Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 KUHUBIRI NA KUFUNDISHA DUNIANI KOTE

Amerika

Amerika
  • IDADI YA NCHI 57

  • IDADI YA WATU 970,234,987

  • IDADI YA WAHUBIRI 3,943,337

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 4,341,698

Waliwakaribisha Nyumbani Kwao

Jijini Las Vegas, Nevada, wenzi fulani wa ndoa ambao si Mashahidi walitaka kuishi mahali patulivu, kwa hiyo waliuza nyumba yao ili wahamie katika Jamhuri ya Dominika. Hata hivyo, ilibidi wahame nyumba hiyo siku kumi kabla ya tarehe ya kuondoka. Majirani wao ambao ni Mashahidi wa Yehova waliwasaidia kwa kuwakaribisha wenzi hao ili waishi nyumbani kwao. Walipokuwa wakiishi na Mashahidi hao, walihudhuria  mkutano katika Jumba la Ufalme. Walishangaa na kuvutiwa sana waliposikia mwaka 1914 ukitajwa. Walijua kwamba huo ulikuwa mwaka muhimu katika historia ya ulimwengu. Wenzi hao walipowasili katika Jamhuri ya Dominika, waliwaomba Mashahidi wa kwanza kuwatembelea wawafundishe Biblia. Miezi 14 baadaye, walijiweka wakfu na kubatizwa.

Hiyo Ndiyo Habari Aliyohitaji Hasa

Akina ndugu waliweka kibanda cha machapisho kwenye Maonyesho ya Kimataifa ya Vitabu ya Mwaka wa 2012 katika jiji la Panama City, Panama. Wasichana wawili walitembelea kibanda hicho. Mmoja wao alimwambia dada aliyekuwa kwenye kibanda hicho kwamba kuna jambo lililokuwa likimhangaisha. Alimweleza kwamba baba yake alikuwa mraibu wa dawa za kulevya na msichana huyo hakujua jinsi ya kushughulikia tatizo hilo. Dada yetu alimwonyesha sura ya 23 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, “Nifanye Nini Ikiwa Mzazi Wangu ni Mraibu wa Dawa za Kulevya au Pombe?” Msichana huyo alisema hivi kwa furaha: “Hii ndiyo habari ninayohitaji hasa!” Wasichana hao walimkumbatia dada yetu na baada ya saa moja wakarudi tena kumshukuru. Katika siku tano za maonyesho hayo, akina ndugu waliwaachia watu vitabu 1,046, magazeti 1,116, na broshua 449. Watu 56 waliacha anwani zao ili watembelewe na Mashahidi.

Alihubiri Peke Yake kwa Miaka Minne

Fredy ambaye lugha yake ya asili ni Cabecar, anaishi katika kijiji kimoja kilicho kwenye eneo la mbali milimani nchini Kosta Rika. Miaka minne hivi iliyopita alipokuwa  akifanya kazi katika mji mkuu, San José, Fredy alipewa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? na broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Mhubiri aliyempa machapisho hayo alimwambia aende kijijini kwao na kuwahubiria watu, hivyo akarudi kijijini. Fredy alijifunza mwenyewe kitabu Biblia Inafundisha na kufanya mabadiliko katika maisha yake, kama vile kuhalalisha ndoa yake. Kisha alijitahidi sana kuwafundisha kweli watu wanaozungumza lugha ya Cabecar.

Fredy alipanga madarasa ya kuwafundisha watu Biblia. Alikuwa na madarasa sita, na kuwapanga wanafunzi kulingana na matokeo ya mtihani aliowapa ili kutahini ujuzi wao wa Biblia. Aliongoza mikutano na hata akaadhimisha Ukumbusho. Aliandika mwenyewe mialiko ya Ukumbusho iliyosema: “Mashahidi wa Yehova wanakualika uhudhurie Ukumbusho wa kifo cha Kristo pamoja nao.” Alifanya mambo yote hayo kwa miaka minne bila kuwasiliana na Mashahidi! Wakati huohuo alimwomba Yehova awatume Mashahidi ili waende kumsaidia.

Hivi karibuni, sala ya Fredy ilijibiwa. Mashahidi fulani walifunga safari ngumu ya kutembelea kijiji hicho na wakashangaa kuona mambo ambayo Fredy alikuwa ametimiza. Walisema hivi: “Ingawa Fredy si Shahidi aliyebatizwa, anaishi kama Shahidi!” Baada ya miezi mitatu tu, alikubaliwa kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Ili abatizwe, ilimbidi ateremke mlima na kuhudhuria kusanyiko lake la kwanza la wilaya akiandamana na watu 19 anaowafundisha Biblia. Sasa anajifunza Biblia na vikundi vitatu zaidi vya wazungumzaji wa lugha ya Cabecar vilivyo katika vijiji vya mbali zaidi.

Costa Rica: Fredy, ambaye sasa ni painia wa kawaida, husafiri hadi maeneo ya mbali ili kuongoza mafunzo ya Biblia

Alitetea Imani Yake Shuleni

Siku moja Anna, mwanafunzi wa sekondari nchini Marekani, alilazimika kutetea imani yake mbele ya wanafunzi wenzake kadhaa ambao waliudhika waliposikia kwamba  haamini fundisho la Utatu. Anna anasema hivi: “Walianza kunizomea, lakini nilikuwa mtulivu kwa kuwa sikutaka watazamaji wawe na maoni mabaya kuwahusu Mashahidi wa Yehova.” Usiku huo alimwomba Yehova ampe ujasiri na akafanya utafiti kuhusu fundisho la Utatu. Siku iliyofuata, Anna alienda shuleni na Biblia yake. Wanafunzi wenzake walimzunguka, wengi wao wakicheka kichinichini. Hata hivyo, kwa ujasiri, aliwaonyesha maandiko kadhaa na kujadiliana nao. Mwishowe, wale waliokuwa wakibishana naye wakanyamaza. Baada ya mazungumzo hayo, mpinzani mkuu ambaye pia alikuwa kiongozi wa darasa alikiri kwamba sasa anawaheshimu Mashahidi wa Yehova. Kipindi chote cha mwaka wa masomo, alimwuliza Anna maswali mengi kuhusu imani yake.

Kiatu Kilikatika kwa Wakati Unaofaa

Jumapili moja asubuhi nchini Barbados, kiatu cha msichana fulani kilikatika alipokuwa akienda kanisani. Msichana huyo alienda kwenye nyumba iliyokuwa karibu na  akaomba pini ya kubana kiatu hicho. Kwa tukio zuri, hiyo ilikuwa nyumba ya dada mmoja Shahidi na binti yake. Msichana huyo alipokuwa akirekebisha kiatu chake, dada alimweleza jinsi ambavyo unabii wa Biblia unatimizwa leo. Kisha binti ya dada huyo akamwalika ahudhurie mikutano pamoja nao kwenye Jumba la Ufalme asubuhi hiyo. Kwa kuwa tayari alikuwa amechelewa kuhudhuria ibada kanisani, msichana huyo alikubali mwaliko. Wakati wa mkutano, alifungua maandiko yote katika Biblia yake ya tafsiri ya King James. Programu yote ilimgusa sana moyo. Alisema kwamba alikuwa amechoka kusikia kelele za ngoma na za watu kanisani, na sikuzote alitamani kujifunza Biblia katika mazingira matulivu. Alikubali kujifunza Biblia kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha. Anahudhuria mikutano yote na kushiriki kwa uchangamfu.

Ni Mtu Mmoja tu Anayeweza Kumzuia Kuhubiri

Ndugu mmoja nchini Guyana anasimulia hivi: “Ninapenda kuwahubiria wanafunzi wenzangu shuleni, lakini kuna kijana mmoja ambaye hapendi kuniona nikihubiri. Siku moja alinibana ukutani na kuniambia, ‘Acha kuhubiri!’ Nilimjibu kwamba ni Yehova peke yake anayeweza kunizuia kuhubiri. Nilipoendelea kuhubiri, kijana huyo alikata mkoba wangu. Kisha akanipiga ngumi usoni, na kunijeruhi mdomoni. Sote tuliitwa kwenye ofisi ya mwalimu mkuu, ambaye aliniuliza kwa nini kijana huyo alinipiga ngumi usoni. Nilimjibu kwamba alinipiga kwa sababu nilikuwa nikihubiri habari njema. Mwalimu mkuu aliniuliza kwa nini sikulipiza kisasi, hata akaniambia kwamba nilipaswa kumpiga pia. Nilimwambia kwamba nilikuwa nimejifunza kwenye Waroma 12:17 kwamba Wakristo hawapaswi ‘kumlipa yeyote uovu kwa uovu.’ Aliposikia hilo, mwalimu mkuu aliniruhusu niondoke na kusema kwamba angemshughulikia kijana aliyenipiga.”

Catamarca, Argentina