Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JESÚS MARTÍN | SIMULIZI LA MAISHA

“Yehova Aliniokoa Nilipokabili Hali Ngumu Zaidi Maishani Mwangu”

“Yehova Aliniokoa Nilipokabili Hali Ngumu Zaidi Maishani Mwangu”

Nilizaliwa jijini Madrid mwaka wa 1936. Wahispania wa kizazi changu hawawezi kuusahau mwaka huo. Ni mwaka ambao vita vikali vya wenyewe kwa wenyewe vilizuka nchini Hispania.

 Vita hivyo vilisababisha mateso makali nchini Hispania kwa zaidi ya miaka mitatu, na watu wengi waliachwa na majeraha ya kimwili na ya kihisia pia. Baba yangu alipata madhara hayo pia. Baba alimwamini Mungu, lakini alisikitika sana na kukata tamaa alipoona jinsi makasisi Wakatoliki walivyojihusisha na vita. Basi akaamua kwamba mimi na ndugu yangu mdogo, hatungebatizwa katika kanisa Katoliki.

Francisco Franco alikuwa na ukaribu sana na Kanisa Katoliki

 Mwaka wa 1950, Mashahidi wawili wa Yehova walibisha mlangoni kwetu. Baba aliwasikiliza na akakubali kujifunza Biblia pamoja nao kila juma. Wakati huo nilikuwa na miaka 14 na nilipenda sana kucheza mpira. Baba alijaribu kunitia moyo nisome baadhi ya machapisho ambayo Mashahidi walikuwa wamemwachia, lakini sikutaka kujihusisha na mambo hayo. Alasiri moja nilirudi nyumbani baada ya kucheza mpira, nikamuuliza mama yangu, “Mama, hao walimu wa Biblia wamekuja tena?” Akanijibu: “Ndiyo, wako kwenye chumba cha kulia pamoja na Baba yako.” Niliposikia hivyo, nikakimbia na kurudi tena barabarani!

 Ingawa sikupenda mafundisho ya Biblia, Baba hakuruhusu hilo limvunje moyo. Alipenda sana kweli alizokuwa akijifunza hivi kwamba katika mwaka wa 1953 alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Jambo hilo lilifanya nitake kujua zaidi, basi nikaanza kumuuliza baba maswali mengi. Hata niliomba nakala ya Biblia. Baba alifanya mipango ili Shahidi moja kijana aliyeitwa Máximo Murcia ajifunze Biblia pamoja nami. Miaka miwili baadaye, nikiwa na umri wa miaka 19, nilibatizwa kwenye Mto Jarama ulio mashariki mwa Madrid, nikawa Shahidi wa Yehova.

Kuhubiri Wakati wa Utawala wa Kimabavu wa Franco

 Katika miaka ya 1950, ilikuwa vigumu sana kuhubiri na kufanya mikutano. Francisco Franco, dikteta aliyekuwa akitawala Hispania, alitaka kila mtu nchini awe Mkatoliki. Kwa sababu hiyo, mara nyingi maofisa wa polisi waliwasumbua sana Mashahidi wa Yehova. Tulikutana katika nyumba za Mashahidi mbalimbali na tulijitahidi kuwa makini ili majirani wasiwe na sababu yoyote ya kutushuku na kuturipoti kwa polisi. Vilevile, tulihubiri nyumba kwa nyumba kwa uangalifu sana, tungehubiri kwenye nyumba tatu katika eneo moja na punde baada ya hapo tungeondoka na kwenda kuhubiri eneo tofauti. Watu wengi walisikiliza ujumbe wetu ingawa si wote walioupenda.

Ndugu F. W. Franz alitoa hotuba katika mojawapo ya makusanyiko yetu ya siri

 Nakumbuka siku moja nilibisha mlango na kasisi Mkatoliki alifungua. Nilipomweleza sababu ya kumtembelea, aliniuliza: “Unafanya kazi hii kwa mamlaka ya nani? Unajua ninaweza kukuripoti kwa polisi?” Nilimwambia kwamba tulijua jambo kama hilo lingeweza kutokea. Kisha nikamwambia hivi: “Maadui wa Yesu walijaribu kumfanya akamatwe. Basi si ajabu kwamba wafuasi wake wanaweza kupatwa na hali kama hiyo, sivyo?” Kasisi hakufurahishwa hata kidogo na jibu langu, na akaingia ndani ili awapigie polisi. Sikusubiri, niliondoka hapo mara moja!

 Licha ya hali hizo ngumu, wahubiri nchini Hispania ambao walikuwa mamia kadhaa, walitambua kwamba nchi hiyo ilikuwa tayari kwa mavuno ya kiroho kwa kuwa wengi walisikiliza ujumbe waliohubiri. Niliwekwa rasmi kutumikia nikiwa painia wa pekee a Februari 1956, nikiwa bado na umri wa miaka 19. Ingawa mapainia wengi, kutia ndani mimi, walikuwa vijana na hawakuwa na uzoefu, wamishonari wachache waliokuwepo walituzoeza na kututia moyo. Mimi pamoja na painia mwingine kijana, tulipewa mgawo wa kutumikia katika jiji la Alicante, ambapo kazi ya kuhubiri haikuwa imeanza. Ndani ya miezi michache, tulianzisha mafunzo mengi ya Biblia na tukagawa mamia ya machapisho.

 Bila shaka, watu waliona tulichokuwa tukifanya. Baada ya kuwa jijini Alicante kwa miezi michache tu, maofisa wa polisi walitukamata na kuchukua Biblia zetu. Walitufunga gerezani kwa siku 33, kisha tukapelekwa Madrid, na huko tukaachiliwa. Kifungo hicho cha muda mfupi, kilikuwa mwanzo tu.

Kukabili Hali Ngumu Zaidi Maishani Mwangu

 Nikiwa na umri wa miaka 21, niliagizwa nijiunge na jeshi. Nilipaswa kuripoti kwenye makao ya kijeshi yaliyokuwa katika jiji la Nador. Wakati huo, jiji hilo lilikuwa sehemu ya eneo la kaskazini ya Morocco lililokuwa chini ya ulinzi wa Hispania. Nilipofika huko, kwa heshima, nilieleza msimamo wangu mbele ya ofisa mkuu. Niliwaeleza kwamba singetumikia jeshini wala kuvaa mavazi ya kijeshi. Maofisa wa kijeshi walinipeleka kwenye gereza la Rostrogordo lililo Melilla, ili nisubiri kesi yangu isikilizwe na mahakama ya kijeshi.

Gereza la Rostrogordo, lililo Melilla

 Kabla ya kesi yangu kusikilizwa, mkuu wa jeshi lililokuwa Morocco ambaye alikuwa Mhispania, aliamua kwamba wangenipiga mpaka nibadili msimamo wangu. Kwa hiyo, nilitukanwa, nikacharazwa viboko kwa dakika 20, kisha nikapigwa mateke mpaka nikaanguka chini nikiwa karibu kuzirai. Kapteni aliyesimamia shughuli hiyo alikuwa bado hajaridhika, basi alinikanyaga-kanyaga kichwani kwa viatu vyake vya kijeshi, na aliacha tu alipoona damu ikitiririka. Kisha nilipelekwa ofisini mwake, akaniambia hivi kwa sauti kubwa: “Usifikiri nimemalizana na wewe. Jitayarishe kupigwa hivyo au hata vibaya zaidi kila siku!” Aliwaamuru walinzi wanifungie katika chumba cha gereza kilicho chini ya ardhi. Chumba hicho kilikuwa na unyevunyevu na giza, na kwa kweli ni kana kwamba sikuwa na matumaini yoyote.

 Bado ninakumbuka wakati huo nikiwa nimelala sakafuni kwenye chumba cha gereza, nikiwa na damu kichwani. Sikuwa na chochote ila blanketi moja nyepesi na chumbani humo mlikuwa na panya wachache waliotokea mara kwa mara. Kile tu nilichoweza kufanya ni kusali kwa Yehova anipe nguvu na uvumilivu. Nikiwa kwenye gereza hilo la chini ya ardhi lenye giza na baridi, nilisali tena na tena. b

 Siku iliyofuata, nilipigwa tena, mara hii nilipigwa na ofisa mwingine. Kapteni alitazama ili kuhakikisha nimepigwa vya kutosha. Ni lazima nikiri kwamba nilianza kujiuliza ikiwa ningeweza kuvumilia kipigo kama hicho tena. Usiku huo wa pili nikiwa kwenye chumba cha gereza, nilimsihi Yehova anisaidie.

 Siku ya tatu, niliitwa tena kwenye ofisi ya kapteni. Nilifikiri walitaka kunipiga tena. Nilipokuwa nikiingia ofisini humo, nilisali kwa Yehova. Don Esteban c, katibu wa mahakama ya kijeshi, alikuwa akinisubiri. Alikuwa amekuja kuanzisha kesi dhidi yangu.

 Don Esteban alipoona bendeji zilizokuwa kichwani mwangu, aliniuliza kilichotokea. Nilisita kwa sababu niliogopa nitapigwa tena, lakini nilimwambia ukweli. Don Esteban aliposikia habari hizo alisema: “Sina uwezo wa kuondoa mashtaka yanayokukabili. Lakini unaweza kuwa na uhakika kwamba hakuna mtu atakayekupiga tena.”

 Kama tu alivyoahidi, hakuna mtu aliyethubutu kunigusa tena katika kipindi chote nilichokuwa gerezani. Sikuwahi kujua kwa nini katibu huyo, alichagua kuzungumza nami siku hiyo. Kile ninachojua ni kwamba sala zangu zilijibiwa kwa njia ya pekee. Nilijionea jinsi Yehova alivyoniokoa nilipokabili hali ngumu zaidi maishani mwangu na hakuruhusu niteswe kupita nilivyoweza kuhimili. (1 Wakorintho 10:13) Nilikabili kesi yangu nikiwa na tumaini hakika katika Yehova.

Nikiwa kwenye gereza la Ocaña

 Nilipewa kifungo cha miaka 19 gerezani, kisha nikaongezewa miaka mingine mitatu kwa sababu ya “kutotii.” Baada ya kukaa gerezani kwa miezi 15 huko Morocco, nilihamishiwa kwenye Gereza la Ocaña, karibu na Madrid, ili niendelee kutumikia kifungo kilichobaki humo. Kupelekwa Ocaña kulikuwa baraka kutoka kwa Yehova. Nilihisi ni kana kwamba niko paradiso, nilipolinganisha hali katika gereza hili na hali zilivyokuwa katika gereza la Rostrogordo. Chumba changu cha gereza kilikuwa na kitanda, godoro, na mashuka pia. Baada ya muda nilipewa kazi ya uhasibu gerezani. Hata hivyo, nilikuwa mpweke sana kwa sababu ya kukaa gerezani kwa muda mrefu. Mojawapo ya majaribu makubwa zaidi niliyokabili, ni kukosa ushirika wa ndugu zangu wa kiroho.

 Wazazi wangu walinitembelea mara kwa mara, lakini nilihisi kwamba nilihitaji faraja nyingi zaidi. Waliniambia kwamba ndugu wengine pia walikuwa wamesimama imara na kukataa kujiunga na jeshi. Basi nikasali kwa Yehova, nikamwomba ampe angalau ndugu mmoja mgawo wa kuja kwenye gereza nililokuwa. Kwa mara nyingine tena, Yehova alijibu sala zangu za kutoka moyoni kwa njia kubwa kuliko nilivyotarajia. Baada ya muda mfupi, ndugu watatu waaminifu—Alberto Contijoch, Francisco Díaz, na Antonio Sánchez—waliletwa kwenye gereza la Ocaña ambamo nilikuwa. Baada ya kuwa peke yangu kwa miaka minne, sasa hatimaye nilipata ushirika mzuri wa kiroho. Sote wanne tulisoma pamoja na pia kuwahubiria wafungwa wenzetu.

Kuachiliwa Huru na Kuirudia Kazi

 Hatimaye, katika mwaka wa 1964, nilipewa msamaha na nikaachiliwa mapema. Kifungo changu cha miaka 22 kilikuwa kimefupishwa kikawa miaka 6 na nusu tu. Siku ambayo niliachiliwa kutoka gerezani, nilihudhuria mkutano. Ingawa nililazimika kutumia pesa kidogo nilizokuwa nazo ili kulipa nauli ya hadi Madrid, nilifika mkutanoni kwa wakati. Nilifurahia sana kuwa na akina ndugu tena! Ingawa nilifurahia sana kushirikiana tena na akina ndugu, nilitaka pia kuanza upainia mapema iwezekanavyo. Licha ya kwamba polisi bado walikuwa wakiwasumbua ndugu na dada, watu kwa ujumla waliitikia vizuri habari njema, na kulikuwa na kazi kubwa ya kufanya.

 Katika kipindi hicho nilikutana na Mercedes, dada kijana mwenye bidii aliyetumikia akiwa painia wa pekee. Mercedes alikuwa dada mnyenyekevu na alijitahidi kadiri ya uwezo wake kumhubiria kila mtu. Isitoshe alikuwa mwenye fadhili na mkarimu, nami nilivutiwa sana naye kwa sababu ya sifa hizo. Sote tulipendana, kwa hiyo, baada ya mwaka mmoja, tulifunga ndoa. Kwa kweli nimebarikiwa sana kuwa pamoja na mke wangu, Mercedes.

Nikiwa pamoja na Mercedes muda mfupi baada ya kufunga ndoa

 Miezi kadhaa baada ya kufunga ndoa tulialikwa kutumikia katika kazi ya kuzunguka. Tulitembelea kutaniko tofauti kila juma, na tulishirikiana na akina ndugu kwenye mikutano na pia tulihubiri pamoja. Kulikuwa na makutaniko mengi mapya nchini Hispania, na akina ndugu walihitaji msaada na kutiwa moyo. Kwa kipindi kifupi, nilipata pia pendeleo la kusaidia kazi siku kadhaa kwa juma, kwenye ofisi ya siri ya Mashahidi wa Yehova iliyokuwa Barcelona.

 Katika mwaka wa 1967, hali ilibadilika na hatukulazimika kuabudu tena kisiri. Wakati huo serikali ilipitisha sheria iliyowapa raia wote wa Hispania uhuru wa ibada. Hatimaye katika mwaka wa 1970, Mashahidi wa Yehova walitambuliwa kisheria. Sasa, tungeweza kukutana kwa uhuru, kuwa na Majumba ya Ufalme, na hata kufungua rasmi ofisi ya tawi.

Migawo Mipya ya Kitheokrasi

 Katika mwaka wa 1971, mimi na Mercedes tulialikwa kuwa washiriki wa kudumu wa ofisi ya tawi jijini Barcelona. Hata hivyo, mwaka mmoja baadaye, Mercedes alipata mimba na kujifungua mtoto mrembo wa kike, na tukampa jina, Abigail. Kwa sababu hiyo hatungeweza kuendelea kutumikia Betheli, hata hivyo, tulikuwa tumepata mgawo mpya, yaani, wa kumlea binti yetu.

 Abigail alipofikia umri wa utineja, ofisi ya tawi ilituomba kurudia kazi ya kuzunguka tena ikiwa ingewezekana. Kama ilivyo kikawaida, tulisali kuhusu jambo hilo na pia tuliomba ushauri kutoka kwa ndugu wakomavu. Mzee mmoja aliniambia: “Jesús, ikiwa wanakuhitaji tena kwenye kazi ya kuzunguka, lazima ukubali.” Basi tukaanza kipindi kingine kizuri maishani. Mwanzoni tulitembelea makutaniko yaliyokuwa karibu na nyumbani ili tuendelee kumtunza Abigail. Bila shaka, baada ya muda binti yetu alikua na akawa mtu mzima na hivyo angeweza kuishi mwenyewe na hilo lilitupatia fursa ya kupanua utumishi wetu wa pekee wa wakati wote.

 Mimi na Mercedes tulitumikia katika kazi ya kuzunguka kwa miaka 23. Nilifurahia sana pendeleo hilo, kwa sababu lilinipa fursa ya kuwatia moyo vijana kwa mambo niliyopitia. Pindi fulani nilitumikia nikiwa mwalimu wa shule za kitheokrasi zilizohudhuriwa na wazee na watumishi wa wakati wote, na katika pindi hizo tuliishi kwenye Betheli ya Madrid. Inapendeza kwamba, kilometa tatu tu kutoka Betheli ndipo unapopita Mto Jarama, mto ambamo nilibatizwa mwaka wa 1955. Singewahi kuwazia kwamba, miongo mingi baadaye ningerudi kwenye eneo hilo ili kuwasaidia ndugu na dada vijana kujiandaa kwa ajili ya majukumu zaidi katika utumishi wa Yehova.

Nikifundisha kwenye shule ya kitheokrasi

 Tangu mwaka wa 2013 tulianza tena kutumikia tukiwa mapainia wa pekee. Ninakiri kwamba haikuwa rahisi kukabiliana na mabadiliko ya kuacha kazi ya kuzunguka na kuanza upainia, lakini tumejionea kwamba badiliko hilo lilikuwa jambo sahihi. Hivi karibuni nimekuwa na matatizo ya kiafya, na hata nilifanyiwa upasuaji tata sana wa moyo. Katika hali hizo pia nimemtegemea Yehova, na kama kawaida yake, hajaniacha. Na kwa miaka 56 sasa, mke wangu mshikamanifu, Mercedes, amenitegemeza sana, na amekuwa mwandamani mwaminifu katika migawo yangu yote ya kitheokrasi.

 Mara nyingi mimi hukumbuka pindi niliyokuwa mwalimu. Ninakumbuka nyuso za wanafunzi, vijana ambao walikuwa tayari kujifunza. Utayari wao ulinikumbusha ujana wangu mwenyewe na bidii niliyokuwa nayo nilipoanza maisha ya utumishi mtakatifu. Kwa kweli nilipitia hali ngumu sana, lakini pia nilifurahia mambo mengi mazuri. Hata majaribu magumu yalinifunza masomo muhimu. Somo muhimu zaidi ya yote ni kwamba, sipaswi kamwe kutegemea nguvu zangu mwenyewe. Majaribu yangu yalinipa fursa ya kuuona mkono wenye nguvu wa Yehova, na mkono huo umenitia nguvu siku zote, hata nilipokabili hali ngumu zaidi maishani mwangu.​—Wafilipi 4:13.

Mimi na Mercedes tunaendelea kutumikia tukiwa watumishi wa wakati wote

a Painia wa pekee ni mtumishi wa wakati wote anayejitolea kutumwa katika eneo lolote ambalo ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova imetambua kwamba kuna uhitaji wa walimu wa Biblia.

b Chumba hicho cha gereza chenye ukubwa wa mita nne tu za mraba, hakikuwa na choo, na nilikaa humo kwa miezi saba. Nililala sakafuni na nilikuwa na blanketi moja tu.

c “Don” ni jina la heshima linalotumiwa katika nchi zinazozungumza Kihispania, na linatajwa kabla ya jina la kwanza la mtu.