Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 KUHUBIRI NA KUFUNDISHA DUNIANI KOTE

Asia na Mashariki ya Kati

Asia na Mashariki ya Kati
  • IDADI YA NCHI 47

  • DADI YA WATU 4,282,178,221

  • IDADI YA WAHUBIRI 674,011

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 672,318

Mwanaume Kipofu, Kiziwi, na Bubu Apata Msaada

Mwaka wa 1999, kutaniko la lugha ya ishara jijini Kobe, Japani, lilipata habari kwamba kuna mwanaume kiziwi anayeitwa Hirofumi. Ndugu mmoja alipomtembelea Hirofumi, mama yake alimzuia kumwona. Ndugu huyo aliwatembelea tena na tena na kumsihi mama ya Hirofumi amruhusu kumwona, hatimaye akamleta mlangoni. Nywele na ndevu zake  zilikuwa ndefu na hazikuwa zimechanwa. Alionekana kama mtu aliyekuwa ameachwa peke yake kwenye kisiwa fulani kwa miaka mingi. Uso wake haukuonyesha hisia zozote. Hirofumi alikuwa kiziwi na pia kipofu. Ingawa ndugu huyo alishtuka alipomwona Hirofumi, alichukua mkono wake na kuanza kumfanyia ishara mikononi mwake. Hakuitikia kwa njia yoyote ile. Hirofumi alikuwa ametengwa na watu na hakuwa amewasiliana na mtu yeyote tangu alipopoteza uwezo wake wa kuona miaka 10 iliyopita akiwa na umri wa miaka 31.

Yule ndugu alimtembelea tena siku mbili baadaye. Mama ya Hirofumi alishangaa, kwa kuwa alidhani kwamba ndugu huyo angekata tamaa baada ya kuona hali ya mwana wake. Kwa mara nyingine tena, ndugu huyo alimsihi mama ya Hirofumi amruhusu amwone mwana wake, naye akamleta mlangoni. Baada ya kumtembelea Hirofumi kwa mwezi mmoja bila matokeo yoyote, mama yake alimwambia ndugu huyo asijisumbue kuwatembelea tena. Hata hivyo, ndugu huyo aliendelea kuwatembelea. Aliwapelekea keki na kuonyesha kwa njia mbalimbali kwamba anawajali. Baada ya kuwatembelea tena kwa miezi mingine miwili bila mafanikio, ndugu huyo alihisi kwamba jitihada zake zimegonga mwamba.

Ndugu huyo aliamua kuwatembelea kwa mara ya mwisho. Kabla ya kufanya hivyo, alimwomba Yehova amsaidie kuamua ikiwa anapaswa kuendelea kumtembelea Hirofumi. Ndugu huyo alipofika nyumbani kwa akina Hirofumi, alichukua mkono wake na kumfanyia ishara ya kwamba kuna Mungu anayeitwa Yehova anayeishi mbinguni, naye humtazama na anaelewa vizuri mateso anayopitia kuliko  mtu yeyote yule. Yehova anamjali na angetaka kumwondolea mateso hayo. Hiyo ndiyo sababu amemtuma Shahidi wake amtembelee. Mwanzoni Hirofumi hakuonyesha hisia zozote; kisha akaushika kwa nguvu mkono wa ndugu huyo, na kuanza kutiririkwa na machozi. Ndugu huyo aliguswa sana moyo, naye akatokwa na machozi pia. Funzo la Biblia likaanzishwa.

Baada ya kujifunza kwa miaka 11, Hirofumi alianza kushirikiana na kutaniko lililokuwa karibu badala ya kusafiri mbali hadi kwenye kutaniko la lugha ya ishara kama alivyokuwa akifanya. Hakuna mtu aliyejua lugha ya ishara katika kutaniko hilo, lakini katika kipindi cha miezi 18 iliyofuata, ndugu na dada 22 walijifunza lugha ya ishara ili wamsaidie Hirofumi. Mnamo Januari 2012, Hirofumi alitoa hotuba yake ya kwanza katika Shule ya Huduma  ya Kitheokrasi huku mhubiri fulani akitafsiri ishara zake. Mnamo Oktoba mwaka huohuo, alistahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa.

Anajifunza na Walinzi

Floren, painia anayeishi nchini Filipino, anawafundisha Biblia watu 25 hivi, na wengi wao ni walinzi. Mara nyingi, wanaume hao hufanya kazi saa za usiku, na baadhi yao hufanya kazi usiku mzima. Kwa sababu hiyo, Floren analazimika kubadilikana kulingana na hali. Floren huenda mahali wanapofanyia kazi walinzi hao na kujifunza nao wakati wa mapumziko au wakati mwingine unaofaa bila kuvuruga kazi yao. Yeye huongoza mafunzo fulani kati ya saa 1:00 na saa 5:00 usiku, na mengine kati ya 11:00 alfajiri na 3:00 asubuhi. Wakati mwingine huwa anafika wakati walinzi wanakaribia kubadilishana zamu. Kwa kufanya hivyo, anaweza kujifunza na mlinzi ambaye yuko karibu kuanza zamu yake, kisha ajifunze na yule ambaye amemaliza zamu yake. Floren anasema, “Kujifunza na watu wengi kumeniletea shangwe ambayo sijawahi kupata maishani.” Baadhi ya walinzi hao sasa wanahudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme. Mmoja wao tayari amebatizwa na kama Floren, anatumikia akiwa painia wa kawaida.

Filipino: Floren akiongoza funzo la Biblia asubuhi na mapema

Walitenda kwa Ujasiri

Walipokuwa wakihubiri siku moja yenye mvua, dada wawili nchini Armenia walimwona mama na binti yake barabarani na wakawapa trakti. Dada hao walishangaa mama huyo anayeitwa Marusya alipowaambia kwamba yeye na binti yake, Yeva, wamekuwa nje kwa saa mbili licha ya mvua wakitumaini kuwa watakutana na Mashahidi wa Yehova. Kwa nini walitaka kukutana na Mashahidi? Ndugu ya Marusya alikuwa amefundishwa kweli akiwa gerezani na ndugu ambao walikuwa wamefungwa kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote.  Marusya alitarajia kwamba ndugu yake angetoka gerezani akiwa sugu na mjeuri. Badala yake, alikuwa mwenye usawaziko na mtulivu sana. Kadiri ndugu ya Marusya alivyoendelea kushirikiana na Mashahidi, ndivyo alivyofanya mabadiliko yanayofaa maishani. Hilo lilimshangaza Marusya na binti yake kwa sababu mara nyingi waliona mabango, na pia vipindi vya televisheni vilivyokusudiwa kuwaharibia jina Mashahidi wa Yehova. Yeva alijiuliza hivi: ‘Mjomba wangu ni mtu mzuri sana. Basi ni kwa nini watu wanawasema vibaya Mashahidi wa Yehova?’ Akiwa ameazimia kupata jibu ya swali hilo, alimwambia mama yake hivi: “Hatutajua ukweli kuhusu watu hao ikiwa hatutatenda kwa ujasiri. Twende sasa hivi tukawatafute Mashahidi ili tuache kujiuliza-uliza maswali.” Hivyo ndivyo walivyokuwa wakifanya siku waliyokutana na dada hao. Siku mbili baadaye, dada hao walianza kujifunza Biblia na mama huyo pamoja na binti yake. Walianza kuhudhuria mikutano na wamefanya maendeleo na kuwa wahubiri ambao hawajabatizwa.

Watoto Walimletea Magazeti

Istanbul, Uturuki: Ndugu akitumia broshua Habari Njema anapohubiri barabarani

Jijini Adana, Uturuki, mwanamke mmoja alikuwa na matatizo mengi ya kibinafsi na ya familia hata alifikiria kujiua. Siku moja alipata magazeti yetu mawili mlangoni. Inaonekana kwamba watoto fulani wa majirani waliyaokota sakafuni na kuyaweka mlangoni pake wakidhani ni yake. Mwanamke huyo alivutiwa sana na masimulizi ya maisha yaliyoandikwa katika magazeti hayo, na akatamani kwamba maisha yake yangebadilika na kuwa kama ya watu waliosimuliwa. Mwanamke huyo alipiga nambari ya simu iliyoandikwa katika mojawapo ya magazeti hayo na akawasiliana na dada mmoja painia aliyeishi karibu naye. Funzo la Biblia lilianzishwa. Mwanamke huyo alithamini sana mambo aliyokuwa akijifunza na akasema kwamba angependa kuhudhuria mikutano. Jambo la kupendeza ni kwamba  nyumba yake ilikuwa karibu na Jumba la Ufalme. Mara moja alianza kuhudhuria mikutano na anaendelea kufanya hivyo.

Siku Kumi Gerezani Hazikubadili Msimamo Wake

Bam, anayeishi nchini Nepal alikuwa polisi aliyependa kwenda kanisani. Siku moja alipokuwa kazini, alikutana barabarani na wenzi wa ndoa ambao ni mapainia wa pekee. Alivutiwa sana na jinsi walivyojibu maswali yake yote kwa kutumia Biblia. Bam alikubali funzo la Biblia, na punde si punde akaanza kuhudhuria mikutano. Alipoendelea kujifunza, dhamiri yake ilianza kumsumbua kuhusu kazi yake, kwa hiyo aliwaomba wasimamizi wake wampe kazi ya ofisini ambayo haingehitaji abebe silaha. Wasimamizi wake walikubali. Hata hivyo, baada ya kuhudhuria kusanyiko la wilaya, dhamiri ya Bam ilianza kumsumbua tena, na hivyo akaamua kuacha kazi ya polisi.

Mke wa Bam hakupendezwa na uamuzi wake kwa kuwa polisi aliheshimiwa sana na watu, alipata mshahara mkubwa, marupurupu na malipo mazuri ya uzeeni. Ili kumshawishi abadili msimamo, mke wake alimwambia hivi, “Ukiendelea kuwa polisi, nitajifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.” Kwa kuwa mbinu hiyo haikufaulu, alimshinikiza msimamizi wa kituo hicho amfunge Bam gerezani akitarajia kwamba kifungo hicho kitamfanya abadili msimamo wake. Baada ya kukaa gerezani kwa siku kumi, Bam aliachiliwa, lakini bado alikuwa ameazimia kutafuta kazi nyingine. Alianza kufanya kazi ya kuendesha baiskeli yenye magurudumu matatu iliyomlazimu afanye kazi kwenye jua kali na kwa saa nyingi. Licha ya hali hiyo ngumu, alikuwa na furaha. Alifanya maendeleo ya kiroho na kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Baada ya muda, mke wake aliacha kumpinga. Kwa sababu ya fadhili alizoonyeshwa na ndugu na dada kutanikoni, alianza kujifunza. Bam  anaendelea kuiandalia familia yake mahitaji yao, na anapata pesa nyingi kuliko zile alizokuwa akipata alipokuwa polisi. Alibatizwa kwenye kusanyiko mnamo Februari 2013, na sasa mke wake na mwana wao wanaandamana naye kwenye mikutano.

Nepal: Bam alipobadili kazi yake, yeye na familia yake walifanya maendeleo ya kiroho

 

Alitaka Kuwa Painia Msaidizi

Myeong-hee, dada anayeishi Korea, ana tatizo kwenye mguu wake mmoja kwa sababu ya ugonjwa wa kupooza aliopata alipokuwa na umri wa miaka miwili. Yeye huchoka haraka na mara nyingine huanguka chini. Isitoshe, mara kwa mara hupatwa na hofu ya ghafla na madhara mengine yanayosababishwa na dawa anazotumia. Myeong-hee ana matatizo ya kupumua, na mkazo na wasiwasi humfanya ahisi maumivu. Licha ya matatizo hayo, Myeong-hee alitaka kuwa painia msaidizi na amefanya hivyo karibu kila mwezi kwa kipindi cha miaka miwili iliyopita. Anamshukuru Yehova kwa kumpa nguvu za kutimiza huduma yake.

“Nimekuwa Nikikitafuta kwa Miaka 30!”

Agnes, mmishonari nchini Indonesia, alikuwa akimhubiria mwanamke fulani wa makamo ambaye alikuwa akitazamia kujifungua. Mwanamke huyo alifanya biashara ya kuuza mboga sokoni. Alipenda sana kusoma magazeti yetu na alifurahia mazungumzo yanayohusu Biblia wakati ambao hakuwa na shughuli nyingi. Siku moja Agnes alipoenda kumtembelea mwanamke huyo sokoni, hakumpata. Mume wa mwanamke huyo alimwambia Agnes kwamba mke wake alikuwa amejifungua. Agnes aliamua kumtembelea. Alimpelekea Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kikiwa kimefungwa vizuri kama zawadi. Mwanamke  huyo alifurahi na kushangaa kwamba Agnes alifunga safari ili kwenda kumwona yeye na mtoto wake, lakini alishangaa hata zaidi Agnes alipompa zawadi. Mwanamke huyo alifungua zawadi hiyo na kwa mshangao akamwuliza Agnes: “Umepata wapi kitabu hiki? Nimekuwa nikikitafuta kwa miaka 30! Nilienda kwenye maduka yote ya vitabu na kuwauliza watu. Lakini hakuna mtu aliyekuwa nacho wala kukijua, na sijawahi kuona kitabu kizuri kama hiki.” Mwanamke huyo alipokuwa mtoto, mjomba wake alikuwa na kitabu Hadithi za Biblia na mwanamke huyo alipenda sana kukisoma. Sasa mwanamke huyo anakisoma tena kitabu hicho, na binti yake mkubwa anapenda kusoma kitabu hicho pia. Agnes alianza kujifunza Biblia pamoja na mwanamke huyo na binti yake.

Indonesia: Agnes akiwa ameshika zawadi ya kitabu alichompa mtu