Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MILTIADIS STAVROU | SIMULIZI LA MAISHA

“Tumejionea Yehova Akitutunza na Kutuongoza”

“Tumejionea Yehova Akitutunza na Kutuongoza”

Nilipokuwa na umri wa miaka 13 hivi, mimi na watoto wengine wa umri wangu tulifurahia kutazama magari machache yaliyopita karibu na nyumbani kwetu huko Tripoli, Lebanon. Nilivutiwa na gari moja hasa. Lilikuwa gari jekundu lililotengenezewa Marekani ambalo lilimilikiwa na mwanamume kutoka Syria. Basi unaweza kuelewa kwa nini nilishangaa kasisi wa Kanisa Othodoksi la eneo letu alipotuambia tulipige mawe gari hilo kwa sababu mmiliki wake alikuwa Shahidi wa Yehova!

 Tulimwambia kasisi huyo kwamba tukifanya hivyo tutamuumiza dereva. Alituambia: “Muueni. Kisha mtumie joho langu kufuta damu kutoka kwenye mikono yenu!” Ingawa nilijivunia kuzaliwa katika familia ya dini ya Othodoksi ya Ugiriki, maneno hayo yenye hasira yalinifanya baadaye niache kuwa mshiriki wa dini hiyo. Ninapofikiria kisa hicho, ninatambua kwamba kilinisaidia kupata kweli kumhusu Yehova.

Kupata Kweli Kumhusu Yehova

 Nilipokuwa mtoto, jiji la bandarini la Tripoli lilikuwa na watu wengi sana kutoka tamaduni, lugha, na dini mbalimbali. Kila familia ilijivunia utamaduni wake, kama tu familia yetu. Mimi na ndugu zangu wakubwa tulijiunga na kikundi kilichoitwa Wanajeshi wa Imani, a ambao waliwapinga Mashahidi wa Yehova. Hatukuwa tumewahi kukutana na Mashahidi, lakini kasisi wetu alituambia kwamba walikuwa genge lililopinga Kanisa Othodoksi la Ugiriki na kiongozi wao aliitwa Yehova. Kasisi huyo alituambia tena na tena kwamba tunapaswa kuwashambulia Mashahidi wakati wowote tunapokutana nao.

 Ingawa sikujua, watatu kati ya ndugu zangu tayari walikuwa wamekutana na Mashahidi wa Yehova. Lakini badala ya kuwashambulia, ndugu zangu walikubali kujifunza Biblia pamoja nao ili kuthibitisha mafundisho yao yana kasoro. Jioni moja, nilirudi nyumbani na kuwakuta Mashahidi wengi sebuleni kwetu wakizungumzia Biblia na familia yetu na majirani kadhaa. Nilikasirika! Ndugu zangu wangewezaje kuisaliti dini ya Othodoksi? Nilikuwa karibu kuondoka lakini jirani mmoja, ambaye alikuwa daktari maarufu wa meno na ambaye pia alikuwa Shahidi, akaniambia niketi na kusikiliza. Rafiki mmoja wa familia yetu alikuwa akisoma kwa sauti Zaburi 83:18 kutoka kwenye Biblia yangu mwenyewe. Papo hapo nikagundua kwamba kasisi wetu alikuwa ametudanganya. Yehova hakuwa kiongozi wa genge fulani—alikuwa ndiye Mungu wa pekee wa kweli!

Muda mfupi baada ya ubatizo wangu

 Nilitaka kujua mengi zaidi kumhusu Yehova, kwa hiyo nikaanza kuhudhuria funzo la Biblia nyumbani kwetu, ambalo liliongozwa na Ndugu Michel Aboud. Siku moja, rafiki yangu aliuliza swali ambalo lilikuwa limenitatiza tangu nilipokuwa mvulana. Aliuliza hivi, “Tuambie, ni nani aliyemuumba Mungu?” Ndugu Aboud alituambia tumtazame paka aliyekuwa amelala kwenye kiti. Alitueleza kwamba paka hawawezi kuelewa maneno ambayo wanadamu wanasema na jinsi tunavyofikiri. Vivyo hivyo, hatuwezi kuelewa mambo mengi kumhusu Mungu. Mfano huo rahisi ulinisaidia kuelewa kwa nini kuna mambo fulani kumhusu Yehova ambayo sikuweza kuelewa kikamili. Muda mfupi baadaye, nilijiweka wakfu kwa Yehova Mungu na kubatizwa mwaka wa 1946 nilipokuwa na umri wa miaka 15.

Upainia Unanisaidia Kuwa na Kusudi Maishani

 Mwaka wa 1948, nilianza kufanya kazi na ndugu yangu Hanna katika biashara yake ya kupiga picha. Duka lake lilikuwa karibu na duka la picha zilizochorwa lililomilikiwa na ndugu anayeitwa Najib Salem. b Najib alihubiri bila woga hadi alipokufa akiwa na umri wa miaka 100. Nilipoandamana naye kuhubiri katika vijiji mbalimbali, ningeweza kuona ujasiri wake licha ya upinzani. Pia, ni kana kwamba angeweza kuanzisha mazungumzo ya Biblia na mtu yeyote, hata iwe alikuwa wa dini gani. Bidii yake ilinichochea sana.

Najib Salem (safu ya nyuma, kulia) amenichochea maisha yangu yote

 Siku moja, tulipokuwa kazini, tulitembelewa na Mary Shaayah, dada mwenye asili ya Lebanon aliyeishi Marekani. Mbali na kuwa mama mwenye shughuli nyingi, alikuwa pia painia mwenye bidii. Maisha yangu yalibadilika siku hiyo. Mary alitueleza mambo aliyojionea katika kazi ya kuhubiri kwa zaidi ya saa mbili. Kabla ya kuondoka, Mary alinitazama na kuniuliza: “Milto, kwa kuwa wewe ni mseja, mbona usiwe painia?” Nilisema kwamba nisingeweza kwa kuwa nilihitaji kujipatia riziki. Kisha akaniuliza: “Nimekuwa hapa pamoja nanyi kwa muda gani asubuhi hii?” Nilijibu: “Kwa muda wa saa mbili hivi.” Mary akasema: “Sijaona ukifanya kazi katika muda huo. Ukihubiri kwa muda kama huo kila siku, unaweza kuwa painia. Kwa nini usijaribu kwa mwaka mmoja tu kisha uamue ikiwa utaendelea au la?”

 Ingawa wanaume katika utamaduni wangu hawangesikiliza ushauri kutoka kwa mwanamke, pendekezo lake lilisikika kuwa linafaa. Januari 1952, miezi miwili baadaye, nilianza utumishi wa upainia. Miezi 18 hivi baadaye, nilipokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 22 la Shule ya Gileadi.

Familia na marafiki walikuja kuniaga nilipokuwa nikienda Shule ya Gileadi mwaka wa 1953

 Baada ya kuhitimu, nilitumwa Mashariki ya Kati. Mwaka mmoja hivi baadaye, nilifunga ndoa na Doris Wood, mmishonari mchangamfu kutoka Uingereza ambaye pia alikuwa akitumikia katika Mashariki ya Kati.

Kuhubiri Kweli za Biblia Nchini Syria

 Muda mfupi baada ya harusi yetu, mimi na Doris tulipewa mgawo jijini Aleppo, Syria. Kwa kuwa kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku nchini humo, tulijifunza Biblia hasa na watu tuliokuwa tumeelekezwa kwao kihususa.

 Siku mmoja, tulimtembelea mwanamke ambaye alipendezwa kujifunza Biblia. Alikuwa na wasiwasi mwingi alipofungua mlango naye akatuambia: “Muwe waangalifu! Polisi wametoka hapa sasa hivi. Walitaka kujua mnaishi wapi.” Ni wazi kwamba majasusi walijua mahali ambapo tuliongoza mafunzo ya Biblia. Tuliwasiliana na ndugu waliosimamia kazi katika Mashariki ya Kati, nao walitushauri tuondoke nchini haraka iwezekanavyo. Ingawa tulisikitika kuwaacha wanafunzi wetu wa Biblia, tulihisi Yehova akitulinda kwa upendo.

Tulijionea Yehova Akituongoza Nchini Iraq

 Mwaka wa 1955, tulipewa mgawo mpya jijini Baghdad, Iraq. Ingawa tulikuwa huru kuwahubiria watu wote kwa busara nchini Iraq, tulikazia fikira kuwahubiria Wakristo hasa.

Nikiwa na wamishonari wenzangu nchini Iraq

 Pia, tulijaribu kuanzisha mazungumzo ya kirafiki na Waislamu tulipokuwa sokoni au barabarani. Mara nyingi, Doris alisema mambo ambayo yangewavutia watu aliokutana nao. Kwa mfano, alisema hivi: “Sikuzote baba yangu alikuwa akiniambia sisi sote tutasimama mbele ya Muumba wetu.” (Waroma 14:12) Kisha angesema: “Maneno hayo yamenisaidia sana maishani mwangu. Una maoni gani kuyahusu?”

 Tulifurahia mgawo wetu wa miaka mitatu hivi jijini Baghdad, tukiwasaidia ndugu wenyeji kupanga kazi ya kuhubiri kwa busara. Tulifanya mikutano ya lugha ya Kiarabu kwenye makao yetu ya wamishonari. Tulifurahi sana kuwakaribisha watu wanyoofu kutoka katika jamii ya Waashuru, kabila linalofanyizwa hasa na watu wanaodai kuwa ni Wakristo. Walipojionea upendo na umoja kwenye mikutano yetu, walitambua kwamba sisi ni wanafunzi wa kweli wa Yesu.​—⁠Yohana 13:35.

Tulifanya mikutano katika makao ya wamishonari huko Baghdad

 Nicolas Aziz alikuwa mmoja kati ya watu waliokubali haraka ujumbe wetu wa amani. Alikuwa mwanamume mpole na mnyenyekevu, aliyependa familia yake, na ambaye alikuwa na asili ya Kiarmenia na ya Kiashuru. Nicolas na mke wake, Helen, walikubali haraka kile ambacho Biblia inafundisha kumhusu Yehova na mwana wake, Yesu—⁠kwamba wao ni watu wawili tofauti. (1 Wakorintho 8:5, 6) Bado ninakumbuka siku ambayo Nicolas na watu wengine 20 walipobatizwa katika Mto Efrati.

Tunajionea Yehova Akitusaidia Nchini Iran

Mwaka wa 1958 nchini Iran

 Mfalme Faisal wa Pili alipouawa Julai 14, 1958 baada ya mapinduzi ya kijeshi nchini Iraq, tulifukuzwa kutoka nchini humo na kupelekwa Iran. Tuliendelea kuwahubiria wageni kwa tahadhari nchini humo kwa miezi sita hivi.

 Kabla tu ya kuondoka Tehran, mji mkuu wa Iran, nilipelekwa kwenye kituo cha polisi kuhojiwa. Hilo lilinifanya nitambue kwamba polisi walikuwa wakitutazama kila wakati. Baada ya mahojiano hayo, niliwasiliana na Doris na kumwambia kwamba polisi walikuwa wakitutazama. Tulikubaliana kwamba ili tuwe salama, sikupaswa kurudi nyumbani, wala hatukupaswa kuwa pamoja kwa muda mfupi hadi tutakapoondoka nchini humo.

 Doris alitafuta mahali salama pa kuishi akisubiri muda tutakapokutana kwenye uwanja wa ndege. Lakini angefauluje kufika uwanjani bila polisi kumwona? Doris alisali kwa Yehova kuhusu jambo hilo.

 Ghafla, mvua kubwa ikaanza kunyesha, na kila mtu akakimbia kutafuta mahali pa kujikinga, kutia ndani polisi. Kwa kuwa barabara hazikuwa na mtu, Doris angeweza kuondoka. Doris anasema hivi, “Mafuriko hayo yalikuwa muujiza!”

 Baada ya kuondoka Iran, tulipewa mgawo katika eneo lingine, ambako tuliwahubiria watu wa makabila na dini mbalimbali. Kufikia mwaka wa 1961, nilitumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko, na tuliwatembelea waabudu wenzetu katika maeneo mbalimbali ya Mashariki ya Kati.

Tulijionea Roho ya Yehova Ikitenda

 Mara nyingi sana nilijionea jinsi roho takatifu ya Mungu ilivyowaunganisha watu katika utumishi wetu tukiwa Mashariki ya Kati. Bado ninakumbuka mazungumzo yenye uchangamfu niliyokuwa nayo nilipojifunza Biblia na Wapalestina wawili, Eddy na Nicolas. Wote wawili walifurahia kuhudhuria mikutano yetu, lakini baada ya muda waliacha kujifunza Biblia kwa sababu ya msimamo wao mkali wa kisiasa. Nilisali Yehova afungue mioyo yao. Walipotambua kwamba Mungu angesuluhisha matatizo, si ya Wapalestina tu bali ya wanadamu wote, waliamua kuanza tena kujifunza. (Isaya 2:4) Waliacha mawazo yao ya kizalendo na wakabatizwa. Baadaye Nicolas akawa mwangalizi wa mzunguko mwenye bidii.

 Tulipotembelea nchi moja baada ya nyingine, mimi na Doris tulivutiwa na uaminifu wa ndugu zetu, licha ya hali walizokuwa wakikabili. Kwa kuwa walikuwa wakivumilia matatizo mengi, niliazimia kuwafariji wakati wa ziara zangu nikiwa mwangalizi wa mzunguko. (Waroma 1:11, 12) Ili kufaulu, sikuzote nimejitahidi kujikumbusha kwamba mimi si bora kuliko ndugu na dada zangu. (1 Wakorintho 9:22) Nilifurahia sana kuwatia moyo waabudu wenzangu waliohitaji msaada.

 Limekuwa jambo lenye kufurahisha sana kuwaona wengi kati ya wale tuliojifunza Biblia pamoja nao wakiwa watumishi waaminifu wa Yehova. Baadhi yao walihamia nchi za ng’ambo pamoja na familia zao ili kuepuka vita nchini kwao. Lakini wamekuwa msaada mkubwa kwa wale wanaotumikia katika makutaniko ya lugha ya Kiarabu nchini Australia, Kanada, barani Ulaya, na Marekani. Katika miaka ya karibuni, baadhi ya watoto wao ambao ni watu wazima wamerudi Mashariki ya Kati ili kutumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri jasiri. Ni shangwe kubwa kwangu na kwa Doris kuwa na watoto na wajukuu wengi sana wa kiroho.

Kumtegemea Yehova Milele

 Katika maisha yetu yote, tumejionea Yehova akitutunza na kutuongoza kwa njia nyingi. Ninashukuru sana kwamba alinisaidia kuondoa ubaguzi na uzalendo niliokuwa nao nilipokuwa kijana. Mazoezi niliyopata kutoka kwa waamini wenzangu wenye ujasiri na wasio na ubaguzi yalinitayarisha kushiriki kweli za Biblia na watu kutoka malezi mbalimbali. Mimi na Doris tuliposafiri kutoka nchi moja hadi nyingine tulikabili changamoto nyingi na pindi fulani hatukujua tutakabili hali zipi. Lakini hilo lilitufundisha tusijitegemee bali tumtegemee Yehova Mungu kikamili.​—Zaburi 16:8.

 Ninapofikiria makumi ya miaka ambayo nimemtumikia Yehova, ninatambua kwamba Baba yangu wa mbinguni amenibariki sana. Ninakubaliana na mke wangu mpendwa Doris, ambaye mara nyingi anasema kwamba hakuna kitu kinachopaswa kutuzuia kumtolea Yehova ujitoaji kamili, hata ikiwa tutakabili kifo! Sikuzote tutaendelea kumshukuru Yehova kwa kuturuhusu tushiriki kueneza ujumbe wa amani katika Mashariki ya Kati. (Zaburi 46:8, 9) Tunatazamia wakati ujao tukiwa na uhakika, tukijua kwamba Yehova ataendelea kuwaongoza na kuwalinda wote wanaomtegemea.​—Isaya 26:3.

a Ili kupata habari zaidi kuhusu kikundi hiki, ona Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova—1980, ukurasa wa 186-188, cha Kiingereza.

b Simulizi la maisha la Najib Salem lilichapishwa katika toleo la Septemba 1, 2001 la Mnara wa Mlinzi, ukurasa wa 22-26.