Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

PHYLLIS LIANG | SIMULIZI LA MAISHA

Yehova Amebariki Utayari Wangu

Yehova Amebariki Utayari Wangu

“Niko tayari kwenda.” Maneno hayo yalisemwa na Rebeka anayetajwa katika Biblia alipoombwa afanye badiliko kubwa maishani ili kutimiza mapenzi ya Yehova. (Mwanzo 24:50, 58) Ijapokuwa sijioni kuwa mtu wa pekee, nimejaribu kuwa na utayari kama wa Rebeka katika utumishi wa Yehova. Nimekabili changamoto mbalimbali, lakini nimejionea jinsi Yehova anavyobariki mtazamo wa utayari, wakati mwingine katika njia ambazo sikutarajia.

Mwanamume Mzee Atuletea Hazina

 Miaka michache baada ya familia yetu kuhamia mji wa Roodepoort, Afrika Kusini, baba yangu alikufa. Mwaka wa 1947, nikiwa na umri wa miaka 16, niliajiriwa kwenye kampuni ya simu ya serikali, na nilifanya kazi ili kusaidia kuitegemeza familia yetu. Siku moja nikiwa nyumbani, mwanamume mmoja mzee alikuja na kutuomba tujiandikishe ili tuwe tukipata gazeti la Mnara wa Mlinzi. Tulijiandikisha ili kumfurahisha tu.

 Hata hivyo, muda si muda tulipata hamu ya kujua kile ambacho kwa kweli Biblia inafundisha. Mama alikuwa mshirika wa dini ya Dutch Reformed Church alipokuwa mdogo, kwa hiyo, aliona waziwazi tofauti kati ya kile ambacho Biblia hufundisha na kile ambacho dini hiyo ilifundisha. Tulikubali kujifunza Biblia na pia tukaanza kuhudhuria mikutano. Nilikuwa mtu wa kwanza katika familia yetu kubatizwa na nilibatizwa mwaka wa 1949. Niliendelea kufanya kazi ya kimwili kwa miaka kadhaa lakini nilitamani kufanya mengi zaidi katika kazi ya Yehova.

Kuwa Tayari Kwenda Mahali Palipokuwa na Uhitaji

FomaA/stock.adobe.com

Koeksisters

 Nilianza upainia wa kawaida mwaka wa 1954, na nilitaka kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi basi nikaomba ofisi ya tawi ya Afrika Kusini mapendekezo kuhusu mahali pa kwenda. Ofisi ya tawi ilipendekeza niende katika jiji la Pretoria na wakafanya mipango dada mwingine painia ajiunge nami huko. Tulipata nyumba nzuri, na bado ninakumbuka maandazi matamu yanayoitwa koeksisters ambayo yaliuzwa karibu na kwetu. Maandazi hayo husokotwa kisha yanachomwa kwenye mafuta na kuchovywa kwenye umajimaji wenye sukari.

 Painia mwenzangu aliolewa na baada ya hapo mtumishi wa ofisi ya tawi, Ndugu George Phillips, aliniuliza ikiwa ningependa kuwa painia wa pekee. Nilikubali bila kusita.

 Nilianza mgawo wangu wa kwanza nikiwa painia wa pekee mwaka wa 1955, katika mji wa Harrismith. Nilipata mwandamani mpya lakini haikuwa rahisi kwetu kupata mahali pazuri pa kuishi. Kwa mfano, washirika wa kanisa moja katika eneo hilo walipojua kwamba tumehamia huko walimshurutisha mwenye nyumba atufukuze.

 Baadaye, nilipewa mgawo wa kwenda Parkhurst, jijini Johannesburg. Dada wawili wamishonari walijiunga nami. Baada ya muda, mmoja alihamishiwa sehemu nyingine na mwingine akaolewa. Dada anayeitwa Eileen Porter alinikaribisha niishi na familia yake hata ingawa nyumba yake haikuwa kubwa. Nililala kwenye chumba kidogo ambacho kilitenganishwa na vyumba vingine kwa pazia tu. Eileen alikuwa mwenye fadhili na alinitia moyo, nilimpenda sana na alinifanya nijihisi nikiwa nyumbani. Nilivutiwa na bidii yake kwa ajili ya kweli licha ya kwamba alikuwa na majukumu mengi ya kutunza familia.

 Muda si muda, nilipewa mgawo wa kutumikia Aliwal North, mji ulio katika mkoa wa Eastern Cape, na dada Merlene (Merle) Laurens alikuwa mwandamani wangu. Wakati huo, mimi na Merlene tulikuwa na miaka ishirini na kitu na tulitiwa moyo na bidii ya dada mwenye umri mkubwa aliyeitwa Dorothy, tulimpenda sana na tulizoea kumwita Shangazi Dot. Alipokuwa kijana, pindi moja alishambuliwa na mbwa kadhaa akiwa katika huduma lakini hilo halikupunguza bidii yake.

 Mwaka wa 1956, Merle alialikwa kuhudhuria darasa la 28 la Gileadi. Nilitamani sana kwenda pamoja naye! Hata hivyo, Shangazi Dot alinitunza vizuri, na tukawa marafiki wakubwa licha ya kwamba alinizidi sana umri.

 Huwezi kuwazia furaha niliyokuwa nayo nilipopokea mwaliko wa kuhudhuria Shule ya Gileadi kama rafiki yangu Merle! Kabla ya kuondoka, nilitumikia kwa miezi nane katika mji wa Nigel, pamoja na Kathy Cooke, mhitimu wa shule ya Gileadi. Kathy alinieleza mambo yenye kusisimua kuhusu shule hiyo na kwa kweli aliichochea hamu yangu, na Januari 1958, nikaenda New York.

Kuwa Tayari Kuzoezwa

 Nilipofika Gileadi, nilikaa chumba kimoja na Dada Tia Aluni kutoka Samoa, na Dada Ivy Kawhe, ambaye ni Mmaori. Nilipokuwa Afrika Kusini, serikali ilitenganisha watu weupe na watu wa jamii nyingine kwa sababu ya sera ya ubaguzi wa rangi, kwa hiyo nilifurahia sana kuishi na dada wa jamii nyingine kwa mara ya kwanza. Punde si punde, tukawa marafiki wa karibu na nilifurahia sana kuwa katika darasa lenye watu kutoka mataifa mbalimbali.

 Mmoja wa walimu wetu wa Gileadi alikuwa Ndugu Maxwell Friend. Kwa kweli njia yake ya kufundisha ilikuwa ya pekee. Darasani alikuwa na taa tatu, taa moja ilikuwa imeandikwa “Sauti,” nyingine “Mwendo,” na ya mwisho “Shauku.” Mwanafunzi alipokuwa akitoa hotuba au onyesho, Ndugu Friend angewasha taa husika ili kumchochea mwanafunzi kuboresha sehemu yake. Kwa sababu mimi ni mwenye haya, mara nyingi aliniwashia taa hizo na wakati mwingine nililia! Lakini bado nilimpenda Ndugu Friend. Pindi fulani nilipokuwa nikifanya mgawo wa usafi kabla ya kwenda darasani, kwa fadhili angeniletea kikombe cha kahawa.

 Kadiri miezi ilivyopita, nilijiuliza nitatumwa wapi. Merle, mwandamani wangu wa awali, alikuwa ameshahitimu Gileadi na kutumwa Peru. Merle alipendekeza nimuulize Ndugu Nathan Knorr, ambaye alikuwa akiongoza kazi wakati huo, ikiwa ningeweza kutumwa Peru. Mmishonari ambaye alikuwa mwandamani wa Merle alikuwa karibu kuolewa kwa hiyo ningeweza kuchukua nafasi yake. Kwa kuwa Ndugu Knorr alitembelea Gileadi kila baada ya majuma kadhaa, ilikuwa rahisi kupata fursa ya kuzungumza naye. Nilipohitimu nilitumwa Peru!

Kutumikia Milimani

Nikiwa na Merle (kulia) nchini Peru, 1959

 Nilifurahi sana kuwa pamoja na Merle tena huko Lima, Peru! Punde tu baada ya kufika Peru, nilipata wanafunzi wa Biblia waliofanya maendeleo, hata ingawa bado nilikuwa nikijifunza Kihispania. Baada ya muda, mimi na Merle tulitumwa Ayacucho, eneo ambalo lilikuwa milimani. Kusema kweli mgawo huo haukuwa rahisi. Ingawa nilikuwa nimejifunza Kihispania, watu wengi katika eneo hilo walizungumza Kikwechua tu, isitoshe, ilikuchukua muda kuzoea hali ya hewa na pia maisha ya milimani.

Nikihubiri nchini Peru, 1964

 Nilihisi kana kwamba sikuwa nimetimiza mengi huko Ayacucho, na nilijiuliza ikiwa kungekuwa na ukuzi katika eneo hilo. Hata hivyo, leo kuna zaidi ya wahubiri 700 jijini Ayacucho na pia kuna ofisi ya utafsiri ya Kikwechua cha Ayacucho.

 Baada ya muda, Merle alifunga ndoa na Ramón Castillo, ambaye alikuwa mwangalizi wa mzunguko, na katika mwaka wa 1964, Ramón alihudhuria masomo ya miezi 10 Gileadi. Katika darasa hilo, Ramón alikutana na ndugu kijana aliyeitwa Fu-lone Liang, ambaye tulisoma pamoja Gileadi. Fu-lone Liang alikuwa akitumikia Hong Kong lakini alikuwa amealikwa tena Gileadi kwa ajili ya mafunzo zaidi kuhusiana na majukumu ya ofisi ya tawi. a Fu-lone alimuuliza Ramón jinsi nilivyokuwa nikiendelea, na baadaye mimi na Fu-lone tukaanza kuandikiana barua.

 Kutoka mwanzoni, Fu-lone alisema waziwazi kwamba kwa kuandikiana barua tulikuwa tumeanza uchumba. Fu-lone aliporudi Hong Kong alikuwa pamoja na Harold King, mmishonari mwenzake. Harold King alienda posta mara kwa mara, basi alikubali kutuma barua ambazo Fu-lone alikuwa akiniandikia. Harold alichora michoro midogo na kuandika ujumbe mfupi juu ya bahasha ambazo zilikuwa na barua kutoka kwa Fu-lone. Kwa mfano aliandika: “Nitajaribu kumtia moyo aandike barua mara nyingi zaidi!”

Mimi na Fu-lone

 Tuliwasiliana kupitia barua kwa miezi 18 hivi kisha tukaamua kufunga ndoa. Niliondoka Peru baada ya kutumikia nchini humo kwa miaka saba hivi.

Kuanza Maisha Mapya Hong Kong

 Mimi na Fu-lone tulifunga ndoa Novemba 17, 1965. Nilifurahia maisha yangu mapya Hong Kong. Mimi na mume wangu tuliishi katika ofisi ya tawi na ndugu wengine wawili pamoja na wake zao. Fu-lone alifanya kazi ya utafsiri na mimi nilifanya kazi ya kuhubiri. Haikuwa rahisi kujifunza Kichina (Kikantoni), lakini mume wangu pamoja na dada wamishonari walinisaidia kujifunza lugha hiyo na walikuwa na subira. Kwa kuwa niliwafundisha watoto wadogo Biblia nilipokuwa nikiendelea kujifunza lugha, hilo lilinipunguzia mkazo kwa kiasi fulani.

Washiriki sita wa familia ya Betheli ya Hong Kong katika miaka ya 1960. Mimi na Fu-lone tuko katikati

 Miaka kadhaa ilipita kisha mimi na Fu-lone tukahamia kwenye nyumba ya wamishonari katika sehemu nyingine ya Hong Kong inayoitwa Kwun Tong, ili Fu-lone awafundishe wamishonari wapya Kikantoni. b Nilifurahia sana huduma katika eneo hili hivi kwamba mara nyingi sikutaka kurudi nyumbani jioni!

 Mwaka wa 1968, nilisisimka tulipopata kitabu kipya cha kujifunzia, Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Kwa kulinganisha na kitabu“Mungu na Awe wa Kweli,” kitabu hicho kipya kilikuwa kimerahisishwa na kiliwasaidia sana wanafunzi ambao hawakujua Biblia wala Ukristo.

 Hata hivyo, nilidhani kimakosa kwamba wanafunzi walikuwa wanakubali kweli kwa sababu tu walikuwa wanajibu vizuri maswali yaliyo kwenye chapisho. Katika kisa kimoja, nilishtukia kwamba mmoja wa wanafunzi wangu wa Biblia alikuwa amemaliza kitabu Kweli na bado hakuamini kuna Mungu! Nilijaribu kuwa na mazungumzo ya ziada pamoja na wanafunzi ili kujua jinsi walivyohisi kuhusu mambo waliyokuwa wakijifunza.

 Tuliishi Kwun Tong kwa miaka kadhaa kisha tukarudi kwenye ofisi ya tawi na Fu-lone akawa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Hong Kong. Kwa miaka mingi nilifanya kazi katika idara ya usafi na pia mapokezi. Pindi fulani, Fu-lone alisafiri kwa ajili ya migawo ya kitheokrasi ya siri na pindi hizo singeweza kuandamana naye, lakini nilihisi ni pendeleo kubwa kumuunga mkono alipokuwa akitimiza majukumu yake.

Fu-lone akitoa buku la pili la chapisho Unabii wa Isaya katika lugha ya Kichina cha zamani na Kichina kilichorahisishwa

Badiliko Ambalo Sikutazamia

 Kwa kusikitisha, mwaka wa 2008 maisha yangu yalibadilika ghafla. Mume wangu mpendwa, Fu-lone alikufa ghafla alipokuwa safarini, muda mfupi tu kabla ya Ukumbusho wa Kifo cha Yesu. Nilichanganyikiwa. Akina ndugu na dada walikuja upesi kunifariji, na wakati wa hotuba ya Ukumbusho, kilichonisaidia kujizuia kulia ni kumsaidia mgeni kutafuta maandiko yaliyokuwa yakisomwa. Nilifarijiwa na andiko ambalo Fu-lone alipenda sana, linasema: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika kwa nguvu mkono wako wa kulia . . . ‘Nitakusaidia.’”​—Isaya 41:13.

 Miaka saba baada ya kifo cha Fu-lone, akina ndugu kwenye ofisi ya tawi ya Hong Kong walipendekeza nihamie kwenye ofisi ya tawi ambayo ni kubwa zaidi ili nipate matibabu niliyohitaji. Kwa hiyo, mwaka wa 2015, nilihamia ofisi ya tawi ya Afrika Kusini ambayo ipo karibu na mahali ambapo nilisikia kweli kwa mara ya kwanza mwaka wa 1947.

 Nimemtumikia Yehova kwa miaka mingi na nimepata shangwe nyingi. Ninahisi kwamba Yehova amebariki utayari wangu. Ninawasiliana na watu niliowafundisha Biblia ambao sasa wanamtumikia Yehova kwa uaminifu na nimejionea jinsi Yehova anavyobariki sehemu ndogo tunayotimiza katika kazi ya kuhubiri. Kwa mfano, idadi ya wahubiri nchini Peru imeongezeka kutoka wahubiri 760 katika mwaka wa 1958 hadi wahubiri 133,000 mwaka wa 2021, na Hong Kong kulikuwa na wahubiri 230 mwaka wa 1965 lakini mwaka wa 2021 idadi ya wahubiri ilikuwa imeongezeka kufikia 5,565.

 Kwa sababu umri wangu umesonga, siwezi kufanya mengi kama nilivyofanya zamani. Lakini bado nina utayari na ninatazamia kuwa na utayari huohuo katika ulimwengu mpya wa Yehova ambapo kutakuwa na kazi nyingi ya kufanya, bila kusita nitasema: “Niko tayari kwenda.”

a Ili kusoma simulizi la jinsi Fu-lone Liang alivyopata kweli, ona 1974 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova, ukurasa wa 51.

b Ili kusoma simulizi kuhusu kijana mmoja ambaye alifundishwa Biblia na Fu-lone alipokuwa Kwun Tong, ona 1974 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova, ukurasa wa 63.