Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

IRMA BENTIVOGLI | SIMULIZI LA MAISHA

Kumtumikia Mpaji wa “Kila Zawadi Njema”

Kumtumikia Mpaji wa “Kila Zawadi Njema”

 Ving’ora vililia kwa sauti kutoa onyo kwamba ndege za kivita zilikuwa zinakaribia kuangusha mabomu. Mama yangu alikimbia huku akiwa amembeba ndugu yangu mdogo na kutupeleka tujifiche chini ya miti. Nilikuwa na umri wa miaka sita tu.

 Shambulizi hilo lilipokwisha, mimi na mama tulienda kumtafuta rafiki yake wa karibu sana. Tulihuzunika sana tulipotambua alikufa wakati wa shambulizi hilo. Shambulizi lililofuata lilikuja siku chache tu baadaye. Pindi hii baba alininyanyua na kunibeba kwenye baiskeli yake upesi, tukaenda mbali sana kutoka jijini.

 Vita vya Pili vya Ulimwengu vilisababisha uharibifu mkubwa sana nchini Italia, nami bado ninakumbuka matukio hayo. Lakini jambo ambalo liliathiri maisha yangu kwa njia kubwa ni kwamba tangu utotoni nimezungukwa na watu wanaomjua na kumpenda Yehova kwa kina.

Zawadi ya Kweli

 Wakati wa majira ya baridi kali ya mwaka wa 1936, baba yangu alifanya kazi kwenye shirika la reli pamoja na mwanamume aliyeitwa Vincenzo Artusi. Hiyo ilikuwa miezi michache kabla ya mimi kuzaliwa. Vincenzo hakuwa Shahidi aliyebatizwa wakati huo, lakini alipenda sana kweli ya Biblia. Walipokuwa wakiondoa theluji kutoka kwenye reli, Vincenzo alimwambia baba yangu mambo ambayo alikuwa akijifunza.

 Mara moja baba yangu alitambua kwamba mambo ambayo alikuwa akisikia yalikuwa kweli. Yeye na watu wengine katika mji wetu wa Faenza walitaka kujifunza mengi zaidi. Siku hizo, mateso ya Wafashisti yalipokuwa yakiendelea, Mashahidi hawakufanya mikutano ya umma na mtu angeweza kukamatwa kwa sababu ya kuwa na machapisho ya Biblia. Baadhi ya Mashahidi walikuwa wamefungwa gerezani. Kwa hiyo, baba yangu na rafiki zake walikutana katika nyumba zilizokuwa mbali kijijini ili kusoma Biblia na kujifunza machapisho waliyokuwa nayo. Pia, kila juma baba yangu angeikusanya familia yetu jioni kwa ajili ya funzo la Biblia.

Zawadi ya Vielelezo Vizuri

 Mwaka wa 1943, wengi kati ya Mashahidi waliokuwa wamefungwa kwa sababu ya utendaji wao wa kidini waliachiliwa. Miongoni mwao kulikuwa na dada mseja, Maria Pizzato. Alipokuwa njiani kurudi nyumbani kwao huko Italia kaskazini, Maria alilala kwetu usiku mmoja. Alikuwa ametimiza jukumu muhimu la kuwasaidia Mashahidi kupokea machapisho na kudumisha mawasiliano na ofisi ya tawi ya Uswisi, ambayo wakati huo ilikuwa ikisimamia kazi nchini Italia. Licha ya kwamba alionekana dhaifu, Maria alikuwa mwanamke mwenye nguvu na jasiri. Baada ya vita, mara kwa mara alikuja Faenza, na sikuzote tulifurahi sana kuwa pamoja naye.

 Dada mwingine ambaye ninamkumbuka sana ni Albina Cuminetti. Nilipokuwa tineja, mjane huyo mwenye umri mkubwa aliishi katika jengo ambalo tulifanyia mikutano yetu. Alikuwa kolpota (mweneza-injili wa wakati wote) nchini Italia kuanzia miaka ya mapema ya 1920. Albina aliniambia hadithi nyingi zenye kusisimua kuhusu jinsi kazi ilivyoendeshwa katika miaka hiyo ya mapema!

 Albina alikuwa na mkusanyo wa machapisho yetu na vitu vingine vya kihistoria. Siku moja niliona pini iliyokuwa na msalaba na taji ambayo zamani ilivaliwa na Wanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo). Nilishtuka na nikacheka huku nikiwa na wasiwasi mwingi kwa kuwa nilijua msalaba ulikuwa na chanzo cha kipagani. Kisha Albina akasema jambo ambalo sijawahi kusahau. Akitaja maneno ya Zekaria 4:10, alisema hivi: “Usidharau siku ya mambo madogo!”

Nilipokuwa na umri wa miaka 14

 Maneno hayo yalinifundisha somo muhimu sana. Hata ingawa Wanafunzi wa Biblia wa mapema hawakuielewa kweli kikamili, nilipaswa kuwaheshimu. Pia, kwa kuwa machapisho yote hayakupatikana katika Kiitalia, ilichukua muda kwa baadhi ya akina ndugu kujipatanisha na uelewaji uliorekebishwa. Isitoshe, Yehova alithamini jitihada zao, nami ninapaswa kuzithamini pia.

 Licha ya kwamba Albina alinizidi umri sana, nilipenda kuzungumza naye. Yeye, Maria, na dada wengine wenye bidii ambao walimtumikia Yehova kwa uaminifu licha ya changamoto nyingi sana, walikuwa vielelezo ambavyo nilitaka kuiga. Ninashukuru sana fursa nilizopata za kushirikiana nao.

Zawadi ya Utumishi wa Betheli

 Wakati wa kiangazi cha mwaka wa 1955, nilisafiri kwenda Rome ili kuhudhuria Kusanyiko la “Ufalme Wenye Ushindi.” Wakati huo, nilitembelea Betheli pamoja na wajumbe kutoka nchi mbalimbali. Nilijiambia, ‘Ningefurahi ikiwa ningepata nafasi ya kutumikia hapa!’

 Desemba 18, 1955, nilibatizwa. Bado nilikuwa shuleni, lakini nilikuwa nimeazimia kuingia katika utumishi wa wakati wote. Mwaka wa 1956, kwenye kusanyiko katika jiji la Genoa, nilisikia tangazo kwamba wajitoleaji walihitajika Betheli. Hata hivyo, mwakilishi wa ofisi ya tawi alisema kwamba akina dada hawakuhitajika Betheli.

 Baadaye, nilizungumza na mwangalizi wetu wa mzunguko, Piero Gatti, a kuhusu miradi yangu. Mweneza-injili huyo mwenye msisimuko na mwenye bidii akaniambia, “Nitakupendekeza kwa ajili ya utumishi wa upainia wa pekee.”

 Baada ya muda, barua ilikuja kutoka ofisi ya tawi. Nilikuwa na uhakika kwamba nimepata mgawo wa kuwa painia, lakini haikuwa hivyo. Nilikuwa nimealikwa kutuma ombi la utumishi wa Betheli!

Nikiwa Betheli na mtafsiri mwenzangu Ilaria Castiglioni (aliyesimama), mwaka wa 1959

 Niliwasili Betheli Januari 1958. Wakati huo familia ya Betheli ilikuwa na watu wasiozidi 12. Nilipewa mgawo wa kuwasaidia watafsiri wawili waliokuwa kwenye ofisi ya tawi. Kulikuwa na kazi nyingi, nami sikuwa na uzoefu wowote wa kutafsiri. Lakini kwa msaada wa Yehova, nilikuja kuupenda mgawo wangu.

 Hata hivyo, kabla ya miaka miwili kwisha, kazi ya kutafsiri ilipangwa upya nami nikapewa mgawo wa kwenda shambani nikiwa painia. Nilishtuka kwa sababu kufikia wakati huo nilikuwa nimefanya Betheli kuwa makao yangu. Hata hivyo, kadiri muda ulivyopita, nikaja kuuona mgawo wangu mpya kuwa zawadi nyingine kutoka kwa Yehova.

Zawadi ya Waandamani wa Kuhubiri Wenye Bidii

 Septemba 1, 1959, nilianza upainia wa pekee katika jiji la Cremona. Painia mwenzangu alikuwa Doris Meyer, ambaye alihamia huko kutoka Denmark. Alinizidi umri kwa miaka michache tu, lakini alikuwa painia mwenye uzoefu, nami nilimheshimu. Doris alikuwa jasiri, hakuogopeshwa kwa urahisi, naye alikuwa na bidii. Tulihitaji kuwa na sifa hizo ili kuhubiri eneo hilo, kwa sababu sisi tu ndio tuliokuwa Mashahidi katika jiji lote.

Nilijifunza mengi kutoka kwa Doris (kushoto) na Brunilde (kulia), waliokuwa mapainia wenzangu huko Cremona

 Doris aliwasili Cremona kabla yangu, na alikuwa amefanya mipango mikutano ifanywe katika nyumba iliyokodishwa. Upesi makasisi Wakatoliki wa eneo hilo wakatambua utendaji wetu nao wakakasirika sana na kuwaonya watu vikali kutuhusu.

 Siku moja, tuliitwa tufike kwenye kituo cha polisi cha eneo hilo. Maofisa hawakutukamata, lakini walionyesha wazi kwamba Doris alipaswa kuondoka Cremona, kwa kuwa alikuwa mtu wa nchi nyingine. Mwishowe, Doris alirudi nchini Denmark ambako aliendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu.

 Baada ya muda mfupi, dada mwingine mseja, aliyeitwa Brunilde Marchi, alipewa mgawo wa kuja Cremona. Brunilde alikuwa mpole, mchangamfu, naye alipenda kazi ya kuhubiri. Alianzisha mafunzo mengi ya Biblia, na baadhi yao walifanya maendeleo mazuri.

 Ninamshukuru Yehova kwamba nilipata nafasi ya kuwa sehemu ya mwanzo mdogo katika kazi ya kuhubiri huko Cremona. Leo, kuna makutaniko matano katika jiji hilo!

Jambo Lenye Kustaajabisha

 Kabla ya miaka miwili kupita nikiwa huko Cremona nilipokea simu kutoka kwenye ofisi ya tawi. Kulikuwa na kazi nyingi ya kutafsiri kwa ajili ya kusanyiko la siku sita la “Waabudu Wenye Umoja,” ambalo lingefanyika Julai 1961. Kwa hiyo, nilialikwa kurudi Betheli. Nilirukaruka kwa shangwe! Februari 1, 1961, nilirudi Betheli.

 Licha ya kwamba tulifanya kazi kwa saa nyingi kila siku, lilikuwa pendeleo kuwa na shughuli nyingi kila siku kutokeza habari zinazotegemea Biblia. Miezi hiyo ilipita upesi, na punde si punde wakati wa kusanyiko ukafika.

 Kwenye kusanyiko hilo, nilisikia tangazo kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ingetafsiriwa katika Kiitalia. Nikajiambia, “Hiyo inamaanisha kutakuwa na kazi nyingi sana.” Sikukosea. Muda wa mgawo wangu Betheli uliongezwa. Kwa kweli, zaidi ya miaka 60 baadaye, bado niko hapa!

Katika Idara ya Utafsiri, mwaka wa 1965

Zawadi Nyingine Zenye Thamani Kutoka kwa Yehova

 Zawadi nyingine ambayo nimethamini sana kadiri ambavyo miaka imepita ni useja. Simaanishi kwamba sikuwahi kufikiria kuolewa. Kwa kweli, kwa muda fulani wazo la kubaki nikiwa mseja lilinitia wasiwasi. Kwa hiyo, nilisali kwa Yehova. Yeye ananijua vizuri kuliko mtu yeyote. Nilimwomba anisaidie kufahamu ni njia gani inayonifaa.

 Nilianza kuelewa Maandiko kama vile Mathayo 19:11, 12 na 1 Wakorintho 7:8, 32 kwa njia mpya, nami nikamshukuru Yehova kwa uelewaji huo na amani ya moyoni aliyonipa. Sijawahi kujutia uamuzi wangu, nami ninashukuru kwamba nimefaulu kutumia useja wangu kumpa Yehova kilicho bora.

 Kadiri ambavyo miaka imepita, nimejionea mabadiliko mengi katika utendaji wa Idara ya Utafsiri, kadiri ambavyo tengenezo la Yehova limetumia teknolojia mpya hatua kwa hatua na “maziwa [mengine] ya mataifa.“ (Isaya 60:16) Mabadiliko hayo yameimarisha umoja wa undugu wetu wa ulimwenguni pote. Kwa mfano, mwaka wa 1985 matoleo ya Kiitalia ya Mnara wa Mlinzi yalianza kutolewa wakati uleule na ya Kiingereza. Leo, makala na video zinapatikana katika lugha nyingi kwenye jw.org, na nyingi kati yake zinatolewa wakati uleule na za Kiingereza. Ni wazi kwamba Yehova anahakikisha watu wake wana umoja na kwamba wanapokea chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.

 Yehova amenionyesha ukarimu mwingi sana. Aliniruhusu niwasaidie watu wengine katika utumishi wa upainia wa pekee. Ametimiza tamaa yangu ya kutumikia Betheli, ambapo nimeanzisha urafiki na watu wenye umri na tamaduni mbalimbali. Isitoshe, baraka ya pekee ambayo nilipata ni kumwona mama yangu akibatizwa na kuwa mtumishi wa Yehova alipokuwa na umri wa miaka 68. Ninatarajia kwa hamu kumwona yeye na familia yangu yote wakati ambapo wale walio katika makaburi ya ukumbusho watafufuliwa.​—Yohana 5:28, 29.

 Ninasubiri kwa hamu kuona kile ambacho Yehova atawafanyia watumishi wake wakati ujao, wakati atakapofanya “vitu vyote kuwa vipya.” (Ufunuo 21:5) Nina uhakika wa jambo hili: Yehova hatawahi kuacha kutumwagia “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.”​—Yakobo 1:17.

Nikifanya kazi katika Idara ya Utafsiri leo

a Simulizi la maisha la Piero Gatti lilichapishwa katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2011, ukurasa wa 20-23.