Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

DAVID MAZA | SIMULIZI LA MAISHA

Familia Yenye Furaha Yatikiswa na Kuwa Imara Tena

Familia Yenye Furaha Yatikiswa na Kuwa Imara Tena

Baada ya kujifunza Biblia na kutumia kanuni zake maishani mwangu nilipata kitu ambacho nilidhani hakiwezi kupatikana, yaani, familia yenye furaha. Mimi na mke wangu pamoja na watoto wetu watatu tulikuwa tunamtumikia Yehova kwa umoja na kwa moyo wote.

Aprili 24, 2004, familia yetu ilipatwa na msiba ambao hatukutarajia na maisha yetu yakabadilika kabisa.

 Mimi na mke wangu Kaye tulipompata mtoto wetu wa kwanza Lauren, sikujua nilichopaswa kufanya ili kuwa baba mzuri. Tulipompata mtoto wetu wa pili, Michael, bado hali ilikuwa ileile. Tangu nilipokuwa mdogo wazazi wangu walipigana sana na hatimaye walitalikiana. Ingawa nilitaka kuiongoza familia yangu vizuri, sikujua jinsi ya kufanya hivyo.

 Hali ilikuwa mbaya hata zaidi kwa sababu nilikuwa mraibu wa pombe na dawa za kulevya tangu nilipokuwa tineja. Sasa nilikuwa mtu mzima lakini bado maisha yangu hayakuwa na mwelekeo. Kufikia wakati huo, nilikuwa mraibu wa kucheza kamari pia na hivyo nikafanya maamuzi mengi mabaya. Mambo yakawa mabaya hata zaidi hivi kwamba Kaye akaniacha na kwenda na watoto wetu wawili. Nilivunjika moyo sana.

 Nilimuuliza Kaye nilichopaswa kufanya ili arudi nyumbani. Kwa kuwa alikuwa ameanza kujifunza Biblia na Gloria ambaye ni Shahidi wa Yehova, alinipa jibu rahisi: “Jifunze Biblia.” Sikujua yote yaliyohusika, lakini nilitaka Kaye arudi nyumbani, basi nikakubali kukutana na Gloria pamoja na mume wake, Bill.

Mazungumzo Yaliyobadili Maisha Yetu

 Bill na Gloria walipokuja nyumbani kwetu, nilivutiwa na uhusiano wao wa karibu. Nilipata kujua kwamba watoto wao walikuwa watu wazima wa umri wangu hivi na mambo waliyotanguliza maishani mwao yalikuwa mazuri na yenye kuridhisha. Kwa mara ya kwanza maishani mwangu nikaanza kufikiria kwamba huenda Biblia ndiyo siri ya kuwa na familia yenye furaha.

 Bill na Gloria walipotutembelea siku hiyo walinisaidia kuchanganua matatizo yangu. Walinionyesha andiko la Wagalatia 6:7 linalosema: “Lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.” Nikajiambia, ‘Ikiwa ningetumia kanuni hiyo kufanya maamuzi, kufikia sasa ningekuwa nimeepuka matatizo mengi sana!’

Kaye na David

 Kadiri muda ulivyopita nilitambua kwamba kutumia kanuni za Biblia kuliboresha maisha yangu sana. Mimi na Kaye tuliacha kuvuta sigara na kupitia msaada niliopata nilifaulu kuacha mazoea mengine mabaya. Mwaka wa 1985, David, mtoto wetu wa tatu alizaliwa, na kwa sababu tulimpenda sana nyumbani tulimwita Davey. Pindi hii nilihisi kwamba nina uwezo wa kuwa baba mzuri.

Kumtumikia Yehova kwa Umoja

 Mimi na Kaye tulitambua kwamba tulipofanya kazi yetu tukiwa wazazi, yaani, kuwafundisha watoto wetu kumhusu Yehova, sisi pia tulihisi tukiwa karibu na Yehova. Tulijifunza mambo mengi kutoka kwenye machapisho kama vile Kumsikiliza Mwalimu Mkuu! Isitoshe, familia mbalimbali katika kutaniko letu zilituwekea mfano mzuri sisi na watoto wetu.

Michael na mke wake, Diana

 Baada ya muda, watoto wetu wote walianza upainia. Kufikia mwanzoni mwa mwaka wa 2004, Lauren alikuwa akitumikia kwenye kutaniko la Kihispania. Wakati huo Michael naye alikuwa ameondoka Betheli ili kufunga ndoa. Baada tu ya kufunga ndoa, yeye na mke wake Diana walianza kufanya matayarisho ya kusafiri kwenda Guam ili kuanza mgawo wao wa kuhubiri huko. Kipindi hicho Davey, akiwa na umri wa miaka 19, alikuwa ameanza kutumikia katika Jamhuri ya Dominika.

 Mimi na Kaye tulijivunia watoto wetu kwa sababu walikuwa wamefanya maamuzi mazuri maishani. Tulipata shangwe ambayo inafafanuliwa kwenye 3 Yohana 4: “Sina shangwe kubwa kuliko hii: kwamba nisikie watoto wangu wanaendelea kutembea katika kweli.” Hatukuwahi kufikiri kwamba maisha yetu yangebadilika ghafla, baada ya kupigiwa simu tu.

Msiba Uliotuvunja Moyo

 Aprili 24, 2004, tulienda kula chakula cha jioni tukiwa na wenzi wanne wa ndoa. Tulisafiri kwa kutumia gari langu kwenda huko kwa sababu mkahawa ulikuwa umbali wa kilomita 100 hivi kutoka eneo tuliloishi. Tulienda kwenye mkahawa tofauti kwa ajili ya kitinda-mlo, na baada ya kuwasili niliwashusha wengine kisha nikaenda kutafuta eneo la maegesho. Simu yangu iliita. Ndugu mmoja alikuwa akinipigia na alisikika amelemewa na mkazo.

 Alisema: “Kuna jambo baya ambalo limetukia. Davey amepatwa na aksidenti.”

 Nilimuuliza: “Ameumia sana?” Hata hivyo, niliogopa kupata jibu.

 Mwanzoni alishindwa kuniambia. Mwishowe, alikusanya nguvu na kuniambia kwamba Davey amekufa.

 Alipokata simu nilisali kwa Yehova ili anipe nguvu. Kisha nikarudi kwenye mkahawa nikawaambia wengine sikuwa nikihisi vizuri na nikawaomba turudi nyumbani. Sikutaka kumpa Kaye habari kuhusu Davey mbele za watu, nilitaka kusubiri tufike nyumbani nimwambie tukiwa peke yetu.

 Katika safari hiyo ya dakika 90 ya kurudi nyumbani, nilihisi uchungu mwingi moyoni. Nilimsikia Kaye akisema kwamba alikuwa akisubiri kwa hamu Davey atutembelee hivi karibuni. Wakati huohuo, watu wengi waliosikia kuhusu kifo cha Davey walikuwa wakinitumia ujumbe kwenye simu yangu, ingawa Kaye hakuwa amejua kwamba mwana wetu alikuwa amekufa.

 Baada ya kuwapeleka wengine nyumbani kwao tulirudi nyumbani pia. Kaye aliponitazama tu alijua kwamba kuna tatizo kubwa. Akaniuliza: “Ni nini kimetukia?” Kama tu nilivyovunjika moyo kwa sababu ya simu niliyopigiwa saa mbili mapema, nilijua yeye pia atavunjika moyo sana nitakapompa habari hiyo.

Kukabiliana na Huzuni Yetu

 Kabla ya hapo, mimi na Kaye tulikuwa tumepata changamoto mbalimbali na tulijua kwamba Yehova huwategemeza watu wake. (Isaya 41:10, 13) Lakini hili lilikuwa jaribu tofauti sana. Mara nyingi nilijiuliza, ‘Kwa nini Davey alikufa? Davey alikuwa amejitolea sana kumtumikia Yehova. Kwa nini Yehova hakumlinda?’

 Watoto wetu wengine pia walikuwa na huzuni sana. Lauren alimpenda sana Davey ni kana kwamba alikuwa mama yake wa pili, basi, kifo chake kilimuumiza sana. Michael pia, aliumia sana. Ingawa Michael alikuwa ameishi mbali na nyumbani kwa miaka mitano hivi alifurahi sana kuona ndugu yake mdogo alikuwa amekomaa na kuwa kijana mwenye kuheshimika.

 Mara tu baada ya kupata habari kwamba tumefiwa, ndugu na dada kutanikoni walitusaidia sana. Kwa mfano, hata Kaye alipokuwa akikabiliana na mshtuko wa kwanza baada ya kupata habari hiyo, ndugu na dada walifika nyumbani ili kutufariji na kutusaidia. (Methali 17:17) Sitasahau kamwe upendo ambao walituonyesha!

 Ili kukabiliana na huzuni tuliyokuwa nayo, mimi na Kaye tulijitahidi kushikamana na ratiba yetu iliyotia ndani kusali, kujifunza Biblia, na kuhudhuria mikutano yetu. Kufanya hivyo hakukuondoa maumivu yetu. Lakini tulijua kwamba ilikuwa muhimu kuendelea kufanya mambo ambayo yangetusaidia kubaki imara kiroho.​—Wafilipi 3:16

Lauren na mume wake, Justin

 Katika kipindi hicho, Michael na Diana walihamia karibu na kwetu, na Lauren akarudi tena katika kutaniko letu la Kiingereza. Tulifaulu kukabiliana na hali hiyo kwa sababu ya kuwa pamoja kwa miaka kadhaa iliyofuata. Baadaye Lauren aliolewa na Justin. Justin amekuwa msaada mkubwa kwetu.

Davey alipokuwa akitumikia katika Jamhuri ya Dominika

Safari Ngumu

 Muda mfupi baada ya kifo cha Davey, tulipanga safari iliyokuwa ngumu sana lakini hatimaye ilitusaidia kukabiliana na huzuni yetu. Kaye atasimulia ilivyokuwa.

 “Mume wangu aliponiambia kwamba Davey amekufa nilikata tamaa sana, nilihuzunika sana, na hali hiyo iliendelea kwa muda mrefu. Nililemewa sana na huzuni hivi kwamba nilishindwa kufanya shughuli zangu za kila siku. Nililia sana. Kusema kweli, wakati mwingine nilimkasirikia Yehova na nilikuwa na uchungu kuwaelekea wengine waliokuwa hai. Nilihisi nikiwa nimechanganyikiwa.

 “Nilitamani kwenda Jamhuri ya Dominika. Nilitaka kuwa mahali ambapo Davey aliishi na kumtumikia Yehova miezi michache kabla ya kifo chake. Lakini pia nilihisi sikuwa na nguvu, na nisingefaulu kwenda huko.

 “Rafiki mmoja wa karibu aliniambia kwamba rafiki za Davey waliokuwa katika Jamhuri ya Dominika walikuwa wakiomboleza pia na walitamani sana kukutana na familia yake. Maneno yake yalinitia moyo hivi kwamba nikapata nguvu za kupanda ndege.

 “Tulihisi kwamba safari hiyo iliisaidia sana familia yetu. Ilitusaidia kutambua kwamba Davey aliona kumtumikia Yehova kuwa jambo muhimu sana kwake. Kutaniko alilokuwa Davey lilikuwa na mzee mmoja na alisema kwamba Davey alikuwa mwenye kutegemeka na sikuzote alitimiza migawo yake.

 “Tulipokuwa kwenye mtaa ambao Davey alikuwa akiishi, watu wengi walitusimulia mambo mazuri ambayo Davey alikuwa amewafanyia. Nilijua kwamba mwanangu alikuwa mtu mwenye fadhili, lakini mambo tuliyosikia, yalinisaidia kutambua jinsi alivyojitahidi kufuata kwa ukaribu hatua za Yesu.

 “Pia, tulifaulu kumtembelea mmoja kati ya watu ambao walijifunza Biblia na Davey. Mwanamume huyo alikuwa akiishi kwenye nyumba ndogo sana na hangeweza kutoka kitandani kwa sababu ya ugonjwa. Ingawa mwanamume huyo alikuwa maskini sana, ndugu na dada kutanikoni walituambia kwamba Davey alimtendea kwa heshima sana. Jambo hilo lilifanya nijivunie Davey sana!

 “Sijawahi kuwa na safari ngumu kama hiyo. Hata hivyo, kuomboleza pamoja na watu waliomjua Davey kulitusaidia tukiwa familia kukabiliana na huzuni yetu na kupata faraja. Tulihisi vizuri zaidi.”

Waliotiwa Moyo na Simulizi la Davey

 Gazeti la Amkeni! la Januari 8, 2005, lilikuwa na makala iliyozungumzia kifo cha Davey na utumishi wake katika Jamhuri ya Dominika. Ilipoandikwa, familia yetu haikujua kwamba makala hiyo ingewasaidia sana wengine. Kwa mfano, Mei 2019, ndugu anayeitwa Nick aliwasiliana nasi na kutuambia hivi:

 “Mwishoni mwa mwaka wa 2004, nilikuwa katika chuo cha ufundi na sikuwa na miradi ya kiroho. Sikuwa na furaha. Nilisali kwa Yehova nikamwomba anisaidie kutumia ujana wangu kwa njia nzuri. Muda mfupi baadaye nilisoma simulizi la Davey katika Amkeni! Simulizi hilo lilikuwa jibu la sala yangu!

 “Niliacha chuo na nikaanza kufanya upainia. Vilevile nilijiwekea lengo la kujifunza Kihispania na kuhamia nchi nyingine. Baada ya muda, nilitumikia nchini Nikaragua na nikahudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme pamoja na mke wangu. Watu wanaponiuliza kuhusu jambo lililonichochea kuwa painia, mimi huwaeleza kuhusu simulizi la Davey.”

 Tulipata jambo lingine lenye kutia moyo tulipokutana na dada anayeitwa Abi. Tulipangiwa hoteli moja tulipokuwa wajumbe katika Kusanyiko la Kimataifa lililofanyika jijini Buenos Aires, Argentina. Abi alikuwa mwenye fadhili sana na mwenye upendo. Mimi na Kaye tulihisi kwamba utu wake ulifanana sana utu wa Davey.

Simulizi la Davey lilimchochea Abi kuanza utumishi wa wakati wote na kuhamia eneo la mbali

 Tuliporudi kwenye chumba chetu hotelini, tulimtumia Abi kiunganishi cha makala ya Amkeni! yenye simulizi la Davey. Baada ya dakika chache alijibu ujumbe wetu. Alitaka sana kuzungumza nasi basi tukakutana naye kwenye sehemu ya mapokezi hotelini. Huku akilia, Abi alitueleza kwamba simulizi la Davey ndilo lililomchochea kuanza upainia mnamo Septemba 2011, na kutumikia katika eneo la mbali. Alisema pia, “Ninapokabili changamoto kwenye mgawo wangu, ninasoma tena makala hiyo.” Hata alikuwa amebeba nakala ya gazeti hilo!

 Mambo kama hayo yanaonyesha kwamba sisi ni sehemu ya familia ya ulimwenguni pote. Hakuna watu wowote ulimwenguni walio na umoja kama wa watu wa Yehova!

 Mimi na Kaye tunafarijika sana kwa kujua kwamba mfano mzuri wa Davey umewanufaisha wengine. Vijana wetu wapendwa wanaomtumikia Yehova kwa bidii wanawanufaisha wengine pia. Huenda hata bila kujua wanagusa maisha ya watu wanaoiona bidii yao, na mfano wao mzuri unawachochea wengine wamtumikie Yehova kadiri ya uwezo wao.

“Kwake, Wote Wako Hai”

 Kwenye Luka 20:37 Yesu anataja maneno ya Yehova. Yehova alisema Yeye ni: “Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.” Yehova hakusema kwamba alikuwa Mungu wao walipokuwa hai lakini anasema kwamba bado yeye ni Mungu wao! Kwa nini? Yesu anatoa jibu kwenye mstari wa 38: “Kwa maana kwake, wote wako hai.”

 Ndiyo, kwa maoni ya Yehova, watumishi wake wote waaminifu wako hai; hilo linaonyesha kwamba ameazimia kuwafufua! (Ayubu 14:15; Yohana 5:28, 29) Nina uhakika kwamba Yehova anahisi hivyo pia kumhusu Davey, na watumishi wake wengine ambao wamelala katika kifo.

 Ninatamani sana kumwona tena Davey, lakini ninatamani hata zaidi kumwona Kaye akimkaribisha Davey katika ulimwengu mpya. Sijawahi kumwona mtu akiwa na uchungu kama wa Kaye. Maneno ya Luka 7:15 yananigusa moyo sana: “Yule mfu akaketi akaanza kuongea, naye Yesu akamkabidhi kwa mama yake.”

 Septemba 2005, nilijiunga na Kaye katika kazi ya upainia. Ni pendeleo kubwa sana kutumikia nikiwa painia pamoja na mke wangu, watoto wetu, na wenzi wao pia. Familia yetu inatenda kwa umoja, na tunategemezana huku tukiendelea kukazia fikira tumaini letu la wakati ujao katika ulimwengu mpya, ambapo tutaungana tena na mpendwa wetu, Davey.