Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

DORINA CAPARELLI | SIMULIZI LA MAISHA

Licha ya Kuwa na Haya, Ikiwa Ningepewa Nafasi Nyingine Nisingebadili Chochote!

Licha ya Kuwa na Haya, Ikiwa Ningepewa Nafasi Nyingine Nisingebadili Chochote!

Nimekuwa mwenye haya tangu nilipokuwa mtoto. Hiyo ndiyo sababu nyakati nyingine ninacheka ninapokumbuka mambo fulani ambayo yametukia katika utumishi wangu kwa Yehova.

 Nilizaliwa mwaka wa 1934, katika jiji la Pescara lililo kwenye pwani ya mashariki ya kati ya Italia, pembezoni mwa bahari ya Adriatiki. Nilikuwa wa mwisho kuzaliwa kati ya wasichana wanne. Baba yetu aliamua kutupatia majina kwa kufuata herufi za alfabeti akianzia na “A,” na ndiyo sababu jina langu linaanza kwa herufi “D.”

 Baba yetu alipendezwa sana na mambo ya kiroho. Alikutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza Julai 1943 alipokutana na mwanamume aliyeitwa Liberato Ricci. Mwanamume huyo ambaye alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi alizungumza naye kuhusu Biblia na kumwazima nakala ya Mnara wa Mlinzi. Muda mfupi baadaye, Baba alianza kuzungumza na watu wengine kwa bidii kuhusu mambo aliyokuwa akijifunza. Mama pia alikubali kweli. Licha ya kwamba hakujua kusoma, yeye pia aliwaeleza watu wengine ujumbe huo wa tumaini, akitumia mistari ya Biblia ambayo alikariri.

 Nyumba yetu ndogo ilianza kuwa eneo lenye shughuli nyingi. Tulifanyia mikutano yetu ya Kikristo hapo. Ingawa tulikuwa na vyumba viwili tu vya kulala, tuliwakaribisha waangalizi wanaosafiri na mapainia.

 Dada zangu wakubwa wawili hawakupendezwa na Biblia na baada ya muda waliondoka nyumbani walipoolewa. Lakini mimi na dada yangu Cesira tulipenda sana kumsikiliza Baba aliposoma Biblia. Tulifurahia pia hotuba zinazochochea za ndugu waliotembelea kikundi chetu kidogo.

 Mara nyingi niliambatana na baba pamoja na watu wengine katika huduma, lakini nilikuwa mwenye haya sana hivi kwamba miezi mingi ilipita kabla ya kupata ujasiri wa kumhubiria mwenye nyumba yeyote. Hata hivyo, upendo wangu kwa Yehova uliendelea kukua na nilibatizwa Julai 1950. Ndugu alitoa hotuba ya ubatizo nyumbani kwetu, kisha tukaenda baharini kwa ajili ya ubatizo. Mwaka uliofuata wenzi wa ndoa wanaotumikia wakiwa mapainia wa pekee walitumwa kwenye eneo letu, na mara nyingi nilienda kuhubiri pamoja nao. Kadiri nilivyotumia muda mwingi katika huduma ndivyo ilivyokuwa rahisi zaidi kwangu. Hatua kwa hatua nikaja kupenda sana pendeleo hilo la utumishi.

Uamuzi Uliobadili Maisha Yangu

 Mwangalizi wetu wa kwanza wa mzunguko alikuwa Piero Gatti. a Alinitia moyo kufanya upainia na hata kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa watangazaji wa Ufalme—jambo ambalo sikuwahi kufikiria kulihusu. Katika eneo letu, ilikuwa desturi kwa wasichana kuishi nyumbani kwa wazazi wao hadi walipoolewa. Kwa hiyo, Machi 1952, nilianza upainia nikiwa bado nyumbani. Sikujua uamuzi huo ungekuwa na matokeo gani maishani mwangu.

 Wakati huohuo, dada mwingine mwenye umri wa miaka 21 hivi, anayeitwa Anna alitaka pia kuanza upainia. Alihamia nyumbani kwetu ili twende kuhubiri pamoja. Mwaka 1954, sisi wawili tulipewa mgawo wa kutumikia tukiwa mapainia wa pekee katika jiji la Perugia, lililokuwa umbali wa kilomita 250, ambalo halikuwa na Mashahidi wowote.

Mimi, Baba, na Anna kabla ya kuondoka kwenda Perugia

 Hilo lilikuwa jambo kusisimua kwangu! Nilikuwa na umri wa miaka 20. Nilikuwa nimetoka nje ya jiji letu mara moja tu nilipoambatana na wazazi wangu ili kuhudhuria kusanyiko. Hivyo, sasa nilihisi kana kwamba ninaenda upande mwingine wa dunia! Baba alikuwa na wasiwasi kidogo kuhusu wazo la mimi na Anna kuishi peke yetu, kwa hiyo alikuja kutusaidia kutafuta mahali pa kuishi. Tulipanga chumba ambacho tungeweza kutumia pia kama Jumba la Ufalme. Hata hivyo, kwa muda fulani ni sisi tu ambao tulihudhuria mikutano. Licha ya hilo, tulifurahia kuhubiri katika jiji la Perugia na pia katika miji na vijiji jirani, na baada ya muda jitihada zetu zikaanza kuzaa matunda. Mwaka mmoja baadaye, ndugu mmoja alihamia Perugia, na hivyo akawa akiongoza mikutano kwa ajili yetu. Kufikia mwaka wa 1957 wakati ambapo tulipewa mgawo katika eneo lingine, kutaniko dogo lilikuwa limeanzishwa.

Mimi na Anna tukiwa na mke wa mwangalizi wa mzunguko karibu na chemchemi ya Fontana Maggiore, jijini Perugia, mwaka wa 1954

 Mgawo wetu uliofuata ulikuwa katika jiji dogo lililoitwa Terni lililokuwa katikati mwa Italia. Tulifurahia sana kuhubiri katika jiji la Terni kwa sababu tayari kulikuwa na watu wengi wanaopendezwa. Lakini tulikuwa na changamoto pia. Ingawa serikali ya Kifashisti ilikomeshwa mwaka wa 1943, wenye mamlaka fulani waliendeleza jitihada za kuwazuia Mashahidi wa Yehova wasihubiri ujumbe wa Biblia na kusema kwamba tulipaswa kuwa na leseni ya kuhubiri nyumba kwa nyumba.

 Mara nyingi Mashahidi wa Yehova walifuatwa na polisi. Nyakati fulani tuliwakwepa polisi kwa kujiingiza katikati ya umati wa watu, lakini hatukufaulu nyakati zote. Nilisimamishwa na kukamatwa mara mbili. Mara ya kwanza nilikuwa nikihubiri na mwangalizi wa mzunguko. Polisi walitukamata na kutupeleka kwenye kituo cha polisi na kutushtaki kwa kuhubiri bila kuwa na kibali cha kisheria, kisha wakatutoza faini. Tulikataa kulipa faini hiyo kwa sababu hatukuvunja sheria yoyote. Moyo wangu ulipiga kwa kasi kwa sababu ya woga! Nilimshukuru Yehova kwamba sikuwa peke yangu. Nilikumbuka maneno yenye kutoa uhakikisho ya Isaya 41:13: “Usiogope. Nitakusaidia.” Tuliachiliwa, na kesi ilipofikishwa mahakamani, hakimu aliifuta. Nilikamatwa kwa mara ya pili miezi sita baadaye. Wakati huo, nilikuwa peke yangu. Lakini kwa mara nyingine tena, hakimu alisema sikuwa na hatia.

Fursa Nyingi Zaidi za Kumtumikia Yehova

 Ninakumbuka nilisisimka sana kuhusu kusanyiko la mwaka wa 1954 lililofanyika Naples, kusini mwa Italia. Nilipofika huko, nilijitolea kufanya usafi wa eneo la kusanyiko na nikapewa mgawo wa kufanya usafi karibu na jukwaa. Nilipokuwa hapo nilimwona mkaribishaji mmoja mwenye sura yenye kuvutia aliyeitwa Antonio Caparelli, aliyekuwa painia nchini Libya. Familia yao ilihamia huko kutoka Italia mwishoni mwa miaka ya 1930.

Antonio akiendesha pikipiki aliyokuwa akitumia nchini Libya

Siku yetu ya harusi

 Antonio alikuwa mwenye nguvu na jasiri. Alisafiri kwenda mbali katika Jangwa la Libya kwa kutumia pikipiki yake ili akawahubirie Waitalia walioishi huko. Mara kwa mara tuliandikiana barua. Hata hivyo, mapema katika mwaka wa 1959, alirudi Italia. Alitumikia kwenye Betheli iliyoko Rome kwa miezi michache kabla ya kupewa mgawo wa kuwa painia wa pekee katika jiji la Viterbo, lililoko katikati mwa Italia. Uhusiano wetu uliendelea kukua, na tukafunga ndoa Septemba 29, 1959. Nilihamia Viterbo na kujiunga na Antonio.

 Tulihitaji mahali pa kuishi na pa kufanyia mikutano. Tulikodi chumba fulani kilichokuwa kama duka dogo lenye bafu upande wa nyuma. Tuliweka kitanda chetu kwenye kona na kuweka aina fulani ya pazia. Hicho kikawa chumba chetu cha kulala. Eneo lililobaki lilitumika kama sebule au Jumba la Ufalme, ikitegemea ni siku ipi. Haikuwa rahisi kuishi katika chumba hicho, na nisingekubali kuishi hapo nikiwa peke yangu. Lakini nilikuwa na furaha kwa sababu nilikuwa na Antonio.

Tukiwa mbele ya pazia iliyotenganisha “chumba chetu cha kulala”

 Mwaka wa 1961, Antonio aliwekwa rasmi kutumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko. Hata hivyo, kwanza alipaswa kuhudhuria shule ya mwezi mzima kwa ajili ya watumishi wa kutaniko, au waangalizi. Hilo lilimaanisha kwamba ningelazimika kuishi peke yangu kwa mwezi mmoja. Kusema kweli nilijihurumia sana, hasa jioni kwa kuwa nilikuwa peke yangu katika chumba hicho kidogo. Hata hivyo, nilikuwa na furaha kwa sababu Antonio alikuwa akitumiwa na Yehova. Nilijitahidi kuwa na mengi ya kufanya, kwa hiyo muda huo ulipita haraka.

 Kazi ya mzunguko ilihusisha kusafiri sana. Tulianzia Veneto, eneo lililo kaskazini mwa Italia, hadi Sicily iliyoko upande wa kusini. Mwanzoni hatukuwa na gari hivyo tulitumia usafiri wa umma. Pindi fulani, baada ya kurushwarushwa ndani ya basi kwa sababu ya barabara mbaya za Sicily vijijini, tulipokewa na akina ndugu wakiwa na punda wa kubeba mizigo yetu. Antonio alikuwa amevaa suti yake na tai, na mimi nilikuwa nimevaa gauni maridadi la mikutano. Huenda ungecheka sana ikiwa ungetuona tukitembea kando ya wakulima na punda waliokuwa wamebeba taipureta na mikoba yetu.

 Akina ndugu walishiriki pamoja nasi chochote walichokuwa nacho hata kama kilikuwa kidogo sana. Baadhi ya nyumba hazikuwa na bafu au maji ya bomba. Pindi moja tulikaa katika chumba ambacho hakikuwa kimetumiwa kwa miaka mingi. Wakati wa usiku niligeuka-geuka sana usingizini hivi kwamba Antonio akaniamsha. Tulipoinua shuka, tulishtuka sana kuona godoro likiwa limejaa wadudu! Hatukuweza kufanya chochote kwa kuwa ilikuwa usiku wa manane. Kwa hiyo, tulijaribu tu kuwatoa wadudu wengi iwezekanavyo na kurudi kulala.

Nikiwa na Antonio katika kazi ya mzunguko miaka ya 1960

 Lakini sikuona mambo hayo kuwa changamoto kubwa kwangu. Changamoto kubwa zaidi niliyokabili ni kwamba nilikuwa mwenye haya. Tulipotembelea kutaniko kwa mara ya kwanza, ilikuwa vigumu kwangu kuanzisha urafiki. Lakini nilitamani sana kuwatia moyo na kuwasaidia akina dada, kwa hiyo, nilifanya jitihada za pekee. Kwa msaada wa Yehova, juma lilipoisha, kwa kawaida nilijihisi huru zaidi. Lilikuwa ni pendeleo kubwa kufanya kazi na ndugu na dada na kuona ukarimu wao, uaminifu wao, na upendo wao kwa Yehova.

 Mwaka wa 1977, baada ya miaka michache kuwa katika kazi ya kuzungukia makutaniko na uangalizi wa wilaya, b tulialikwa Betheli huko Rome ili kusaidia kufanya matayarisho ya Kusanyiko la Kimataifa la “Imani Ishindayo” la 1978. Baada ya miezi michache tu, tukawa sehemu ya familia ya Betheli. Muda mfupi baada ya hapo, Antonio akawekwa rasmi kutumikia kwenye Halmashauri ya Tawi.

 Betheli ilikuwa eneo jipya kwangu, kwa mara nyingine tena hisia zangu za haya zilinizuia kujihisi huru. Lakini kwa msaada wa Yehova na Wanabetheli wengine, nilianza kuona Betheli kuwa kama nyumbani.

Kukabiliana na Changamoto Mpya

 Miaka iliyofuata tulikabili changamoto mpya, yaani, matatizo ya kiafya. Mwaka wa 1984, Antonio alifanyiwa upasuaji wa moyo, na baada ya miaka mingine kumi, akawa na matatizo mengine ya afya. Kisha mwaka wa 1999, aligunduliwa kuwa na uvimbe mbaya sana. Sikuzote alikuwa mwenye nguvu na bidii, lakini alishindwa kupambana na ugonjwa huo mbaya. Nilihuzunika sana kumwona akidhoofika hatua kwa hatua. Nilisali kwa Yehova kwa bidii, na kumwomba anipe nguvu za kumsaidia mume wangu. Pia, nilisoma kitabu cha Zaburi mara nyingi. Maandiko hayo yalinifariji kwa kiasi fulani nilipokuwa na wasiwasi. Antonio alikufa Machi 18, 1999. Tulikuwa tumeoana kwa miaka 40 hivi.

 Ni ajabu kwamba unaweza kujihisi mpweke hata ingawa umezungukwa na watu wengi. Nilionyeshwa upendo mwingi na nilifarijiwa sana na Wanabetheli wenzangu pamoja na ndugu na dada tuliowafahamu wakati wa kazi ya mzunguko. Hata hiyo, moyo wangu ulijaa huzuni hasa niliporudi kwenye chumba changu cha Betheli jioni na kuwa peke yangu, ni maumivu ambayo ni vigumu hata kuelezea. Sala, kujifunza kibinafsi, na kuacha muda upite kulinisaidia kurudia hali yangu ya kawaida. Sasa, ninapokumbuka mambo tuliyofanya pamoja na Antonio, naburudika sana moyoni. Bado ninapenda kukumbuka mambo ambayo tulifanya pamoja, na nina uhakika kwamba Antonio yupo katika kumbukumbu la Yehova na nitamwona tena atakapofufuliwa.

 Nimekuwa na migawo mbalimbali hapa Betheli, kwa sasa ninatumikia katika idara ya ushonaji. Ninafurahia kufanya kazi ambayo inanufaisha familia kubwa ya Betheli. Pia, ninajitahidi kushiriki kwa bidii katika huduma. Ni kweli kwamba siwezi kufanya mengi kama ilivyokuwa wakati uliopita, lakini bado ninafurahia kushiriki habari njema ya Ufalme—pendeleo ambalo nilifurahia tangu nilipokuwa msichana. Kwa sababu hii, ninapenda kuwatia moyo vijana wafanye upainia. Ninajua kwamba kazi hiyo inasisimua sana.

“Ninafurahia kufanya kazi ambayo inanufaisha familia kubwa ya Betheli”

 Ninapofikiria miaka karibu 70 ambayo nimetumia katika utumishi wa wakati wote, ninajionea jinsi ambavyo Yehova amenisaidia na kunibariki. Bado nina haya, kwa hiyo ninajua kwamba kwa nguvu zangu mwenyewe, nisingeweza kufanya mambo yote niliyotimiza. Nimesafiri kwenda maeneo ya mbali, nikajionea mambo mengi yenye kutia moyo, na nikakutana na watu wengi ambao wamenifundisha mambo mengi muhimu. Ninaweza kusema bila shaka lolote kwamba ikiwa ningepewa nafasi nyingine nisingebadili chochote.

a Simulizi la maisha la Piero Gatti, “Niliogopa Kifo—Sasa Ninangoja ‘Uzima kwa Wingi,’” linapatikana kwenye toleo la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2011.

b Mwangalizi wa wilaya alitumikia mizunguko kadhaa iliyofanyiza wilaya.