangetuhoji, Yehova angetupatia jambo la kusema. Wakati mwingine, hata hatungehitaji kujibu.​—Mathayo 10:19; 27:12, 14.

AFP PHOTO

Machafuko ya kisiasa ya mwaka wa 1974

 Nilipomaliza shule nilipata kazi kwenye shirika la ndege la Ethiopian Airlines. Siku moja, nilipoingia kazini asubuhi, wafanyakazi wenzangu walianza kunipongeza kwa sababu nilikuwa nimechaguliwa kuongoza gwaride la kuadhimisha sikukuu ya serikali. Mara moja, nilimwambia msimamizi wangu kwamba mimi ni Mkristo na siungi mkono upande wowote wa kisiasa kwa hiyo singeshiriki katika sherehe hiyo.

 Nikiwa kazini siku iliyofuata niliwaona wanaume waliobeba bunduki wakija kwenye eneo la kukagua tiketi za wateja. Nilidhani wanakuja kumkamata mtu anayejaribu kutoroka nchini. Hata hivyo, nilishtuka sana walipokuja kunikamata mimi. Kwani nilikuwa nimefanya nini? Siku ilikuwa imeanza vizuri lakini ilibadilika ghafula!

Napata Msaada Nikiwa Gerezani

 Wanajeshi hao walinipeleka kwenye ofisi fulani ambapo nilihojiwa kwa saa kadhaa. Waliniuliza kwa ukali, “Ni nani anayewalipa Mashahidi wa Yehova? Wewe unafanyia kazi Chama cha Eritrean Liberation Front? Wewe au baba yako mnafanyia kazi serikali ya Marekani?” Ingawa hali hiyo inaweza kuleta mkazo, nilikuwa mtulivu kwa sababu Yehova alinisaidia.​—Wafilipi 4:6, 7.

 Baada ya kuhojiwa, wanajeshi walinipeleka kwenye nyumba fulani iliyokuwa ikitumiwa kama gereza. Waliniweka kwenye chumba chenye ukubwa wa mita 28 za mraba. Nilikuta wanawake 15 wakiwa wamebanana katika chumba hicho kidogo. Walikuwa wamefungwa kwa sababu ya msimamo wao wa kisiasa.

Nikiwa nimeajiriwa na kampuni ya ndege

 Kwenye chumba hicho tulilala sakafuni na kwa sababu nilikuwa nimekamatwa nikiwa kazini, bado nilikuwa nimevaa mavazi rasmi ya kazi. Usiku huo, nilikuwa na mahangaiko mengi kwa sababu nilijua wazazi wangu na wadogo zangu walikuwa na wasiwasi mwingi kunihusu. Walikuwa wamepata taarifa kwamba nimekamatwa lakini hawakujua nimepelekwa wapi. Nilimsihi Yehova awasaidie kujua nilipo.

 Nilipoamka asubuhi, nilionana na kijana mmoja ambaye tulifahamiana! Alikuwa mlinzi hapo. Alishtuka sana aliponiona, akaniuliza, “Aster, unafanya nini hapa?” Nilimwomba aende nyumbani na kuwaambia wazazi wangu mahali nilipo. Siku hiyohiyo, wazazi wangu walinitumia chakula na nguo. Yule kijana alikuwa amewapa taarifa. Yehova alijibu sala yangu! Jambo hilo lilinihakikishia kwamba siko peke yangu.

 Sikuruhusiwa kuwa na Biblia au machapisho mengine. Isitoshe, familia yangu na marafiki hawakuruhusiwa kunitembelea. Hata hivyo, Yehova alinitia moyo kupitia wafungwa wenzangu. Niliwahubiria kila siku na walivutiwa na ukweli kuhusu Ufalme wa Mungu. Mara nyingi, waliniambia: “Sisi tunapigania serikali ya wanadamu tu lakini wewe unapigania serikali ya Mungu. Usilegeze msimamo wako hata wakikutishia kwamba watakuua!”

 Wakati mwingine walinzi waliwahoji wafungwa na pia waliwapiga. Siku mmoja, walikuja kwenye chumba cha gereza saa tano usiku na wakanichukua. Walinipeleka kwenye chumba cha mahojiano na wakanisingizia mashtaka mengi. Walisema kwamba mimi siungi mkono serikali. Waliniamuru nirudie baada yao maneno fulani ya kisiasa, yaani, kauli mbiu yao, na nilipokataa walinzi wawili wa kiume walinipiga. Hiyo haikuwa mara ya mwisho, hata baada ya siku hiyo, walinihoji tena na tena. Kila nilipoenda kuhojiwa nilimlilia Yehova anisaidie, naye alifanya hivyo.

 Miezi mitatu baadaye, mlinzi alikuja na kuniambia kwamba nimeachiliwa huru. Nilishangaa na nikafurahi sana, ingawa nilihuzunika kidogo kwa sababu nilikuwa nikifurahia kuwaambia wafungwa wenzangu kuhusu tumaini la Ufalme.

 Miezi michache baadaye, wanajeshi walikuja nyumbani kwetu kuwakamata watoto wote ambao walikuwa wamefikia umri wa utineja katika familia yetu. Waliwakamata dada zangu wawili na ndugu yangu mmoja lakini mimi sikukamatwa kwa sababu nilikuwa nimetoka kidogo. Nilipoona hali ilivyokuwa, niliamua ni bora zaidi kuondoka nchini. Hata hivyo, nilipofikiria kuiacha familia yangu nilijawa na huzuni moyoni lakini mama alinitia moyo niwe na nguvu na nimtumaini Yehova. Muda mfupi baadaye, nikapanda ndege na kuelekea Marekani. Jioni ya siku hiyohiyo, wanajeshi walirudi nyumbani kwetu ili kunikamata. Waliponikosa nyumbani walifululiza moja kwa moja hadi kwenye uwanja wa ndege lakini walikuwa wamechelewa kwa sababu ndege yetu tayari ilikuwa imepaa.

 Nilipowasili katika jimbo la Maryland, nilikaribishwa na Haywood Ward na mke wake, Joan, wamishonari ambao waliwafundisha wazazi wangu ukweli. Baada ya miezi mitano, nilifaulu kufikia lengo langu la kuwa painia wa kawaida. Tulifanya upainia pamoja na Cyndi, binti ya Haywood na Joan. Mimi na Cyndi tulikuwa na wakati mzuri sana katika huduma.

Nikiwa na Cyndi Ward, dada ambaye tulifanya upainia pamoja

Kumtumikia Mungu Kikamili Betheli

Nikiwa na mume wangu kwenye Betheli ya Wallkill, New York

 Katikati ya mwaka wa 1979, nilitembelea Betheli jijini New York, na hapo nikakutana na Wesley Parker. Alikuwa na sifa nzuri na alikuwa amejiwekea miradi ya kiroho. Mambo hayo yalinivutia sana. Tulifunga ndoa mwaka wa 1981 kisha nikahamia Wallkill, New York, ili kujiunga na Wesley katika utumishi wa Betheli. Nilifanya kazi katika Idara ya Usafi na Idara ya Dobi na baadaye nilifanya kazi na kikundi cha MEPS kwenye Idara ya Kompyuta. Kutumikia Betheli kulinipatia nafasi ya kujitoa kikamili katika utumishi wa Yehova na pia fursa ya kuwafahamu ndugu na dada ambao wamekuwa marafiki wetu mpaka sasa.

 Hata hivyo, nilikuwa na huzuni kwa sababu familia yetu huko Ethiopia ilikuwa ikikabili mateso makali. Bado dada zangu wawili na ndugu yangu walikuwa gerezani. b Kila siku mama yangu alihitaji kutayarisha chakula na kuwapelekea kwa sababu huko gerezani wafungwa hawakuandaliwa chakula.

 Ingawa nilikuwa na mkazo katika kipindi hicho Yehova alikuwa kimbilio langu na familia ya Betheli ilinifariji na kunitegemeza. (Marko 10:29, 30) Siku moja, Ndugu John Booth aliniambia: “Tunafurahi sana kuwa na wewe hapa Betheli. Usingeweza kutumikia hapa bila baraka za Yehova.” c Maneno yake ya fadhili yalinihakikishia kwamba Yehova alikuwa amebariki uamuzi wangu wa kuondoka Ethiopia na angeitunza familia yetu.

Kumtumikia Yehova Tukiwa Familia

 Januari 1989, tuligundua kwamba nilikuwa mjamzito. Mwanzoni, tulishtuka sana! Hata hivyo, siku chache baadaye wasiwasi wetu ulipungua tukaanza kuwa na furaha lakini bado tulikuwa na maswali mengi. Je, tutafaulu kuwa wazazi wazuri? Tutaishi wapi? Baada ya kuondoka Betheli tutafanya kazi gani ili kuiruzuku familia yetu?

 Aprili 15, 1989, tuliweka vitu vyetu kwenye gari kisha tukaelekea Oregon. Tulikuwa tumepanga kuishi huko na kuwa mapainia wa kawaida. Muda mfupi baada ya kuwasili kwenye eneo hilo, marafiki wenye nia nzuri walituambia kwamba hali zetu hazikuturuhusu kufanya upainia. Ni kweli kwamba tulikuwa na vitu vichache vya kimwili na pia tulikuwa tukitarajia kupata mtoto. Sasa tulihitaji kufanya uamuzi. Pindi hiyohiyo, tulikuwa na ziara ya mwangalizi wa mzunguko, Guy Pierce, na mke wake, Penny. d Walitutia moyo kuendelea na mipango yetu. Kwa hiyo, tulianza upainia tukiwa na uhakika kwamba Yehova atatutunza. (Malaki 3:10) Mtoto wetu wa kwanza, Lemuel alipozaliwa bado tuliendelea na upainia, na hata mtoto wetu wa pili, Jadon alipozaliwa, hatukuacha kufanya upainia.

 Tulithamini sana pendeleo ambalo tulipata la kufanya upainia watoto wetu wakiwa bado wadogo. Kazi ya upainia ilitokeza fursa nyingi za kuwafafanulia kweli za Biblia si majirani wetu tu bali pia wana wetu. (Kumbukumbu la Torati 11:19) Hata hivyo, Japheth, mwana wetu wa tatu alipozaliwa, tulilazimika kuacha upainia kwa muda.​—Mika 6:8.

Tuliwazoeza Wana Wetu Kumtumikia Yehova

 Tulitambua kwamba jukumu letu kubwa zaidi tukiwa wazazi ni kuwasaidia watoto wetu kumwona Yehova akiwa halisi na pia kuwasaidia kusitawisha urafiki wa kibinafsi pamoja naye. Ili kufikia lengo hilo, tulijaribu kufanya ibada yetu ya familia iwe yenye kufurahisha. Walipokuwa na umri mdogo sana, tuliwasomea Kitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Hata tuliigiza baadhi ya hadithi tulizosoma. Kwa kuwa mimi ndiye niliyekuwa mwanamke pekee katika familia yetu, tulipoigiza hadithi ya Yezebeli, basi mimi nilikuwa Yezebeli. Wanangu walipenda kuigiza kana kwamba wanamsukuma Yezebeli kutoka kwenye kiti na kisha wangeigiza kama mbwa waliomla Yezebeli. Mbali na ibada yetu ya familia, Wesley alijifunza kibinafsi na kila mtoto.

 Tuliwapenda na kuwatunza watoto wetu, na tulimwomba Yehova aisaidie familia yetu iwe na umoja na ukaribu. Walipoendelea kukua tuliwafundisha kazi za nyumbani. Waliosha vyombo, walisafisha vyumba vyao, walifua nguo zao, na hata walijifunza kupika.

 Hata hivyo, si watoto wetu tu waliojifunza mambo, hata sisi wazazi tulijifunza mambo mengi. Wakati mwingine, hatukushughulikia hali vizuri na tulisema maneno yasiyo ya fadhili. Ikiwa tulikuwa tumewakosea watoto wetu tuliwaomba msamaha na ikiwa tulikuwa tumekoseana sisi wenyewe tuliombana msamaha. Kuomba msamaha kulihitaji unyenyekevu.

 Mara nyingi tuliwaalika nyumbani ndugu na dada kutoka kutanikoni, bila kusahau Wanabetheli waliotembelea kutaniko letu, wamishonari, waangalizi wa mzunguko, na wale waliokuwa wakitumikia katika maeneo yenye uhitaji. (Waroma 12:13) Tulipokuwa na wageni hatukuwaambia watoto wetu waende kucheza kwenye chumba kingine. Tulikaa pamoja nao na wao pia walifurahia kushiriki katika mazungumzo na kusikiliza masimulizi. Mara nyingi, watoto wetu ndio waliokumbuka mambo mengi zaidi kuhusu mazungumzo hayo kuliko sisi.

 Mimi na Wesley tulijitahidi sana kufanya watoto wetu wafurahie kumtumikia Yehova. Kwa mfano, tulifanya mipango mapema ili tuweze kusafiri nchi mbalimbali. Tulihitaji kuweka pesa kidogo-kidogo na kuhifadhi siku za likizo. Tulipoenda nchi fulani, tulitembelea ofisi ya tawi, tukahudhuria mikutano, na kushiriki katika huduma. Mambo hayo yalitusaidia kulithamini sana tengenezo la Yehova la ulimwenguni pote, na pia familia yetu ikawa na ukaribu zaidi.

Familia yetu ilipotembelea makao makuu Brooklyn, New York, mwaka wa 2013

Kuendelea Kumtumikia Yehova Kikamili

 Tuliona kwamba kulikuwa na watu wengi katika eneo letu waliozungumza Kihispania, lakini hawakuwa wakihubiriwa kwa ukawaida. Ingawa watoto wetu walikuwa bado wadogo, tulimuuliza Ndugu Pierce maoni yake kuhusu wazo la kuhamia kutaniko la Kihispania. Alitabasamu, akatuambia, “Mvuvi huenda mahali samaki walipo.” Maneno hayo yalitutia moyo, tukaamua kuhamia kutaniko la Kihispania la Woodburn, Oregon. Ilikuwa shangwe kubwa kuona baadhi ya wanafunzi wetu wa Biblia wakifanya maendeleo na kubatizwa. Isitoshe, tuliona kikundi kidogo cha Kihispania kikipanuka na kuwa kutaniko.

 Pindi fulani, Wesley alipoteza kazi. Alipata kazi mpya katika jimbo la California na tulilazimika kuhamia huko. Miaka miwili baadaye, mimi, Lemuel, na Jadon tulianza upainia. Katika mwaka wa 2007, sote tulihudhuria Shule ya Utumishi wa Painia. Nilifurahia sana kuhudhuria shule hiyo pamoja na wanangu. Baada tu ya shule hiyo, tuligundua kwamba katika eneo letu kulikuwa na watu wengi wanaozungumza Kiarabu. Tuliamua kujiunga na kutaniko la Kiarabu baada ya kutumikia katika makutaniko ya Kihispania kwa miaka 13. Tumefurahia kuwahubiria wageni wengi wanaoishi katika eneo letu ambao wanazungumza Kiarabu. Isitoshe, tumeshiriki katika kampeni za pekee za kuhubiri katika nchi nyingine. Kwa sasa, bado tunaendelea kufanya upainia na kuwahubiria watu wanaozungumza Kiarabu katika eneo la San Diego, California.

 Wesley ni mume mzuri sana na anatimiza jukumu lake akiwa kichwa cha familia kwa njia nzuri. Anaheshimu sana tengenezo la Yehova. Wesley hawajahi kukosoa mipango ya Betheli au ya kutaniko. Badala yake, sikuzote yeye hujitahidi kusema mambo yanayojenga. Tunasali pamoja na pia yeye husali kwa ajili yangu. Sala zake zimenifariji na kunisaidia hasa katika pindi ambazo tumekabili hali ngumu.

 Ninapofikiria maisha yangu, ninaona jinsi ambavyo tumefurahia utumishi wa wakati wote, kulea watoto, na kutumikia katika makutaniko yenye uhitaji mkubwa. Tumejionea jinsi Yehova anavyowabariki wale wanaomtanguliza maishani na hatujawahi kukosa mahitaji yetu. (Zaburi 37:25) Ninaamini kwamba uamuzi niliofanya wa kumtumikia Yehova kikamili ndio uamuzi bora zaidi niliowahi kufanya.​—Zaburi 84:10.

Pamoja nami, kuanzia kushoto: Japheth, Lemuel, Jadon, na Wesley

a Ndugu Linck alitumikia kwenye ofisi ya tawi ya Kenya iliyosimamia kazi ya kuhubiri nchini Ethiopia.

b Dada zangu wawili na ndugu yangu waliachiliwa huru baada ya kukaa miaka minne gerezani.

c Ndugu Booth alikuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza hadi alipomaliza mwendo wake wa kidunia mwaka wa 1996.

d Ndugu Pierce alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza na alitumikia hadi alipomaliza mwendo wake wa kidunia mwaka wa 2014.