Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JAY CAMPBELL | SIMULIZI LA MAISHA

Niliinuliwa Kutoka Ardhini Nikakwezwa Kwa Njia Ambayo Sikutazamia

Niliinuliwa Kutoka Ardhini Nikakwezwa Kwa Njia Ambayo Sikutazamia

 Tangu nilipokuwa mdogo nilikuwa mwenye haya sana. Nilipendelea kukaa ndani ya nyumba na kujificha ili watu wasinione. Mara nyingi nilijihisi sifai. Kwa kuwa sikuwa na zoea la kutoka nje, sikukutana sana na watu na nilikuwa na hofu kwamba watanitendea kwa dharau au kunivunjia heshima. Acheni niwasimulie kuyahusu maisha yangu.

 Mnamo Agosti 1967 nikiwa na miezi 18 nilipata homa kali. Siku ilikuwa imeanza vizuri na nilikuwa mtoto mwenye afya lakini baadaye siku hiyo, mambo yakabadilika. Nilipoamka siku iliyofuata miguu yangu ilikuwa dhaifu sana. Nilipelekwa hospitalini jijini Freetown, Sierra Leone, ambapo tuliishi na ikagunduliwa kwamba nilikuwa na ugonjwa wa polio. Ugonjwa huo unasababishwa na virusi na unamfanya mtu apooze na mara nyingi watoto walio chini ya miaka mitano ndio wanaoupata. Nilifanya mazoezi ya kuimarisha misuli lakini bado miguu yangu iliendelea kuwa dhaifu. Pole kwa pole, ilizidi kuwa dhaifu hivi kwamba singeweza kutembea au hata kusimama. Kwa sababu nilikuwa kilema, baba yangu alisema tena na tena kwamba mimi ni “nusu ya mtoto tu.” Nilijihisi sifai. Nilikuwa na uwezo wa kutambaa tu, basi nilihisi nitabaki hapohapo ardhini sikuzote.

Naendelea Kukua Huku Nikitambaa

 Mimi na mama tuliishi pamoja na familia nyingine maskini sana katika nyumba kadhaa zilizozungukwa na ua. Nililelewa hapo. Ingawa watu walinipenda, nilitamani sana kupendwa na baba, lakini baba yangu hakunipenda. Baadhi ya watu waliamini kwamba ugonjwa wangu haukuwa wa kawaida bali nilikuwa nimerogwa. Wengine walimshauri Mama anipeleke kwenye majengo ya shirika la kuwatunza watoto walemavu na kuniacha hapo nje langoni. Walimwambia akifanya hivyo, mzigo wa kunitunza utakuwa umemwondokea. Mama alikataa katakata mashauri hayo na alifanya kazi kwa bidii sana ili kunitunza.

 Kwa sababu singeweza kusimama au kutembea, nilitambaa tu. Hata hivyo, nilipojiburuta, niliumizwa na ardhi na sehemu nyingine nilizopitia. Ili nisiumie sana, nilijitahidi kuvaa nguo nzito na kwenye mikono, nilivaa viatu vya kanda mbili au slipa. Baadaye nilitumia mbao zenye umbo la herufi U na zililinda mikono yangu vizuri zaidi. Ili kusogea, niliweka vibao hivyo mbele yangu, kisha ningevishikilia kwa mikono nikiwa nimeinama na kuuburuta mwili wangu. Baada ya kusonga “hatua moja” nilijiandaa tena ili kuchukua hatua nyingine. Ilikuwa vigumu sana. Mikono na mabega yangu yalichoka sana. Kwa kuwa ilikuwa vigumu kutoka sehemu moja hadi nyingine, nilitoka nje ya uzio au ua wetu mara chache sana. Basi sikwenda shule au kucheza na watoto wengine. Mara nyingi nilikuwa na wasiwasi hali yangu itakuwaje ikiwa mama yangu atakufa.

 Nilisali kwa Mungu, nikamwomba anisaidie na asiruhusu nipate shida na kufikia hatua ya kuwa ombaomba. Nilihisi kwamba ikiwa ningemkaribia Mungu na kumtumikia kwa njia inayofaa, basi angeshughulikia mahitaji yangu. Kwa hiyo, siku moja mwaka wa 1981, licha ya uchungu mwingi uliohusika, nilitoka nje ya uzio wetu ili nikahudhurie ibada katika kanisa moja lililokuwa katika mtaa wetu. Sikustarehe hata kidogo kwa sababu ya vile watu walikuwa wakiniangalia. Kasisi hakunikaribisha, hata alimkemea mama yangu kwa sababu nilikuwa nimeketi kwenye benchi ambalo wengine walikuwa wamelipia ili waketi. Niliamua sitarudi huko tena.

Jinsi Nilivyoanza Kumfahamu Baba Yangu wa Mbinguni

 Mwaka wa 1984 nilikuwa na umri wa miaka 18. Nyumba yetu ilikuwa na chumba cha ghorofa na kama kawaida yangu asubuhi moja nilipanda kwenye chumba hicho ili niketi karibu na dirisha. Nilipenda kuketi hapo ili nione mambo yanayoendelea ulimwenguni. Hata hivyo, niliamua kushuka na kwenda hapo nje ya nyumba kwa sababu kwa kawaida watu hawakuwa wengi hapo. Nilipofika hapo, nilikutana na wanaume wawili ambao walikuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba. Walinieleza kwamba wakati ujao mambo yatakuwa mazuri na hali yangu itabadilika. Walinisomea Isaya 33:24 na Ufunuo 21:3, 4. Kisha wakanipa broshua maridadi, Furahia Milele Maisha Duniani! na wakaahidi kwamba wangerudi na kunifundisha mengi zaidi.

 Waliporudi mara ya pili, waliniambia kwamba wangemleta Pauline, mmishonari ambaye alikuwa amekuja nchini muda si mrefu. Pauline aliendelea kunifundisha. Mimi na Pauline tukawa karibu kama mama na binti. Mama yangu alinitia moyo niendelee kujifunza Biblia pamoja na “mama yangu mpya” ambaye alikuwa mwenye kujidhabihu, mwenye upendo, subira, na fadhili. Isitoshe, Pauline alipendezwa nami na alipitia nyumbani mara nyingi ili kujua jinsi ninavyoendelea. Alinifundisha kusoma. Kwa wororo, alitumia chapisho Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia ili kunisaidia kumfahamu Baba mwenye upendo ambaye nilikuwa nimetamani kupata sikuzote.

Pauline, dada mmishonari ambaye alinifundisha Biblia

 Mambo niliyojifunza kutoka kwenye Biblia yalinipa shangwe nyingi. Siku moja, nilimuuliza Pauline ikiwa ningeweza kuhudhuria mkutano uliofanywa na Mashahidi wa Yehova ulioitwa Funzo la Kitabu la Kutaniko. a Ulikuwa ukifanywa katika nyumba ya Shahidi mmoja karibu na kwetu. Pauline alikubali. Jumanne iliyofuata, alikuja na akasubiri nioge na kuvaa ili tuhudhurie mkutano huo pamoja. Mtu mmoja alisema kwamba ninapaswa kumwambia Pauline anilipie usafiri, lakini nilimwambia, “Nitatembea kwa vibao vyangu.”

 Muda wa kuondoka ulipofika, mama yangu na pia majirani walinitazama kwa wasiwasi. Nilipokuwa nikijiburuta kuelekea langoni, baadhi ya majirani walimwambia Pauline kwa sauti kubwa, “Unamlazimisha!”

 Pauline aliniuliza kwa upole, “Jay, unataka kwenda?” Hii ilikuwa nafasi yangu ya kuonyesha kwamba ninamtegemea Yehova. (Methali 3:5, 6) Nikajibu: “Ndiyo, huu ni uamuzi wangu.” Majirani walinyamaza, lao likawa jicho tu lakini walibadili msimamo nilipokaribia lango. Nilipotoka tu nje ya lango, walinishangilia sana.

 Nilifurahia sana mkutano huo! Uliniburudisha sana! Kila mtu alinikaribisha kwa uchangamfu. Hakuna mtu aliyenionyesha dharau. Nilijihisi nikiwa nyumbani. Kwa hiyo, nikaanza kuhudhuria mkutano huo kwa ukawaida. Muda mfupi baadaye, nikauuliza ikiwa ningeweza kuhudhuria mikutano mikubwa zaidi iliyofanywa kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Nilikuwa maskini na nilikuwa na magauni (nguo) mawili tu na pea moja ya kandambili au slipa. Hata hivyo, nilikuwa na uhakika kwamba watu wa Mungu wangenikubali. Na bila shaka walinikubali.

 Ili kufika kwenye Jumba la Ufalme, nilihitaji “kutembea” hadi mwisho wa mtaa wa kwetu na kisha kuchukua teski iliyonipeleka hadi bondeni ambapo Jumba la Ufalme lilikuwa. Kisha akina ndugu wangenibeba kwenye mikono yao na kuniingiza kwenye jumba.

 Nilihisi nimeonja wema wa Yehova, na nilitamani kumfanya awe kimbilio langu. Kwa hiyo, niliamua kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. (Zaburi 34:8) Katika msimu wa mvua, mara nyingi nilifika kwenye Jumba nikiwa nimeloa na nikiwa na matope, hivyo nililazimika kubadili nguo baada ya kufika; lakini nilijua jitihada hizo hazikuwa za bure!

 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1985 kilieleza kuhusu kisa changu. Josette, dada kutoka Uswisi, alisoma simulizi langu kwenye kitabu hicho, na aliguswa moyo sana hivi kwamba akanitumia kiti cha magurudumu. Kiti hicho kilikuwa na magurudumu matatu yenye mabango mazuri ya kuzuia matope na pia taa za nyuma zenye rangi maridadi. Sasa ningeweza kusafiri nikiwa nadhifu. Watoto walikipenda sana kiti changu cha magurudumu na walifurahi sana waliponiona nikikiendesha. Nilikuwa nimeinuliwa kutoka ardhini! Sikuhitaji kutambaa tena. Niliacha kuhisi sifai, sasa nilihisi kana kwamba mimi ni malkia anayeheshimiwa.

Nakwezwa Juu Zaidi

 Haikuwa vigumu kwangu kufanya maendeleo ya kiroho kwa sababu nilikuwa ninaishi maisha rahisi na nilikuwa na maadili mazuri. Kiti changu kilifanya iwe rahisi kwenda utumishi. Nilibatizwa Agosti 9, 1986. Ubatizo ulibadili maisha yangu na nikawa na shangwe na uradhi. Isitoshe, nilihisi ninajiheshimu na nikawa na maoni mazuri kujihusu kwa sababu sasa nilikuwa nimepata Baba anayenipenda na nilikuwa nimezungukwa na watu wanaonipenda kikweli.

 Nilifikiria kile nitakachofanya ili nimlipe Yehova, na nilihisi kufanya upainia ni njia nzuri ya kutimiza tamaa hiyo. Hata hivyo, nilikuwa na wasiwasi kwamba nitashindwa. (Zaburi 116:12) Nilisali kuhusu jambo hilo na nikaamua kujaribu. Nilianza upainia Januari 1, 1988, na bado ninaendelea! Nimefurahia sana baraka ya kuwa painia. Ndugu na dada wapendwa hunisaidia kufikia takwa la saa kila mwezi. Zaidi ya hilo, Yehova amekuwa akinitegemeza kupitia roho yake takatifu.​—Zaburi 89:21.

 Baada ya kuanza upainia nilienda sehemu mbalimbali ili kuwafikia watu na kufanya hivyo kuliisaidia miguu yangu kupata nguvu kidogo ingawa bado ilikuwa dhaifu. Baada ya muda nilienda kwenye hospitali moja mpya nikitumaini kupata huduma ya mazoezi ya kuimarisha misuli. Hata hivyo, muuguzi mmoja hapo aliniambia nisijichoshe kutafuta matibabu kwa sababu ningekufa baada ya muda mfupi. Muuguzi mwingine aliponiambia maneno hayohayo, nilikata tamaa. Basi niliporudi nyumbani nilimsihi Yehova anisaidie kukabiliana na hisia hizo na nikamwomba pia anisaidie kupata matibabu.

 Kwa kushangaza, niligundua kwamba dawa nzuri zaidi kwa ajili ya ugonjwa wangu ni kushiriki utumishi wa shambani. Kwenda huku na huku kulinisaidia kufanya mazoezi ya kutosha. Miaka kadhaa baadaye, mmoja wa wale wauguzi ambao walikuwa wameniambia nitakufa, alipita karibu na Jumba la Ufalme na akaniona. Alishtuka sana alipoona kwamba bado niko hai!

 Licha ya ugonjwa wangu, nimejitahidi kuendelea kumtumikia Yehova kwa bidii. Akina ndugu na dada hunipongeza kwa sababu ya bidii yangu na pia kwa sababu ninafika mapema mikutanoni. Ninapenda kufika mapema ili nipate muda wa kusalimiana na ndugu na dada zangu na kuwajulia hali.

 Nimeonja wema wa Yehova na nimejionea jinsi ambavyo amenibariki maishani. Nimefurahia pendeleo la kuwasaidia watu watatu kufikia ubatizo. Mmoja wao ni Amelia, na alihudhuria darasa la 137 la Gileadi. Nimehudhuria Shule ya Utumishi wa Painia zaidi ya mara moja na kwa kweli shule hiyo ni zawadi nzuri kutoka kwa Yehova. Yehova amenifanya niwe mtu mwenye furaha zaidi, anayejiheshimu, na mwenye ujasiri. Sasa watu wananiheshimu. Sijionei aibu tena. Nina marafiki wazuri, si jijini Freetown tu, bali katika nchi nzima na pia sehemu mbalimbali ulimwenguni. Wao si marafiki tu, bali pia ni ndugu zangu.

 Ni zaidi ya miaka 40 tangu niliposikia kuhusu ahadi ya Mungu ya dunia mpya ambapo ulemavu hautakuwepo tena. Ahadi hiyo inanitia moyo sana, ninajua kwamba itakuja na ninaisubiri kwa hamu. Nina mtazamo wa kumngojea Mungu wangu, Yehova, kwa sababu ninajua kwamba hatachelewa. (Mika 7:7) Kuendelea kusubiri kumeniwezesha kupata baraka nyingi. Yehova amenisaidia kukabiliana na matatizo mbalimbali. Sikuzote, yeye hunipa msaada wakati unaofaa. Nina furaha ya kweli na ninaendelea kutabasamu kwa sababu niliinuliwa kutoka ardhini nilipokuwa nikatambaa nikakwezwa kwa njia ambayo sikutazamia.

a Sasa linaitwa Funzo la Biblia la Kutaniko.